Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Tuesday 1 July 2014

MWACHENI RAIS KIKWETE ASAFIRI, ANATULETEA VIBABA JAMANI MWE…!



  



Na Daniel Mbega, Iringa

“Bajeti ya safari za Kikwete nje yapaa!”, “Safari za Kikwete zakausha Hazina!”, “Mabilioni yafyekwa safari za Kikwete!” Hivi ni baadhi tu ya vichwa vya habari ambavyo vimekuwa vikipamba vyombo vya habari hapa nchini kuzungumzia kuhusu safari zinazofanywa na Rais Jakaya Mrisho Kikwete nje ya nchi.
Naam, na safari hizo zimezua mijadala mingi tangu mwaka 2009 (kama sikosei) wakati hoja za tuhuma za ufisadi hasa wa Richmond/Dowans zilipofifia na Watanzania wakaanza kuzijadili ziara hizo.
Wakati wa kusoma Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2014/2015 pale Mjengoni Dom, tukaambiwa kwamba katika bajeti iliyopita, yaani ya mwaka 2013/14, safari za Rais zilitengewa Sh15 bilioni lakini inaonekana fedha zilizotumika ni nyingi zaidi maana ndani ya miezi miwili tu zote zilikuwa zimemalizika!
Kwa hiyo basi, wabunge wakapiga kelele, kama kawaida ya walio wengi wanaotaka kuzibwa midomo, na kelele zao zikazaa matunda na Sh11 bilioni kati ya Sh50 bilioni zilizokuwa zimetengwa kwa safari za Rais, zikapigwa panga. Hivyo zitakazotumika kwa mwaka wa fedha ujao kabla ya kuelekea katika uchaguzi mwingine (Uchaguzi Mkuu) ni Sh39 bilioni!
Tena basi kiasi kilichobakizwa ni ongezeko la asilimia 260 la Sh15 bilioni zilizopitishwa na Bunge kwa mwaka 2013/2014 kwa ajili ya safari za Rais katika mwaka wa fedha uliomalizika Juni 30 mwaka huu. Ongezeko la asilimia 260 katika nchi ambayo akina yakhe wanachakarika kupata mlo mmoja bila mafanikio!
Watu wanapiga kelele kwamba safari za Mheshimiwa JK ni nyingi sana na zinatumia mahela mengi mno. Halafu wanakwenda mbali kwa kumfananisha Rais wetu, ambaye tangu mwaka 2005 alipoteuliwa tu na CCM viongozi karibu wote wa Kiroho walisema ni ‘Chaguo la Mungu’, eti anafanana na Vasco da Gama, yule Mreno ‘mvumbuzi’ aliyesafiri katika bahari zote na kuwa Mzungu wa kwanza kufika Bara Hindi!
Watanzania mbona mnamkosea adabu Rais? Mtamfananishaje na mtu anayedai kuvumbua Ras ya Tumaini Jema wakati ipo barani mwetu? Mtamfananishaje na mtu ambaye kupitia biashara zake alisaidia uchumi wa Ureno – uliokuwa ukitegemea tu biashara ya Afrika Magharibi na Kaskazini pekee – kukua kwa kasi baada ya kuanzisha njia za kuleta viungo (spices) kutoka India?
Hivi mnathubutuje kuhoji matumizi ya zaidi ya safari 300 za Rais eti tu kwa sababu kuna watu wanakosa hata mlo mmoja? Hivi mnadhani hao wakifa kwa njaa walioko wizarani nao watakufa?
Nasikia watu wanalalamika tu kuhusu kubana matumizi na mambo kama hayo. Nawashangaa sana. Bajeti yetu inategemea mapato ya ndani ya bangi na gongo (samahani – namaanisha sigara na pombe), na sehemu kubwa inategemea fedha za wafadhili.
Hivi mnadhani Rais akikaa pale Magogoni tu na Mwalimu, hao wafadhili wanaweza kuchota mahela na kuyamwaga bila kusikia mahitaji yetu? Si lazima Baba yetu asafiri akawaambie mahitaji yetu ni nini na tumepungukiwa wapi?
Msihoji kuhusu mabalozi wetu walioko huko bwana, hivi unajua akienda mkuu wa nchi kunakuwa na uzito mkubwa?
Mnazungumza tu kuhusu shughuli za maendeleo bila hata kuwa na kumbukumbu sahihi. Hivi maendeleo gani mnayoyazungumzia wakati JK amekuta viwanda vyote vimeuzwa, tena wengine wamejiuzia wakiwa pale pale Magogoni? Yako wapi mashirika ya umma yaliyoanzishwa na Mwalimu? Sasa mnataka JK akae tu na kuona maendeleo yakishuka wakati hakuna vyanzo vingine vya mapato?
Enhe! Mapato yenyewe yapi wakati wanaolipa kodi ni makabwela tu kupitia kwenye bidhaa za mabwanyenye wanaokwepa kulipa hizo kodi!
