Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Sunday 23 August 2015

MAGUFULI ‘TINGATINGA’ AJIVUNIA KUSIMAMIA UJENZI WA 6,276KM ZA BARABARA NCHINI

Wakati wakandarasi walipokuwa wanajenga daraja hili katika eneo la Miangalua kwenye barabara ya Tunduma-Sumbawanga mwaka 2011. Barabara hiyo sasa imekamilika.
Barabara ya Mwanza-Musoma iko katika hali nzuri. 
Ujenzi wa barabara ukiendelea katika baadhi ya miradi nchini.
Ujenzi wa barabara ya Iringa-Dodoma umekamilika kwa asilimia 95, bado maeneo machache tu likiwemo hili la Mlima Nyang'oro ambapo Wachina wameuchonga ili kupunguza kona katika umbali wa kilometa 15. (Picha zote na Daniel Mbega wa www.brotherdanny.com).

 Na Daniel Mbega, brotherdannyblog
Sumbawanga: NAJIWEKA vyema kwenye kiti na kutazama nje kupitia dirishani. Japokuwa giza limetanda majira haya ya saa 4:30 usiku, lakini ninaweza kuhisi jinsi basi hili nililopanda la kampuni ya Majinjah linavyotafuna lami.
Abiria mwenzangu wa jirani ananiambia tutaingia saa sita kasoro usiku Sumbawanga mjini. Nafarijika japo uchovu ni mwingi, maana kuketi kwenye basi kwa saa takriban 15 siyo mchezo ingawa tulipata nafasi mara kadhaa za kupumzika 'kuchimba dawa' na kupata mlo.
“Barabara yote ni lami tupu ndugu yangu, kasoro tu ni haya matuta kutoka Tunduma hadi Sumbawanga, lakini yamesaidia kupunguza mwendokasi,” ananieleza.

Tunduma tumeondoka kama saa tatu hivi kuzikabili kilometa 222 hadi Sumbawanga, lakini safari hii ya kutoka Dar es Salaam inayokadiriwa kuwa na umbali wa kilometa 1,000 imekuwa siyo ndefu licha ya uchovu wa kiuno na mgongo kutokana na kuketi tangu saa 12 alfajiri. Faraja pekee ni kwamba ninatumia siku moja tu kufika Sumbawanga, tofauti na miaka mitano iliyopita ambapo nililazimika kutumia siku mbili huku nikiingia gharama za ziada za kulala Lodge pale Mbeya kutokana na kutokuwepo na usafiri wa uhakika kutokana na ubovu wa barabara.
Wakati huo, ukilala Mbeya unalazimika tena kuamka mapema kuwahi basi ambalo licha ya kuondoka saa 12 alfajiri, bado litafika Sumbawanga saa 8 mchana.
Jirani yangu ananiambia kwamba sasa unaweza kwenda na kurudi Sumbawanga mara mbili ukitokea Mbeya kwani mabasi ni mengi na njia ‘inateleza’.
“Wametukomboa sana, magari hayajazi kama zamani, unasafiri kwa raha na kwa wakati – muda wowote unaotaka,” ananieleza.
Ndiyo. Nakumbuka safari moja wakati nikitokea Sumbawanga jinsi basi lilivyokuwa limejaza abiria mpaka sehemu ya kupita ikakosekana. Walioketi walikuwa wachache kuliko waliosimama, sasa piga hesabu lilikuwa na abiria wangapi! Hata kondatka mwenyewe alilazimika kupita kwa kuinama juu ya siti ili kwenda nyuma kuwapanga abiria waliosimama na kuchukua nauli. Ilikuwa ni hatari.
Lakini leo barabara hii imetandikwa lami na imekuwa sehemu ya barabara zenye urefu wa jumla ya kilometa 6,276 ambazo zimetengenezwa na utawala huu wa Awamu ya Nne, huku sehemu kubwa yabarabara hizo ikiwa imesimamiwa na Dk. John Pombe Joseph Magufuli kama Waziri wa Miundombinu.
Nimezunguka karibu nchi nzima nikifanya habari za uchunguzi kwa miaka kumi iliyopita. Mazingira ya wakati ule na ya sasa ni tofauti kabisa, maeneo ambayo yalikuwa hayafikiki, hivi sasa hali ni nzuri. 
