Askofu Paul Akyoo wa KKKT Dayosisi ya Meru
Meru: Zaidi ya kaya 4000 zimepatiwa msaada wa chakula katika vijiji tofauti tofauti ndani ya Wilaya za Arumeru na Longido na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Dayosisi ya Meru ikiwa ni msaada wa wahisani kutoka Marekani ili kuisaidia serikali kupunguza makali ya njaa kwa baadhi ya maeneo yaliyokumbwa na baa la njaa.
Askofu wa kanisa hilo Paulo Akyoo amesema baada ya Dayosisi hiyo kuona baadhi ya maeneo kuna upungufu mkubwa wa chakula aliomba msaada kutoka kwa wahisani marafiki zake waliopo Marekani wanaoitwa Wakristo wa (The Greater Milwakee) walitoa pesa kidogo ambazo askofu Akyoo aliona ni vyema wanunue magunia ya mahindi 1000 sawa na tani 100.
Akyoo amesema kuwa msaada huo wa chakula hicho sio cha Wakristo peke yao bali ni kwa ajili ya wananchi wote bila kujali itikadi za dini wala vyama kwani njaa haina mwenyewe na wamelenga maeneo yaliyokumbwa na upungufu wa chakula kwa kiasi kikubwa ambapo hadi hivi sasa jumla ya tani 40 zimeshagawiwa kwa kaya 2,200.
Aidha mratibu wa msaada huo ambaye ni Diwani wa Halmashauri ya Meru, Loti Nnko amesema kutokana na hali ya hewa kutokuwa nzuri hivyo imepelekea baadhi ya maeneo kuwa na upungufu mkubwa wa chakula hivyo mpaka sasa wamegawa katika Kijiji cha Ngarenanyuki, Majengo, Kia, Mbuguni, Engareyani, Longido, Katanumbe, Malaba,
Nnko amebainisha kuwa ingawa msaada huo sio mkubwa lakini unawasaidia wananchi hivyo amewaomba wahisani wenye uwezo kuweza kulisaidia Kanisa ili liweze kuwahudumia wananchi wengi zaidi.
Hata hivyo ameongeza kuwa katika awamu hii ya kwanza ya msaada huo kaya zaidi ya 4000 zitapata chakula huku kila mwananchi anapata kilo 20 na kwa sasa wanaelekea Tarafa ya Mbuguni na Maroroni.
Nao wananchi wa ngarenanyuki katika halmashauri ya meru wamelishukuru Kanisa la KKKT Dayosisi ya Meru kwa kuona kuwa nao ni sehemu ya tatizo hivyo wameomba wadau wengine kuisaidia serikali kwenye baadhi ya matatizo.
No comments:
Post a Comment