Unajua nashangaa sana wakati hoja za safari za JK zinapotolewa. Najiuliza hata sipati majibu kama wanaosema wako makini au la.
Mtanzania gani anayeweza kuwekeza bila kuwa na msaada kutoka nje au kuingia ubia na wenye pua ndefu? Serikali yenyewe inaingia ubia, halafu mnataka Rais asisafiri, hao wabugiaji na wakwapuaji watakuja vipi nchini kama hawakuelezwa mazingira yalivyo?
Semeni tu nyie wenyewe, kuna miradi mingapi iliyoanza kutajwa kwa miaka 20 sasa na haijatekelezwa? Mingi imetengewa fedha, zimeliwa na wajanja wachache, lakini kutokana na umakini wa Rais, ndiyo maana anasafiri kwenda nje kutafuta misaada zaidi ili kuziba mapengo, japo siamini kama jino la pembe linaweza kuwa dawa ya pengo.
Kusema ukweli ni kwamba, safari za JK nje ya nchi zina manufaa makubwa sana kwa Tanzania, wanaopinga yawezekana ni vipofu, hawaoni, lakini pia ni viziwi, hawasikii, wamebaki kubwabwaja tu.
Hivi hamjui kwamba Rais ndiye Msimamizi Mkuu wa sera za ndani na nje ya nchi, hivyo sehemu zote mbili zinahusiana moja kwa moja na usimamizi na utekelezaji wake? Halafu msihoji amekwenda mara ngapi nje ya nchi, wakati wowote kunapokuwa na umuhimu wa kufanya hivyo anakwenda tu.
Si mliambiwa jamani kwamba ziara yake ya Uchina mwaka 2008 ilivyokuwa na mafanikio kwa kufuta deni la Dola 315 milioni za Marekani? China ikaahidi kusaidia uanzishwaji maeneo makubwa ya maendeleo ya kiuchumi na kutoa Yuan 80 milioni, ikaahidi kutoa Yuan 20 milioni kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha kisasa cha mikutano cha Julius Nyerere (makubaliano tayari yamefikiwa na uzinduzi uefanyika hivi karibuni) na shughuli za maendeleo Zanzibar, ikaahidi kuanzisha ushirikiano wa masuala ya anga na safari za ndege kati yake na Tanzania japokuwa Shirika letu la ndege limekufa na hatuna ndege, ikafuta deni la Dola 500,000 za Marekani za reli ya Tazara pamoja na kuahidi kujenga shule za kisasa za mfano za msingi na sekondari.
Wanaodai kwamba Rais Kikwete anatumia muda mwingi nje ya nchi hawajui tu kwamba huyu baba yetu anakwenda kutuombea vibaba. Wawekezaji waliojaa tele nchini wametokana kwa kiasi kikubwa na jitihada zake.
Tanzania haiwezi kufahamika zaidi baada ya Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere ikiwa Rais Kikwete atabaki Magogoni tu, lazima azunguke huku na kule na kuhudhuria mikutano na dhifa mbalimbali ili hata hao wafadhali wamuone na wajue kwamba Tanzania ipo.
Nyie mnataka azunguke aende Ukerewe akaangalie wavuvi wanaohitaji msaada? Atakwendaje mikono mitupu jamani, lazima muwe waelewa kidogo.
Kumbukeni kwamba Rais ana ndege kubwa ambayo haiwezi kutua pale Ukerewe, na ndege ile ilinunuliwa kwa fedha kiduchu tu (Pauni 15 milioni) wakati wa Ben Mkapa ili isafiri angani, sasa mnataka ikae pale uwanjani halafu vyuma viote kutu eboh!
Kumbukeni tu wakati ule yule waziri alisema kwamba (wakati analazimisha kununua kwa sababu kuna waliopinga pia), kwamba ndege hiyo itanunuliwa hata kama itawalazimu Watanzania kula mihogo! Unadhani ilikuwa inanunuliwa ili liwe pambo!
Hivi mnafahamu kwamba Wamarekani hawazijui nchi nyingi za Kiafrika kwa majina, hivyo Rais wetu anapokwenda huko mara kwa mara maana yake sasa wanaelewa kuwa kuna Tanzania. Hamuoni fahari kwa Tanzania kutembelewa na marais wawili wa Marekani walio madarakani? Unadhani ni heshima ndogo hiyo?
Nyie hamjui tu, Watanzania wanaoishi Marekani wanayo fursa ya kuitangaza Tanzania, na wako wanaofanya hivyo, kwa kadiri ya uwezo wao. Lakini Rais Kikwete anapokwenda, suala hilo linakuwa na mafanikio makubwa zaidi. JK ana mvuto wa kipekee bwana.
