Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Monday, 17 August 2015

UKAWA WAKISHINDA KUJA NA SERIKALI TATU, MUUNGANO WA SASA KWAHERI




Na Daniel Mbega

MCHAKATO wa kutafuta Katiba Mpya utaendelea endapo Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) utatwaa Dola Oktoba mwaka huu, imefahamika.
Taarifa kutoka ndani ya Ukawa zinaeleza kwamba, umoja huo utaipitisha Rasimu ya Pili ya Katiba iliyotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba ambayo inapendekeza muundo wa Muungano wa Serikali Tatu.
Rasimu hiyo ya Tume ya Warioba ilipendekeza muundo wa Serikali Tatu, ambapo ile ya Muungano itakuwa ya mkataba badala ya mfumo wa sasa ulivyo.
Hali hiyo inatasfiriwa kwamba, ushindi wa Ukawa ndio utakuwa mwisho wa Katiba Pendekezwa ambayo ilikuwa ipigiwe kura ya maoni mwaka huu kabla ya kuahirishwa.
“Chanzo cha Ukawa ni kutetea ‘Katiba ya Wananchi’ ambapo wapinzani tuliungana pamoja kuiafiki Rasimu ya Pili ya Katiba kama ilivyowasilishwa na Jaji Joseph Sinde Warioba aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, hivyo tukitwaa Dola, lazima tuwatendee haki Watanzania kwa kuwapa kile wanachokitaka,” alisema mbunge mmoja wa Chadema ambaye aliomba hifadhi ya jina lake kwa kuwa siyo msemaji.
Mbunge huyo amesema sababu ya wao kususia vikao vya Bunge Maalum la Katiba tangu Aprili 2014 ni kupinga hila za Chama cha Mapinduzi za kuichakachua Rasimu ya Pili ya Katiba kwa kuwa ilikuwa inawabana viongozi wa Serikali ya chama hicho.
Mnamo Jumatatu Machi 17, 2014 wabunge wa upinzani walianza kupinga mchezo mchafu uliofanyika baada ya Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Samuel Sitta, kumruhusu Jaji Joseph Sinde Warioba (Mwenyekiti wa Tume ya Marekebisho ya Katiba), awasilishe Rasimu ya Katiba hiyo Bungeni kabla ya
Rais Jakaya Kikwete kulihutubia Bunge hilo.
Hali hiyo iliwalazimu wabunge waliokuwa wanaunda Ukawa kutoka vyama vya Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi, UDP, DP, Chausta, Chauma,NRA, NLD na CCK pamoja na wajumbe walioteuliwa kutokana na makundi yaliyotajwa katika kifungu cha 22(1)(c) cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, kutoka nje.
Hata hivyo, wabunge wa vyama vya Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na NLD waiamua kususa moja kwa moja vikao baada ya kutoka nje ya Bunge hilo mnamo Jumanne Aprili 15, 2014 na tangu hapo hawakuhudhuria tena.
Baada ya hapo wabunge wote wa Ukawa wakaanza ziara ya nchi nzima na kufanya mikutano ya hadhara kueleza namna CCM ilivyokuwa inaichakachua Rasimu hiyo, mikutano ambayo baadaye ikazaa makubaliano ya kusimamisha mgombea mmoja wa urais.