Tangu Januari hadi Juni 2015 pekee nimezunguka karibu kilometa 20,000 hapa nchini. Nimezunguka nikitokea Iringa kwenda Arusha kupitia Dodoma-Singida hadi Manyara; nimezunguka kutoka Dar es Salaam-Kiteto-Kondoa hadi Babati; nimepita Babati-Kondoa-Mayamaya hadi Dodoma; nimepita Mwanza-Shinyanga-Tabora-Mpanda hadi Sumbawanga mpaka Mbeya; nimetoka Dar es Salaam-Njombe-Songea hadi Mbambabay; nimetoka Mwanza-Musoma hadi Sirari; nimezunguka Mwanza-Sengerema-Geita hadi Bukoba; nimetoka Bukoba kupita Kahama hadi Dar es Salaam; nimetoka Shinyanga-Maswa-Bariadi hadi Lamadi; na maeneo mengine mengi kwa miezi sita.
Hakika nilichokiona kinastahili kupongezwa kwamba kimefanyika. Ingawa barabara kadhaa zimesimama kutokana na kukosekana kwa fedha kufuatia msukosuko wa wafadhili kushindwa kutoa fungu, lakini nyingi kati ya hizo zimekamilika na kuiunganisha vyema Tanzania.
Nilipita wakati fulani ilipoanza kutengenezwa barabara hii, nadhani ilikuwa mwaka 2011 nikiwa katika harakati zangu za kuandika habari za maendeleo vijijini. Barabara hii ilimegwa katika vipande vitatu ili kuharakisha ujenzi wake na kuzingatia ubora.
Kipande cha kwanza kilikuwa kutoka Tunduma hadi Ikana chenye urefu wa kilometa 63.2 ambacho kilijengwa na kampuni ya Consolidated Contractors Group kwa gharama ya Dola 82.521 milioni; Kipande cha pili chenye urefu wa kilometa 64.2 kilikuwa kutoka Ikana hadi Laela na kilijengwa na kampuni ya China Newera (64.2km Ikana-Laela) kwa Dola 46.812 milioni; na kipande cha mwisho kilikuwa kutoka Laela hadi Sumbawanga chenye urefu wa kilometa 95.31 ambacho kilijengwa na kampuni ya Aarsleff-Interbeton J.V kwa gharama ya Dola 130.038 milioni. Kwa hiyo kilometa zote 222.71 ziligharimu jumla ya Dola 259.371 milioni ambazo ni fedha za wahisani na fedha za ndani.
Ni fedha nyingi sana lakini haziwezikuzidi thamani halisiya barabara hii ambayo licha ya kuwakomboa wananchi wa pembezoni hasa katika mikoa ya Mbeya, Rukwa na Katavi, lakini pia itasaidia kuiunganisha Tanzania na nchi jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kwa sababu ujenzi wa barabara yenye urefu wa kilometa 112 kutoka Sumbawanga-Matai hadi bandari ya Kasanga katika Ziwa Tanganyika unaendelea chini ya kampuni ya China Railway 15th Bureau Group Corporation - CR15G kwa gharama ya Dola 80.912 milioni.
Dk. Magufuli, ambaye sasa ni mgombea urais kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), anazifahamu karibu barabara zote nchini na hatua zilikofikia. Alipoingia kwa mara ya kwanza bungeni mwaka 1995 baada ya kushinda katika jimbo la Chato akiwa na miaka 36 tu,  Rais Benjamin Mkapa akamteua kuwa Naibu Waziri katika Wizara ya Miundombinu. Kazi ya Ubunge na unaibu waziri ilimpeleka salama hadi mwaka 2000.
Uchaguzi wa mwaka 2000 ulipoitishwa, Dk. Magufuli aligombea na kushinda kwa mara ya pili. Rais Mkapa akamteua kuwa Waziri wa Wizara ya Miundombinu, wadhifa aliodumua nao hadi kipindi cha uongozi wa Mkapa kilipomalizika.
Mwaka 2005 alishinda ubunge kwa mara ya tatu, lakini safari hii aliingia katika orodha ya wabunge waliopita bila kupingwa. Rais Jakaya Kikwete akamteua kuongoza Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi hadi mwaka 2008 alipohamishiwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, ambayo aliiongoza hadi mwaka 2010.
