Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Sunday 20 April 2014

SIMBA NA YANGA WALINDA HESHIMA

Keke kuwasha moto Tamasha la Pasaka

WATANI wa jadi wa soka la Tanzania, Simba na Yanga, jana  walitunziana heshima baada ya kufunga msimu wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kwa sare ya bao 1-1 katika mechi kali iliyochezwa Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.
Zikicheza mbele ya mashabiki wachache, Simba walionekana kukamia mechi hiyo kwa kufanya mashambulizi ya nguvu langoni mwa Yanga, hadi filimbi ya mapumziko kulikuwa hakuna bao.
Kati ya kosa kosa za hatari langoni mwa Yanga ndani ya kipindi cha kwanza mbele ya mwamuzi, Jesse Erasmo, ni paleMasoud Nassor Cholo alipopiga krosi ambayo iliokolewa na Kelvin Yondani.
Simba waliendelea kulisakama lango la Yanga ambapo Ramadhani Singano ‘Messi’ naye alipiga shuti ambalo liliokolewa na kipa Dida, ambaye alifanya kazi kubwa langoni.
Shuti jingine la Simba, lilipigwa na Said Ndemla ambalo hata hivyo lilipanguliwa na Dida huku Yanga wakipata nafasi moja tu ya kuweza kufunga, lakini pia wakishindwa kuitumia.
Kipindi cha pili cha mechi hiyo iliyochezwa huku ubingwa wa ligi hiyo ukiwa umepata mwenyewe Azam FC, kwa mara ya kwanza katika historia yake huku Yanga ikimaliza ya pili, Simba ilikuwa ya kwanza kupata bao.
Alikuwa ni Haruna Chanongo ‘Messi’ aliyewainua wapenzi na mashabiki wa Simba dakika ya 75 baada ya kuifungia bao kutokana na krosi ya Uhuru Selemani aliyeingia kuchukua nafasi ya Ndemla.
Baada ya bao hilo, mashabiki wa Simba walishangilia bao hilo kwa staili ya kutaja jina la mshambuliaji wa kimataifa waUganda, Emmanuel Okwi wa Yanga, aliyewahi pia kuichezea Simba.
Kwa upande wa Yanga, bao hilo lilionekana kuwaamsha kwani walianza kufanya mashambulizi ya nguvu na kufanikiwa kusawazisha bao hilo dakika ya 86, likifungwa na Simon Msuva akiwazidi mbinu mabeki.
Msuva alifunga bao hilo akisawazisha makosa ya dakika ya 65, alipopiga shuti ambalo lilitemwa na kipa Ivo Mapunda na kugonga mwamba huku mashabiki wa Yanga wakigawana taulo la kipa Ivo.
Baada ya bao hilo la kusawazisha, shabiki wa  Yanga alipoteza fahamu kwa mshituko hadi kulazimika kupewa msaada wa Msalaba Mwekundu kwa kuokoa uhai wake.
Dakika tatu kabla ya bao hilo, Kocha Msaidizi Selemani Matola na Meneja wa Vifaa, Ally Chenge, walitolewa katika benchi na mwamuzi wa mchezo huo kwa sababu za utovu wa nidhamu.
Bao hilo lilionekana kuamsha nguvu zaidi kwa pande zote kwa kila timu kusaka bao la ushindi, lakini hadi filimbi ya mwisho, matokeo yakawa sare ya bao 1-1.
Matokeo hayo yameifanya Yanga kumaliza msimu ikiwa nafasi ya
pili kwa pointi 56, nyuma ya Azam kwa pointi sita, baada ya jana kuifunga JKT Rvu bao 1-0 katika Uwanja wa Chamazi, nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.
Azam ambayo jana ilishuka dimbani ikiwa tayari imebeba ubingwa wa ligi hiyo tangu walipoifunga Mbeya City, bao lake lilifungwa na mtokea benchi, Bryan Umony, katika dakika ya 79, akiingia kuchukua nafasi ya Kipre Tchetche.
Umony alifunga bao hilo kutokana na kazi nzuri ya mtokea benchi, Kelvin Friday, ambaye kuingia kwake, kuliongeza uhai kwa upande wa Azam iliyoanzishwa Juni 24, 2007.
Kwa ushindi huo, Azam wamemaliza kwa rekodi ya aina yake kwani mbali ya ubingwa, pia wamemaliza wakiwa na pointi 62 huku bila kupoteza mechi, isipokuwa kushinda na sare.
Katika mechi ya jana, kama si kushindwa kuzitumia nafasi walizopata dakika ya 45; 60; 62 na 77, Azam wangeweza kuibuka na ushindi mnono katika mechi hiyo iliyohitimishwa na hafla ya kukabidhiwa ubingwa.
Nafasi pekee kwa JKT Ruvu kupata bao kama wangetulia, ilikuwa dakika ya 75, pale Idd Mbaga alipopiga shuti, lakini kipa wa Azam, Aishi Manula, alifanya kazi ya ziada kupangua na kuwa kona.
Hata hivyo, licha ya kuwepo kwa mashambulizi kadhaa kwa kila upande, hadi mwamuzi Theophil Mohamed kutoka Morogoro anamaliza dakika 90, Azam walikuwa wababe kwa bao 1-0.
Kombe la ubingwa lilikabidhiwa kwa Azam na Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi, ambaye licha ya kuingia uwanjani hapo akiwa na suti, alivishwa fulana yenye ujumbe wa ‘Azam bingwa 2013/2014.’
Yanga: Deogratius Munish ‘Dida,’ Mbuyu Twite, Oscar Joshua, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ Kelvin Yondani, Frank Domayo, Simon Msuva, Hassan Dilunga, Didier Kavumbagu, Mrisho Ngassa na Hamisi Kiiza.
Simba: Ivo Mapunda, Nasor Said, Issa Rashid, Joseph Owino, Donald Musoti, Jonas Mkude, Haruna Chanongo, Said Ndemla,
Amis Tambwe, Amri Kiemba na Ramadhani Singano.
Katika Uwanja wa Azam Complex; Azam ikuwa hivi:
Aishi Manula, Erasto Nyoni, Michael Gadiel, Said Morad, David Mwantika, Kipre Balou, Himid Mao, Salum Aboubakar, Gaudence Mwaikimba, John Bocco na Kipre Tchetche.
JKT Ruvu: Hamis Seif, Kessy Mapande, Edward Charles, Chacha Marwa, Jamal Machelenga, Nashoni Naftari, Gido Chawala, Richard Daniel, Samuel Kamuntu, Thomas Ndimbo na Emmanuel Pius.
CHANZO: TANZANIA DAIMA

No comments:

Post a Comment