Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Sunday 23 August 2015

CHADEMA KAMA CCM, TAZAMA ILIVYOWACHAKACHUA WASHINDI KURA ZA MAONI

 Esther Bulaya - Bunda Mjini
Ansbert Ngurumo - Muleba Kaskazini
 Fred Mpendazoe - Kishapu
 Njelu Kasaka - Lupa
 Said Nkumba - Sikonge
 Mwita Mwikwabe Waitara - Ukonga

Na Daniel Mbega
CHADEMA imekifanya kile ambacho imekuwa ikituhumu kufanywa na Chama cha Mapinduzi (CCM) – upendeleo na kushindwa kukubali maoni ya wananchi walio wengi.
Chama hicho kimewabwaga makada 12 walioshinda kura za maoni na kuwapitisha wengine ambao walishindwa, uamuzi ambao umechukuliwa na wachambuzi wa mambo ya siasa kama wa ‘upendeleo’ na hauna tofauti na utaratibu wa CCM wa miaka yote wa kuangalia pia sifa mbalimbali ikiwemo mchango wao kwa chama, uadilifu na uwezo katika utendaji.
Baadhi ya waliobebwa na ‘mbeleko ya chuma’ ya Chadema ni Esther Bulaya, Fred Mpendazoe, Njelu Kasaka, Mwita Mwikwabe Waitara, Michael Aweda na Ansbert Ngurumo ambao wamekuwa miongoni mwa wateule 138 waliosimamishwa na chama hicho baada ya mgawanyo wa majimbo kwa vyama vyote vinavyoundwa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Idadi hiyo ni asilimia 54 ya majimbo 253 ambayo umoja huo umesimamisha wagombea kati ya majimbo yote 265 nchini.
Mgawanyo huo unaonyesha kwamba Chama cha Wananchi (CUF) kimesimamisha wagombea 99 sawa na asilimia 29 (yakiwemo majimbo 49 ya Zanzibar), NCCR-Mageuzi yenyewe imesimamisha wagombea 14 (sawa na asilimia 5.5) na NLD imesimamisha wagombea watatu (sawa na asilimia 1.2).
Uchunguzi uliofanywa na www.brotherdanny.com unaonyesha kwamba, katika Mkoa wa Mara, Chadema imembeba aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum (Vijana) wa CCM, Esther Bulaya kwa kumteua kugombea Jimbo la Bunda Mjini licha ya kushindwa vibaya katika kura za maoni kwa kushika nafasi ya tatu.
Katika uchaguzi huo wa kura za maoni Chadema, Bulaya alipata kura 37 nyuma ya mshindi Pius Masururi aliyepata kura 61 na Magembe Makoye aliyepata kura 40. Wengine walikuwa Frank aliyepata kura 35, Maganja (5) na Jane na Chacha Nyamhanga ambao hawakuambulia hata kura moja.
Lakini Bulaya alikuwa ameshinda kwenye Viti Maalum katika jimbo hilo kwa kupata kura 71 na kuwazidi Godliver Masamaki (31), Joyce Sokombi (4), Minza Shani (3), Dk. Jane Nyamsenda (1) na Alice Wandya (0).
Baadhi ya wanachama wa Chadema mkoani humo walikuwa wakipinga uamuzi wa chama hicho ‘kumzawadia’ Bulaya ubunge wakati kuna watu ambao walifanya kazi kubwa kukijenga chama.
Bulaya sasa atapambana na ‘babu’ Steven Wasira katika jimbo hilo, ambalo wachunguzi wa siasa wanaeleza kwamba ‘lilitengenezwa’ kwa ajili yake akiwa CCM, na kuondoka kwake kunaonekana kama ni ‘ukorofi’ ambao utakuwa mtaji wa chama chicho tawala.
Mkoani Simiyu katika Jimbo la Kisesa, Chadema imemteua mshindi wa pili wa kura za maoni Masanja Manani badala ya William Masanja aliyeshinda kwa kupata kura 270. Manani yeye alipata kura 219 wakati wagombea wengine walikuwa Masunga Ndemela (47), Sendama W. Hunge (16), Matondo Sebastian (4), Nkwabi Mahona (3), Erasto Kassanga Tumbo na Simon Jilala walioambulia kura mbili kila mmoja.
Katika Jimbo la Itilima mkoani humo, Martin Makondo aliyeshinda kwa kupata kura 377 amepigwa chini na Chadema kumpitisha Martine Magile aliyeshika nafasi ya pili kwa kupata kura 153. Wagombea wengine jimboni humo walikuwa Lucas (18), Mchungaji Machimu (10) na Bahati (8).
Katika Mkoa wa Shinyanga, Chadema imempitisha Fred Tungu Mpendazoe kuwania Jimbo la Kishapu licha ya kushika nafasi ya nne kwenye kura za maoni kwa kuambulia kura 11 tu kati ya wagombea watano waliojitokeza. Mshindi wa jimbo hilo alikuwa Kahema ambaye alipata kura 291, Edmund akapata kura 76 na Pius Singiri alipata kura 27, wakati aliyeshika nafasi ya mwisho alikuwa Dk. Bundu aliyepata kura 6.
Ni Mpendazoe huyu aliwahi kutolewa kafara na kundi la wapinga ufisadi na kutangulizwa kama chambo katika chama ambacho hakikuwa na usajili - Chama cha Jamii (CCJ) - mwaka 2010, akajiuzulu ubunge miezi michache kabla ya Bunge kuvunjwa, CCJ ilipokosa usajili akakimbilia Chadema na kugombea Jimbo la Segerea ambako alishindwa na Dk. Milton Makongoro Mahanga wa CCM. Sasa wanataka 'kumrejeshea jimbo lake'.