Mwaka 2010 akagombea tena ubunge, lakini safarihii akapambana na mgombea wa Chadema, Rukumbuza Vedastus Albogast ambaye alitoa upinzani mkubwa ingawa hatimaye Magufuli alishinda kwa asilimia 66.39 dhidi ya asilimia 26.55 za mpinzani wake. Rais Kikwete akamrudisha katika Wizara ya Ujenzi ambako yuko hadi hivi sasa.
Tangu kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2005, wengi walikuwa wakimtaja Magufuli kwamba anafaa kuwania urais, lakini yeye alikaririwa akisema wakati huo kwamba hana mpango huo.
Hata makada wenzake walipoanza kuonyesha nia kwa ajili ya uchaguzi wa mwaka huu, yeye hakuwa na papara na iliwashangaza wengi Mei 29 alipoamua kujitosa kimya kimya, akachukua fomu na kuondoka, bila mbwembwe wala madoido kama walivyofanya wengine.
Wanaomfahamu wanasema nguvu yake kubwa iko kwenye elimu yake, lakini kukaa muda mrefu kwenye wizara zake na mambo makubwa aliyoyafanya katika wizara alizopata kuziongoza, pamoja na uwezo wake wa kutoa maamuzi magumu kila mara vinampa sifa ya kuwa rais anayefaa katika kipindi hiki ambacho rushwa, ufisadi na ukosefu wa maadili vimetamalaki.
Udhaifu wake pekee unaotajwa na walio karibu yake ni kufanya maamuzi ya haraka, jambo ambalo linaweza kurekebishwa.

UJENZI WA BARABARA
Katika kipindi cha uongozi wa Serikali ya awamu ya nne, barabara zenye urefu wa jumla ya 6,276.82km zimejengwa kwa gharama ya Dola 102,654.98 milioni, nyingi kati ya hizo zikiwa za lami na hivyo kuutengeneza mtandao imara wa miundombinu ya barabara.
Kujengwa kwa barabara hizo kumerahisisha hata usafiri ambapo leo hii magari ya abiria na mizigo kutoka Dar es Salaam kwenda Musoma, Mwanza, Kagera na Kigoma hayahitaji kuzunguka Nairobi bali yanakwenda moja kwa moja.
Hivi sasa usafiri wa kutoka Dar es Salaam kwenda Sumbawanga ni wa siku moja badala ya siku mbili, kama ilivyo kwa usafiri wa Dar es Salaam kwenda Mbinga, jambo ambalo miaka 10 iliyopita lilikuwa ndoto.
Asilimia 90 ya miradi hiyo imesimamiwa na Dk. Magufuli akiwa Waziri wa Miundombinu katika kipindi cha mwaka 2010 hadi 2015na bado miradi mingine inaendelea kujengwa japo imesimama kidogo kutokana na ufinyu wa bajeti.
Kampuni za Kichina zimepata mikataba mingi ya ujenzi. Kwa mujibu wa taarifa kutoka Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), katika kipindi cha miaka 10 iliyopita, kampuni 14 kutoka China zimeingia jumla ya mikataba 58 ya ujenzi wa kilometa 3,140.85 yenye thamani ya Dola 1.75 bilioni.
Kampuni ya China Henan International Cooperation Group Co., Ltd. (CHICO) ambayo ilipata mkataba wenye thamani ya Dola 206 milioni kutoka Wakala wa Barabara Zambia kujenga barabara ya Mansa-Luwingu yenye urefu wa kilometa 175, peke yake imeingia mikataba 13 nchini Tanzania ya barabara zenye urefu wa kilometa 705.2 zikiwa na thamani ya Dola 490.26 milioni.
Hizi ni pamoja na barabara za Singida-Iguguno (76km) yenye thamani ya Dola 20.55 milioni; Sekenke-Shelui (33km) yenye thamani ya Dola 12.51 milioni; Mwandiga-Manyovu (60km) wenye thamani ya Dola 32.54 milioni; Kigoma-Kidahwe (35.7km) kwa Dola 19.56 milioni; Bonga-Babati (19.20km) kwa Dola 11.95 milioni; Tabora-Urambo (42km) kwa Dola 31.17 milioni; Kyaka-Bugene (59.1km) kwa Dola 51.6 milioni; Dareda-Minjingu (84.6km) kwa Dola 51.6 milioni); Kidahwe-Uvinza-Ilunde (76.6km) kwa Dola 47.5 milioni; Isaka-Ushirombo (132km) kwa Dola 88.223 milioni; Kilwa Road Phase III (1.5km) kwa Dola 3.4 milioni; Nyanguse-Musoma (85.5km) kwa Dola 3.3 milioni; na Kagoma-Lusahunga (154km ) kwa ubia na kampuni ya CRSG kwa gharama ya Dola 116.2 milioni.