Siyo siri, safari za JK zina umuhimu mkubwa sana katika kuitangaza Tanzania kuliko kama angekwenda mbunge au waziri kama wanavyotaka baadhi ya Watanzania. Siyo rahisi mbunge au waziri aende Marekani aweze kuwavuta watu kama anavyowavuta JK.
Na lazima mkumbuke kwamba, kuna mambo ambayo mabalozi wanayafanya na mengine yanafanywa na mawaziri. Si tumesikia jinsi waziri wa mambo ya ughaibuni anavyokusanya fedha kwa ajili ya uchaguzi mkuu akisema kwamba ametumwa na Rais! Ingawa amekanusha, lakini tumesikia kwanza. Naam, anamsaidia Rais katika mambo mengi.
Kwa hiyo mambo ya kuomba vibaba ni jukumu la baba mwenyewe, siyo kutuma watoto bwana! Unajua mtoto anapokwenda kwa jirani kuomba chakula hawezi kueleweka, tena wanaweza kumwambia “…Kaa hapa ule, ushibe, halafu pangusa mdomo… ukimaliza kawaambie hata kwa jirani hakuna!” Lakini baba akienda na macho makavu, hata akikaribishwa mezani anaweza kukataa kula kwa sababu anawafikiria watoto wake – sisi Watanzania. Mzazi mwema anaanza kuifikiria njaa ya watoto kabla hajajifikiria mwenyewe. Ndivyo anavyofanya Rais wetu, mnaompinga mna inda, fitna na tadi, hamna lolote nyie!
Nataka niwaambie tu wale wanaoziponda safari za JK kwa kufananisha na zile za Mwalimu Nyerere au hata za Obama kwamba hawana pointi ya msingi. Zama za Nyerere zilikuwa za analojia, hizi ni zama za kidijitali bwana. Nyerere hakutaka ardhi ichimbuliwe kutafuta madini, wala hakutaka wanyamapori wetu wachezewe ovyo ovyo, lakini sasa si mnaona mashimo makubwa tuliyoachiwa na wawekezaji wachimba madini wanaoacha fedha kiduchu? Si mnaona wawekezaji katika sekta ya maliasili wanavyotumia fedha kuwafukuza hata wazawa kwenye maeneo yao ya asili? Tena wengine wanachukua na wanyama hai kwenda kuwafuga kwao.
Mnataka kusema hawa watu wangekuja namna gani ikiwa hakuna utaratibu ‘mzuri’ wa kuwakaribisha na kuwaacha wafanye watakavyo?
Obama huwezi kumfananisha na JK hata kidogo, kwanza yeye hatakiwi hata kusafiri kwa sababu taifa lake ni imara, lina uchumi imara na wanachofanya ni kulinda maslahi yao, kazi ambayo wanaweza kuifanya mabalozi wao tu. Anaposafiri ni kwa sababu maalum, yeye hahitaji msaada kama sisi tunavyouhitaji. Mgonjwa humtafuta daktari, lazima sisi wenye njaa tukaombe misaada na tuwakaribishe wawekezaji.
Si mnakumbuka ziara mojawapo ya Rais Kikwete ya Marekani ambayo ilisaidia tukapewa msaada wa Dola 700 milioni kupitia Mfuko wa Changamoto za Milenia (MCC) ili kupambana na Malaria (mfano kupatiwa madawa, chanjo na vyandarua ambavyo baadhi yenu mkatumia kwenye bustani). Si fedha hizi pia ambazo zilisaidia ujenzi wa barabara za Mtwara-Masasi- Tunduru- Songea hadi Mbamba Bay, na ile ya Tunduma hadi Sumbawanga?
Ziara yake ya Uchina si mnaona ilivyozaa matunda jamani mwaka jana? Tumewapa Wachina Mchuchuma na Liganga, tukaingia mikataba 17 iliyosainiwa pale Dar es Salaam usiku tena Rais wa China, Xi Jinping, akiwa ameiteua Tanzania miongoni mwa nchi nne tu alizozuru Afrika! Hamuoni kwamba hiyo ni sifa kubwa?
Mheshimiwa Rais, nadhani hawa wivu unawasumbua ndiyo maana wamesahau, kwamba wewe siyo mgeni ‘kuvunja majeti’ na kwenda Ulaya. Umesafiri sana wakati wa enzi ya Mzee wa Ukapa ukiwa waziri wa nje, au wamesahau kwamba kwa miaka kumi yote ulikuwa pale jirani na Magogoni?
Rais Kikwete wewe mtoto wa mjini bwana, kamwe usitishwe na kelele za watu kuhusu safari zako. Endelea kuvunja majeti na kukata upepo angani, ilimradi unatuletea vibaba vya unga. Kwanza miezi yenyewe imebaki michache kabla hujaondoka Magogoni, wanataka usafiri utakapostaafu?
Kanyaga twende! Ni mawazo yangu tu... washkaji msijenge chuki!



0656-331974

No comments:

Post a Comment