Dk. Abdallah Omar Kigoda - kuwa Waziri Mkuu

Mwigulu Lameck Madelu Nchemba - kuwa Waziri wa Fedha
Celina Ompeshi Kombani - Mazingira
Jenista Joachim Mhagama - Utumishi
WAKATI siku 64 za mtifuano wa kampeni zinatarajiwa kuanza Agosti 22 kwa
mujibu wa ratiba ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), watakaounda Baraza la
Mawaziri la Chama cha Mapinduzi (CCM) baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba 25, 2015 wamekwishaanza kutajwa, imefahamika.
Duru za siasa kutoka chama hicho kikongwe kabisa barani Afrika zinasema,
licha ya vuguvugu kubwa la mageuzi lililopo nchini, lakini wana uhakika wa
kukamata tena dola na sasa wanapanga mikakati madhubuti ya kutetea majimbo yao
na kuyarejesha yaliyotwaliwa na upinzani.
Baraza hilo linaelezwa kuwa na uwiano sawa wa jinsia katika harakati za
CCM kutimiza malengo ya “nusu-kwa-nusu” katika uongozi, kama alivyofanya
mgombea urais Dk. John Magufuli alipomteua Samia Suluhu Hassan kuwa mgombea
mwenza.
Kwa mujibu wa duru hizo, wakati tayari mgombea urais na mwenza wake
wamejulikana, hivi sasa wanaangalia ni nani kati ya makada wake ambaye anaweza
kuwa waziri mkuu baada ya chama hicho kurejea madarakani.
“Baada ya Oktoba Rais ni Dk. (John) Magufuli na makamu wake ni Samia
(Suluhu Hassan), sasa tunaangazia nani atakayeweza kuwa mtendaji mkuu wa
serikali ingawa tayari tumemuona,” kinasema chanzo kimoja ndani ya CCM.
Ingawa chanzo hicho kimegoma kumtaja mtu wanayedhani atakuwa waziri
mkuu, lakini taarifa zinasema, Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk. Abdallah Omar
Kigoda, ndiye anayelengwa kushika wadhifa huo.
“Huyu jamaa ndiye waziri mkongwe kuliko wote, ameshika wizara nyingi na
anaweza kusimamia vyema utendaji wa serikali,” kilieleza chanzo kingine.
Mbali ya Dk. Kigoda, mwingine anayetajwa kukabidhiwa wizara nyeti ya
fedha ni Mwigulu Lameck Madelu Nchemba, ambaye kwa sasa anatetea kiti chake
katika Jimbo la Iramba Magharibi.
Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, Nchemba, ambaye ni naibu waziri wa fedha
anayeshughulikia uchumi, anafaa kupewa nafasi hiyo kwani katika kipindi cha
wiki mbili tu baada ya kuteuliwa aliweza kukusanya kodi zaidi ya Shs. 3 bilioni
kutoka kwa wafanyabiashara wakubwa ambao wanatajwa kwamba wamekuwa wakwepaji
sugu wa kodi.
“Huyu jamaa ndiye hasa anayestahili kukaa kwenye ofisi ile, amewahi
kufanya kazi Benki Kuu na zaidi ni mtendaji, ukiangalia utendaji wake katika
kipindi cha tangu Januari 2014 hadi sasa unaweza kuamini kwamba ndiye hasa
anayefaa,” kilisema chanzo kingine.
Hata hivyo, licha ya baraza hilo kuwa na uwiano sawa wa jinsia, lakini
taarifa zinasema litakuwa na sura nyingi ngeni na wachache wa zamani.
Ifuatayo ni orodha pendekezwa ya baadhi ya wizara za sasa:
Waziri katika Ofisi ya Rais (Utawala Bora): George Huruma Mkuchika,
Mbunge wa Newala ambaye kwa sasa ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu
(Tamisemi).
Waziri Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma): Jenista Mhagama.
Waziri katika Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu): Profesa Jumanne
Maghembe ambaye kwa sasa ni Waziri wa Maji na Umwagiliaji.
Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge): Steven
Masatu Wasira ambaye kwa sasa ni Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika.
Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi): Aggrey Mwanri, Mbunge wa Siha
mkoani Kilimanjaro ambaye kwa sasa ni naibu waziri katika wizara hiyo na
utendaji wake umekuwa ukimfunika hata waziri mwenyewe.
Waziri katika Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira): Celina Ompeshi
Kombani, ambaye amekuwa kwenye baraza la mawaziri kwamuda mrefu.
Waziri katika Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano): Shamsi Vuai Nahodha,
Waziri Kiongozi wa zamani wa Serikali ya Mapinduzi ambaye pia amewahi kuongoza
wizara kadhaa za Muungano zikiwemo Ulinzi na JKT pamoja na Mambo ya Ndani.
Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji na Uwezeshaji): Saada
Mkuya, ambaye alikuwa waziri wa fedha.
Waziri wa Fedha, Uchumi na Mipango: Mwigulu Lameck Madelu Nchemba, naibu
waziri kwenye wizara hiyo anayeshughulikia uchumi.
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi: Dk. Shukuru Kawambwa anatajwa
kwamba anaweza kurejea kwenye wizara hiyo aliyoiongoza kwa muda mrefu.
Waziri wa Maliasili na Utalii: Mahmoud Mgimwa, naibu waziri wa sasa
katika wizara hiyo ambaye anatetea kiti chake katika Jimbo la Mufindi
Kaskazini.
Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi: William Vangimembe
Lukuvi, ambaye tangu alipoteuliwa kwenye nafasi hiyo ameweza kusaidia kutatua
migogoro mingi ya ardhi mikoani huku mwenyewe akisimamia kupokea malalamiko ya
wananchi hao.
Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto: Ummy Mwalimu, alipata
kuwa naibu waziri katika wizara hiyo pia.
Wizara ya Katiba na Sheria: Angela Kairuki ambaye kwa sasa ni naibu
waziri katika wizara hiyo.
Wizara ya Viwanda, Biashara na Masoko: Mary Michael Nagu, anayewania
Jimbo la Hanang’ mkoani Manyara.
Wizara ya Sayansi, Teknolojia na Elimu ya Juu: January Yussuf Makamba,
Mbunge wa Bumbuli mkoani Tanga na naibu waziri katika wizara hiyo.
Wizara ya Kazi na Ajira: Anne Kilango Malecela, ambaye licha ya kuwa
naibu waziri kwa sasa, lakini suala la ajira amekuwa akilipigia kelele muda
mrefu. Anafaa kuiongoza wizara hiyo.
Wizara ya Habari, Michezo, Utamaduni na
Vijana: Dk. Fenella Mukangara ambaye anawania ubunge katika Jimbo la Kibamba
mkoani Dar es Salaam.
Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa:
Dk. Hussein Ali Hassan Mwinyi, ambaye anawania ubunge katika Jimbo la Kwahani,
Zanzibar. Ndiye anayeiongoza wizara hiyo.
Wizara ya Mambo ya Ndani: Adadi Rajabu,
Mkurugenzi wa zamani wa Makosa ya Jinai ambaye kwa sasa ni Balozi wa Tanzania
nchini Zimbabwe.
Wizara ya Nishati na Madini: George
Simbachawene, waziri wa sasa katika wizara hiyo.
Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii: Dk.
Stephen Kebwe, ambaye kwa sasa ndiye Naibu Waziri.
Wizara ya Ujenzi: Dk. Harrison George
Mwakyembe, ambaye kwa sasa ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Wizara ya Uchukuzi: Job Yustino Ndugai,
ambaye amekuwa naibu spika kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita.
Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika: Dk.
Mathayo David Mathayo ambaye aliwahi kuiongoza wizara hiyo.
Wizara ya Maji na Umwagiliaji: Dk.
Christine Ishengoma, amekuwa mbunge na mkuu wa mkoa kwamuda sasa na ni mhadhili
wa zamani katika Chuo Kikuu cha Kilimocha Sokoine.
Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki: Balozi
Khamis Kagasheki, japokuwa alijiuzulu katika Wizara ya Maliasili na Utalii
kufuatia kashfa ya Operesheni Tokomeza, lakini bado anatajwa kama kiongozi
makini anayeweza kuiongoza wizara hiyo.
Wiziri ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi: Dk.
Titus Kamani, ambaye ndiye alikuwa akiiongoza wizara hiyo. Ingawa ameshindwa na Dk. Raphael Chegeni kwenye kura za maoni Jimbo la Busega, lakini bado anaweza kuteuliwa kupitia kwenye 'kapu'.
Wengine wanaotajwa kuwemo kwenye baraza la mawaziri wakiwa naibu
mawaziri na wizara husika kwenye mabano ni Kassim Majaliwa (Tamisemi), Margaret
Mkanga (Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto), Namelock Sokoine (Maendeleo ya
Mifugo), Mariam Reuben Kasembe (Elimu), Dk. Charles Tizeba (Uchukuzi), Dk.
Suzan Kolimba (Wizara ya Afya), Lucy Mayenga (Ardhi), Daniel Mtuka (Mambo ya
Ndani), Prudensia Kikwembe (Tamisemi) na Godfrey Zambi (Kilimo).
IMECHAPWA MARA YA KWANZA NA GAZETI LA WAJIBIKA AGOSTI 17, 2015



No comments:
Post a Comment