China Sichuan International Cooperation Co., Ltd (SIETCO) inajenga barabara zenye urefu wa 283.9km zenye thamani ya Dola 123.03 milioni ambazo ni Isuna-Singida (63km) kwa Dola 18.5 milioni; Tarakea-Rongai-Kamwanga (32km) kwa Dola 8.8 milioni; Iringa-Migori (95.1km) kwa Dola 51.123 milioni; na Migori-Fufu Escarpment (93.8km) kwa Dola 44.7 milioni, wakati kampuni ya CICO inajenga barabara ya Nangurukuru-Mbwemkuru yenye 95km kwa thamani ya Dola 23.82 milioni.
Kampuni ya China Geo-Engineering Corporation International Ltd (CGC INT'L) inajenga barabara zenye urefu wa 525.9km zikiwa na thamani ya Dola 151.2 milioni. Barabara hizo ni Shelui-Nzega (112km) kwa Dola 12.6 milioni; Kyamorwa-Buzirayombo (120km) kwa Dola 29.822 milioni; Manyoni-Isuna (54km) kwa Dola 18.4 milioni; Arusha-Namanga (104.2km) kwa Dola 49.64 milioni; Chalinze-Tanga Phase I (125km ) kwa Dola 25.9 milioni na ndiyo kampuni iliyojenga Daraja la Mkapa (Daraja la Umoja 10.7km) linalounganisha Tanzania na Msumbiji kwa gharama ya Dola 14.9 milioni.
Katika orodha hiyo, ipo kampuni inayomilikiwa na serikali ya China, Hydropower Engineering and Construction Company (SINOHYDRO) ambayo ilipata mikataba 12 nchini Tanzania ya ujenzi wa barabara zenye urefu wa jumla ya 779.95km zenye thamani ya Dola 434.36 milioni. Barabara hizo ni Sengerema-Usagara (40km) kwa gharama ya Dola 21.724 milioni; Buzirayombo-Geita (100km) kwa Dola 25 milioni; Geita-Sengerema (50km) kwa Dola 24.034 milioni; Dodoma-Mayamaya (43.65km) kwa Dola 25 milioni; Manyoni-Itigi-Chaya (89.3km) kwa Dola 66.56 milioni; Puge-Tabora (56.1km) kwa Dola 35.085 milioni; Handeni-Mkata (54km) kwa Dola 34.81 milioni; Korogwe-Handeni (65km) kwa Dola 38.4 milioni; Katesh-Dareda (73.8km) kwa Dola 38.94 milioni; Singida-Katesh (65.1km) kwa Dola 31.34 milioni; Tanga-Horohoro (65km) kwa Dola 42.43 milioni; na Peramiho Junction-Mbinga (78km) kwa Dola 48.444 milioni.
CHIKO ilijenga barabara ya Sam Nujoma jijini Dar es Salaam yenye urefu wa 4km kwa thamani ya Dola 7.9 milioni, China Civil Engineering Construction Corporation (CCECC) ilipata mikataba minne ya kujenga barabara zenye urefu wa 145.6km kwa thamani ya Dola 95 milioni. Barabara hizo ni Magole-Turiani (48.6km) kwa Dola 25.43 milioni; Tabora-Urambo (52km) kwa Dola 36.3 milioni; Dumila-Rudewa (45km) kwa Dola 25.5 milioni na Jangwani Depot kwa ajili ya mradi wa mabasi yaendayo kasi Dar es Salaam (BRT) kwa Dola 7.81 milioni.
China Communications Construction Company (CCCC) ina mikataba mitano ya ujenzi wa barabara za urefu wa 273.5km zikiwa na thamani ya Dola 178.333 milioni ambayo inahusisha barabara za Mbeya-Lwanjilo (36km) kwa Dola 33.622 milioni; Lwanjilo-Chunya (36km) kwa Dola 24.5 milioni; Mwigumbi-Maswa-Bariadi-Lamadi (71.8km) kwa Dola 40.91 milioni; Nzega-Puge (58.8km ) kwa Dola 40.283 milioni na Fufu Escarpment-Dodoma (70.9km) kwa Dola 39.05 milioni.