Mkoani Mwanza, Chadema imempiga chini Shejamabu aliyeshinda kura za maoni katika Jimbo la Sengerema kwa kupata kura 182 na kumpitisha mshindi wa pili, Hamis Tabasamu aliyeambulia kura 85.
Katika Mkoa wa Kagera, Chadema imefanya kile ambacho kilishaelezwa kupitia kwenye mitandao ya kijamii kwamba Kamati Kuu ingempitisha mwanahabari Ansbert Ngurumo ‘iwe-isiwe’ licha ya kudondoka vibaya kwenye kura za maoni kwenye Jimbo la Muleba Kaskazini.
Kwenye uchaguzi wa kura za maoni, Ngurumo alipata kura 55 tu wakati Najim Kasange alishinda kwa kupata kura 247! Mgombea mwingine, Christina Mwainunu alijitoa kabla ya uchaguzi.
Katika Jimbo la Lupa mkoani Mbeya, Chadema imetumia mbeleko ya chuma kumbeba mwanasiasa mkongwe nchini, Njelu Edward Mlugale Kasaka licha ya kushika nafasi ya pili kwenye kura za maoni kwa kupata kura 45 nyuma ya Miraji Hussein aliyepata kura 65 huku Filipo Mwakibinga akipata kura 32.
Njelu, muasisi waHoja ya Serikali ya Tanganyika Bungeni mwaka 1993, amekuwa akitangatanga tangu aliposhindwa kura za maoni ndani ya CCM mwaka 2010, ambapo alikimbilia CUF, akarudi CCM na baadaye amekimbilia Chadema.
Kwenye Jimbo la Kalenga mkoani Iringa, Chadema imepiga ‘ana-ana-do’ na kumpitisha Mussa L. Mdede na kumwacha Sinkala Lucas kufuatia wagombea hao wawili kupata kura 64 kila mmoja wakati wa kura za maoni. Grace Tendega, ambaye mwaka 2014 aligombea katika uchaguzi mdogo jimboni humo, alishika nafasi ya tatu kwa kuambulia kura 27 na Mwanahamisi Muyinga akapata kura 16.
Huko mkoani Manyara, Chadema pia imecheza tik-tak kwa kumpitisha kada wake wa mirandaoni Michael Petro Aweda badala ya Amani Paul Gaseri.
 Kura za maoni za awali zilionyesha kwamba Gaseri alishinda kwa kupata kura 76 na Aweda akapata 75, lakini katika hali ya kushangaza, ‘eti’ ikabidi uchaguzi urudiwe kwa wagombea hao wawili tu kwa maelezo kwamba Katiba ya chama hicho Ibara ya 6.3.1 (c) inasema: Majina ya wagombea wote wenye sifa zilizotakiwa yatapigiwa kura za siri na kikao kinachohusika na mshindi atapatikana kwa uwingi wa kura usiopungua 50% ya wapiga kura halali waliohudhuria kiako cha uchaguzi!
Ajabu ni kwamba, kati ya waliopitishwa kuwania majimbo hayo, wapo ambao hawakufika hiyo asilimia 50, na kuna wengine ambao walipata kura sawa.
Lakini waliporudia kwa shinikizo na njama za wasimamizi wa uchaguzi huo jimboni humo, Aweda akapata kura 163 na Gaseri 120.
Kwenye uchaguzi wa awali, wagombea wengine na kura zao kwenye mabano walikuwa James Gitonge Sombi (52), Emmanuel Darabe Tippe (39), Michael Tarimo Lorri (29), Yuda Qoryo Gurty (16) na Paschal Awaki Side (0).
Mkoani Dar es Salaam, Chadema iliendelea na sera zile ambazo imekuwa ikiikosoa CCM za kuwabeba watu walioshindwa kwenye kura za maoni kwa kigezo cha kuangalia mchango wao kwenye chama na siyo matakwa ya watu.
Kwenye Jimbo la Ukonga, chama hicho kimempitisha Mwita Mwikwabe Waitara aliyeshika nafasi ya pili kwa kupata kura 49 badala ya Nickson Tugara alishinda kwa kura 59. Wagombea wengine walikuwa Elly Dallas (15), Deogratias Munishi (8), Lucas Otieno (6), Asia Msangi na Deogratias Mramba waliopata kura tano kila mmoja na Gasto Makwetta (1). Wengine saba hawakuambulia kura hata moja.
Aidha, katika Jimbo la Ilala, pia wamembwaga Naomi Kaihula aliyepata kura 34 na kumpitisha Muslim Hassanali Haiderali aliyeshika nafasi ya pili kwa kura 20. Bi. Kaihura ndiye aliyegombea jimbo hilo mwaka 2010 na kushindwa na mgombea wa CCM, Mussa Azzan Zungu.
Katika Mkoa wa Pwani mambo hayakuwa na tofauti pia hasa katika Jimbo la Chalinze ambapo mshindi wa kura za maoni, Chacha Machera aliyepata kura 69 ametemwa na nafasi yake kuchukuliwa na aliyekuwa mshindi wa pili, Mathayo Torongey aliyepata kura 53. Torongey ndiye aliyegombea kwenye uchaguzi mdogo jimboni humo mwaka 2014 na kushindwa na Ridhiwani Kikwete wa CCM.
Huko Morogoro katika Jimbo la Mvomero, Chadema imempitisha mshindi wa pili wa kura za maoni Oswald Mlay aliyepata kura 181 badala ya Owden aliyepata kura 185.


(Imeandaliwa na www.brotherdanny.com. Simu: 0656-331974)

No comments:

Post a Comment