Tume ya Katiba
Ikiwa Ukawa wataingia madarakani na kurejea Rasimu ya Pili, watakuwa wamenusuru takriban Shs. 60 bilioni zilizotumiwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba katika michakato mbalimbali, ikiwemo posho za wajumbe.
Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilikuwa na wajumbe 34 na iliundwa chini ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Sura 83, Toleo la 2012, Vifungu 5, 6 na 7 ambapo Mwenyekiti wake alikuwa Jaji Warioba na Makamu Jaji Mkuu mstaafu Augustino Ramadhan.
Wajumbe waliokuwa wanaonda Tumehiyo kutoka Tanzania Bara walikuwa Profesa Mwesiga Baregu, Riziki Shahari Mngwali, Dk. Edmund Sengodo Mvungi (sasa marehemu), Richard Shadrack Lyimo, John Nkolo, Alhaj Said El-Maamry, Jesca Sydney Mkuchu, Prof. Palamagamba Kabudi, Humphrey Polepole, Yahya Msulwa, Esther Mkwizu, Maria Malingumu Kashonda, Aly-Shymaa John Kwegyir (MB), Mwantumu Jasmine Malale na Joseph Warioba Butiku.
Wajumbe kutoka Zanzibar walikuwa Dk. Salim Ahmed Salim, Fatma Said Ali, Omar Sheha Mussa, Raya Suleiman Hamad, Awadh Ali Said, Ussi Khamis Haji, Salma Maoulidi, Nassor Hamis Mohammed, Simai Mohammed Said, Muhammed Yussuf Mshamba, Kibibi Mwinyi Hassan, Suleiman Omar Ali, Salama Kombo Ahmed, Abubakar Mohammed Ali na Ally Abdullah Ally Saleh.
Aidha, Uongozi wa Sekretarieti ya Tume hiyo ulikuwa na Assaa Ahmad Rashid (Katibu) na Casmir Sumba Kyuki (Naibu Katibu).
Bunge la Bajeti liliwahi kuidhinisha Sh. 33.944 bilioni mwaka 2012/2013na kiasi kama hicho kikaombana Wizara ya Sheria na Katiba kwa mwaka 2013/2014 kwa ajili ya matumizi ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Kiasi cha Sh. 33.944 bilioni kilichoombwa mwaka 2013/2014 kilihusisha Sh. 12.193 bilioni kwa ajili ya posho za vikao kwa wajumbe wa Tume 34 na Sekretarieti 160; Sh. bilioni 1.728 za posho ya kujikimu kwa ajili ya wajumbe na Sekretarieti wanaposafiri ndani ya nchi kikazi; na Sh. bilioni 1.650 kwa ajili ya kulipa gharama za nyumba za wajumbe na Sekretarieti wanaotoka nje ya Dar es Salaam.
Pia Sh. 18 milioni ziliombwa kwa ajili ya kughariamia chakula kwa wajumbe wa Tume na Sekretarieti watakaokuwa wamepata maambukizi ya Ukimwi; Sh. 60 milioni kwa ajili ya usafiri wa ndani; Sh. 50 milioni kwa ajili ya gharama za malazi kwa wajumbe wa Tume na Sekretarieti ‘wanaposafiri kikazi’; Sh. 423 milioni kwa ajili ya ‘chai na vitafunwa’; na Sh. 50 milioni kwa ajili ya wahudumu wanaosaidia kazi za Tume wakiwa mikoani wakati wa kushiriki kwenye Mabaraza ya Katiba na zoezi la upigaji kura ya maoni.
Aidha, kulikuwa na maombi ya Sh. 19.039 bilioni nyingine kwa ajili ya posho za aina mbalimbali na malipo mengine yanayowahusu wajumbe na Sekretarieti ya Tume kwa mwaka wa fedha 2013/14.
Wizara iliomba Bunge liidhinishe Sh. 60 milioni kulipia maji kwa matumizi ya ofisi za Tume; Sh. 30 milioni kwa ajili ya kulipia gharama za usafiri wa basi na teksi kwa wajumbe na Sekretarieti watakaposafiri ndani ya nchi kikazi; Sh. 103 milioni kwa ajili ya kulipia gharama za simu za mikononi; na Sh. 604 milioni kwa ajili ya posho kwa wajumbe wa Tume na Sekretarieti wakati wa Bunge Maalum la Katiba.

Wajumbe wa kawaida wa Tume kwa mujibu wa mchanganuo wa bajeti, walikuwa wanalipwa Sh. 200,000 kama posho ya vikao kwa siku. Maofisa waandamizi wa Tume hiyo walikuwa pia wanalipwa posho ya Sh. 200,000 kwa siku, maofisa wa kati walikuwa wanalipwa Sh. 150,000 kutwa na maofisa wa ngazi za chini walikuwa wanalipwa Sh. 100,000 kwa siku kulingana na taratibu za Serikali.

Bunge Maalum la Katiba
Bunge hilo lilikuwa na wajumbe 640 likijumuisha wabunge wote 357 wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, wajumbe 82 wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar pamoja na 201 kutoka kwenye makundi mbalimbali.
Makundi hayo na idadi ya wajumbe kwenye mabano ni Taasisi zisizo za Kiserikali (20), Taasisi za Dini (20), Vyama vya Siasa (42), Taasisi za Elimu (20), Makundi ya Walemavu (20), Vyama vya Wafanyakazi (19), Vyama vya Wafugaji (10), Vyama vya Wavuvi (10), Vyama vya Wakulima (20) na Makundi yenye Malengo yanayofanana (20).
Bunge hilo, ambalo lilisusiwa na wapinzani kwa uchakachuaji wa rasimu, lilianza Februari 18, 2014 likiwa limepangiwa kufanyika kwa siku 90, na linatajwa kwamba lilitumia gharama kubwa kiasi cha Shs. 192 bilioni kwa posho tu za wajumbe mbali ya gharama nyingine za uendeshaji.
Ikiwa Ukawa wataamua kuirejea Rasimu ya Pili kama ilivyo, gharama za Bunge Maalum la Katiba zitakuwa zimekwenda na maji na kwamba fedha nyingine zaidi zitalazimika kutengwa ili kuitisha kikao kingine cha Bunge Maalum kuijadili upya rasimu hiyo.
Vipo vikwazo vingi vilivyoleta mgongano wakati wa mjadala wa rasimu hiyo ya pili, lakini kikubwa zaidi ni hoja ya Muundo wa Muungano wa Serikali Tatu ambao CCM waliupinga kwa nguvu zote kwa mtazamo kwamba ungeua muungano wa sasa.
Hoja nyingine ni vipengele vya kuwabana viongozi wa kuchaguliwa, wakiwemo Rais na Wabunge, na kwamba Rais anaweza kupigiwa kura ya kutokuwa na imani naye hata akiwa madarakani na pia anaweza kushtakiwa.
Wananchi wengi walionekana kuunga mkono rasimu hiyo ya pili wakiwanaimani kwamba wanaweza kuwawajibisha wawakilishi wao na hivyo maendeleo kupatikana.


CHANZO: GAZETI LA WAJIBIKA, AGOSTI 17, 2015

No comments:

Post a Comment