Beijing Construction Engineering Group Co., Ltd. (BCEG) ilishinda zabuni katika mradi wa BRT kuanzia Stendi ya Mabasi Ubungo likiwemo Daraja la Stendi Kuu; Kariakoo na Kivukoni kwa gharama ya Dola 30.446 milioni, wakati China Henan ndiyo iliyojenga Daraja la Ruvu kwa Dola 2.69 milioni.
Kampuni nyingine za China na miradi yao kwenye mabano ni, Jiangxi Geo-Eng (75km Sumbawanga-Kanazi) kwa Dola 47.9 milioni, China Hunan Construction Engineering Group Corporation - CHCEG (76.6km Kanazi-Kizi-Kibaoni) kwa Dola 50.3 milioni, China Railway 15th Bureau Group Corporation - CR15G (112km Sumbawanga-Matai-Kasanga) kwa Dola 80.912 milioni, na China Newera (64.2km Ikana-Laela) kwa Dola 46.812 milioni.
Kampuni za Kijapani ambazo katika miaka ya 1980 na mwishoni mwa 1990 ndizo zilikuwa zikishindana na kampuni kutoka Ulaya, katika kipindi hiki zilifanikiwa kupata mikataba sita tu ya kujenga barabara za urefu wa 204.4km yenye thamani ya Dola 106.09 milioni. Kampuni ya Tokura Corporation ilipata miradi miwili yenye urefu wa jumla ya 55.1km kwa Dola 33.980 milioni. Miradi hiyo ni Masasi – Mangaka Phase II (17.6km) kwa Dola 11.4 milioni; barabara ya Masasi – Mangaka Phase I (15km) kwa Dola 6.8 milioni; na Masasi – Mangaka Phase III (22.5km) kwa Dola 15.78 milioni.
Kampuni ya Konoike ilipata miradi miwili ambayo ni ujenzi wa barabara ya Dodoma – Manyoni (127km) kwa Dola 103.4 milioni na upanuzi wa Barabara ya Bagamoyo kwa urefu wa 17.2km kwa Dola 21.6 milioni, na Kajima ilipata mradi wa ujenzi wa Barabara ya Kilwa Phase II (5.1km) kwa Dola 15.78 milioni ambayo inaendelea kukarabatiwa baada ya Dk. Magufuli kuikataa kutokana na kutokidhi viwango.
Kampuni kutoka Ulaya na kwingineko Afrika zilikuwa 13 ambazo zilijenga barabara zenye urefu wa 1,598.91km na thamani ya Dola 579.25 milioni. Kampuni ya Grinaker-LTA ilijenga barabara ya Tinde – Mpaka wa Shinyanga/Mwanza (96km) kwa Dola 53.23 milioni na barabara ya Nzega-Tinde-Isaka (73km) kwa Dola 41.55 milioni.
Kampuni ya NCC International Denmark A/S ilifanya ukarabati katikaBarabara ya Morogoro – Dodoma (256km) kwa Euro 42.5 milioni.
Kampuni ya General Nile ilipata miradi miwili ambayo ni Marangu – Rombo Mkuu (32km) kwa Dola 25.076 milioni; na Rombo Mkuu – Tarakea (32km) kwa Dola 15.783 milioni.
Kampuni ya MSS JV ilijenga Barabara ya Mandela yenye urefu wa 15.6km kwa Dola 41.222 milioni.
Kampuni ya CF Tech ilinajenga Barabara ya Tabora – Nyahua – Chaya yenye urefu wa 85km kwa gharama ya Dola 93.401 milioni.
Kampuni ya Strabag, mbali ya kupewa tenda katika Mradi wa Magari Yaendayo Kasi jijini Dar es Salaam, pia ilipata mkataba wa kujenga Barabara ya Ushirombo – Lusahunga yenye urefu wa 110km kwa gharama ya Dola 114.5 milioni.
