Na Mwandishi Wetu, BrotherDanny Blog
Arusha: JUMLA ya watoto 687,543 chini ya miaka 15 mkoani Arusha watapewa chanjo ya ugonjwa wa Surua Rubella, matone ya Vitamin A na dawa za minyoo.
Hayo yameelezwa na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo, kwenye hotuba yake iliyosomwa na Mkuu wa Wilaya ya Longido, James ole Millia, kwenye uzinduzi wa kampeni za mkoa zilizofanyika kijiji cha Mbuguni Halmashauri ya Wilaya ya Meru.
Mulongo, amesema mwaka 2011 katika kampeni kama hiyo iliyolenga watoto chini ya miaka 5 mkoa uliwapatia chanjo ya surua watoto 287,303 ambayo ni sawa na asilimia 102, chanjo bya polio watoto 332,682 sawa na asilimia 106.
Amesema bado kuna changamoto za kufikia malengo ya Mkukuta, ambazo ni npamoja na kutokuwa na wataalam wa kutosha katika kutoa huduma za afya,hudumja kuwa mbali na walengwa katika baadhi ya maeneo katika halmashauri za Ngorongoro, Karatu, Monduli na Longido.
Mulongo, amesema wizara ya afya na usitawi wa jamii imeelekeza mikoa na halmashauri zote kuhakikisha zahanati mpya zilizojengwa na kukamilika zisajiliwe na kuanza kazi ya kutoa huduma mara moja.
Amesema katika kampeni hiyo ambayo imeanza kutekelezwa Oktoba 18 itakamilika Oktoba 24 na hakuna mtoto atakae achwa bila kpatiwa chanjo hiyo.
Aidha halmashauri zote ziimarishe ufuatiliaji wa na usimamizi ili kuboresha huduma za afya nchini ikiwemo ujazaji sahihi wa takwimu, pia halmashauri zitenge fedha za kutosha kununulia dawa,vitendea kazi, vifaa tiba sambamba na kusimamia matumizi kulingana na maelekezo ya serikali.
Pia amewapongeza wataalam wa afya kwa kufanya kazi kwa kujituma licha uchache wao na mazingira magumu.
Awali mganga mkuu wa mkoa wa Arusha, Dakta Frida Mokiti ,amesema kuwa kiwango cha chanjo katika mkoa huo kimepanda kutoka asilimia 98 mwaka 2005 hadi kufikia asilimia 119 mwaka 2013,pia vituo vya kutolea chanjo navyo vimeongezeka kutoka 171 mwaka 2007 hadi 236 mwaka 2013.
Aidha ongezeko hilo limewezesha kutokomezwa kwa ulemavu unaosababishwa na virusi vya polio na ugonjwa wa pepo pounda na hivyo kufungwa kwa wodi za surua ,pamoja na kudhibitiwa maradhi ya donda koo ,kifaduro na surua.
Amewahakikishia wananchi kuwa chanjo hizo ni salama na zimethibitishwa na shirika la afya ulimwenguni, WHO , na wizara ya afya na usitawi wa jamii.
Hadi sasa mkoa huo kuanzia Januari hadi Julai mwaka huu jumla ya watoto wanane kati ya ishirini na saba waliokuwa wamehisiwa kuwa na ugonjwa wa surua na Rubella,wamethibitika baada ya uchunguzi wa kimaabara.
Amesema ugonjwa huo wa Rubella, ni hatari, pindi unapoimpata mama mjamzito husababisha madhara makubwa nay a kudumu kwa mtoto ukiwemo ugonjwa wa moyo, udumavu, mtoto wa jicho, mtindio wa ubongo, na kifo.
Dakta Mokiti, amekiri kuwa surua ya Rubella, ambayo asili yake ni surua ya Kijerumani, imekuwepo mkoani Arusha kwa kipindi kirefu na bado ipo.
Amesema tafiti zimethibitisha kuwa surua ya Rubella, imekuwepo kwa kipindi kirefu nchini na inashambulia pia ubongo wa mtoto.
No comments:
Post a Comment