Kampuni ya Progressive Higleig JV ilipata mikataba mitatu ambayo ni barabara ya Namtumbo – Kilimasela Lot A (60.7km) kwa gharama ya Dola53.23 milioni; Barabara ya Matemanga – Tunduru Lot C (58.7km) kwa gharama ya Dola 63.409 milioni; na Barabara ya Kilimasela – Matemanga Lot B (68.2km) kwa gharama ya Dola 64.017 milioni.
Kampuni ya Aarsleff-Interbeton J.V ilipata mikataba ya kutengeneza Barabara ya Tanzam Highway kutoka Iyovi-Iringa-Mafinga (149.6km) kwa gharama ya Dola 127.71 milioni; na barabara ya Laela – Sumbawanga (95.31km) kwa gharama ya Dola 130.038 milioni.
Kampuni ya SBI-International Holdings ilipata mkataba wa kujenga barabara ya Chalinze – Tanga Phase II (120km) kwa gharama ya Dola 67.2 milioni.
Kampuni ya LAC & JFM ilipata mkataba wa kujenga barabara ya Tanga Magharibi PMMR (224.8km) kwa gharama ya Dola 7.805 milioni.
Kampuni ya Y.N & Lucky ilipata mkataba wa PMMR: Tanga Mashariki (116.8km) kwa gharama ya Dola 3.59 milioni.
Kampuni ya Spencon ilipewa zabuni ya kusambaza umeme wa barabarani kwa gharama ya Dola 5.599 milioni na kampuni ya Consolidated Contractors Group ilijenga barabara ya Tunduma – Ikana (63.2km) kwa gharama ya Dola 82.521 milioni.
Kampuni za wazalendo ambazo zimepata zabuni mbalimbali za ujenzi wa barabara jumla yake ziko 10 ambapo zimepata miradi 14 ya barabara zenye urefu wa 1,222.51km kwa gharama ya Dola 462.771 milioni.
Kampuni ya Estim imejenga barabara kutoka Kituo cha Mabasi Ubungo – Kigogo – Mzunguko wa Barabara ya Kigogo yenye urefu wa 6.4km kwa gharama ya Dola 11.44 milioni na Barabara ya Bagamoyo – Msata (64km) kwa gharama ya Dola 89.608 milioni.
Kampuni ya Hari Singh imejenga barabara yenye urefu wa 2.7km kutoka Mzunguko wa Barabara ya Kawawa - Bonde la Msimbazi - Makutano ya Mtaa wa Twiga kwa ghara ya Dola 7.639 milioni.
Kampuni ya M.A Kharafi & Sons imejenga barabara ya Ndundu – Somanga (60km) kwa Dola 58.813 milioni na barabara ya Mbwemkuru – Mingoyo Lindi (95km) kwa Dola 51.49 milioni.
Kampuni ya Nyanza Road imejenga barabara ya Jet Corner – Vituka – Davis Corner (10.3km) kwa Dola 12.474 milioni na ukarabati wa barabara za Mwanza Magharibi (208.4km) kwa Dola 6.329 milioni.
Kampuni ya Sogea-Satom imejenga barabara ya Arusha – Minjingu (98km) kwa Dola 75.511 milioni na Songea – Namtumbo (67km) kwa Dola 62.25 milioni.
Kampuni ya Hanil Engineering ilijenga daraja la Maragarasi na barabara zinazoingia zenye urefu wa 48km kwa gharama ya Dola 56.366 milioni, wakati ambapo KMM (2006) Enterpreneurs Ltd ilikarabati barabara za vijijini Rukwa Kusini (189.98km) kwa gharama ya Dola 5.763 milioni.
Kampuni ya Inhouse imejenga barabara ya Mkuranga – Kibiti (60km) kwa Dola 17.52 milioni; kampuni ya Summry’s Enterprises imejenga barabara za vijijini Rukwa Kaskazini (173.8km) kwa Dola 3.189 milioni; na kampuni ya Katemayanga imejenga barabara za Mwanza Mashariki (138.93km) kwa Dola 4.379 milioni.
Wengi wanaamini kwamba, Tanzania ya leo inafikika kirahisi kutokana na mtandao wa barabara ambao serikali ya CCM imeutekeleza kwa kiwango kikubwa, hivyo wanaamini pia kwamba ikipewa nafasi nyingine inaweza kufanya mambo makubwa zaidi hata katika sekta nyingine.

(Imeandaliwa na www.brotherdanny.com. Simu: 0656-331974)

No comments:

Post a Comment