Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Friday 3 October 2014

WANAJESHI, POLISI WATWANGANA RISASI HADHARANI!


Msemaji wa JWTZ, Luteni Kanali Erick Komba

Askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na askari wa Jeshi la Polisi, wameshambuliana kwa silaha mbele ya raia na kusababisha baadhi ya maofisa waandamizi kujeruhiwa kwa risasi, baadhi yao vibaya.

Tukio hilo lilitokea juzi saa 11:00 jioni katika Kituo Kikuu cha Mabasi mjini Tarime.

Waliojeruhiwa katika tukio hilo ni askari JWTZ, Aloyce Filbert (24),  aliyepigwa risasi mguuni na Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Kipolisi wa Tarime/Rorya, SSP Salum, aliyejeruhiwa kichwani pamoja askari kadhaa.



Askari wengine saba walijeruhiwa kwa kupigwa risasi mguuni na Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Kipolisi Tarime/Rorya (RCO), SSP Salum, alijeruhiwa kichwani huku askari kadhaa wa majeshi hayo wakijeruhiwa katika vurugu hizo ambazo zilisababisha maduka kufungwa na huduma kukwama.

Kutokana na tukio hilo, wananchi walilazimika kufunga maduka yao kwa muda na huduma muhimu kwa jamii kusitishwa kwa hofu ya kujeruhiwa au kuuawa kwa silaha za moto zilisohusika katika mapambano hayo.

Kamanda  wa Polisi Mkoa wa Tarime/Rorya, Lazaro Mambosasa, alithibitisha kutokea kwa vurugu hizo kati ya Polisi na JWTZ wa Kikosi cha Nyandoto na kueleza kuwa Jeshi la Polisi linawashikilia askari wawili wa JWTZ kwa mahojiano.

“Tunakwenda kwenye kikao cha Kamati ya Ulinzi na Usalama kuzungumzia masuala haya, taarifa kamili mtaipata baadaye ,” alisema kamanda huyo.

Baadhi ya mashuhuda wa tukio hilo ambao hawakutaka majina yao kutajwa gazetini, walisema chanzo ni askari wa JWTZ aliyejulikana kwa jina moja la Mkama ambaye alikuwa anaendesha pikipiki bila kuvaa kofia ngumu akiwa na wenzake,  Alyoce Filbert na Deus Dominick, kukamatwa na askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani.

Walisema baada ya kukamatwa, askari wa JWTZ aliomba msamaha huku akionyesha kitambulisho cha kazi, lakini trafiki hao walikamata pikipiki yake huku Mkama naye akijaribu kuwazuia ndipo walipowaita polisi wengine kwa msaada zaidi.

Walisema Polisi walifika na magari mawili wakiongozwa RCO huku askari wa JWTZ nao wakiitana na kufikia zaidi ya 10, akiwamo mkubwa wao  ambao walijaribu kusuluhisha kusitokee vurugu bila mafanikio.

“Wakati RCO na Mkuu wa askari wa JWTZ (ambaye hajafahamika kwa jina), wakizungumza mmoja wa askari wa JWTZ alimpiga kwa kitu RCO shavuni na kichwani na ndipo askari Polisi walipojibu mashambulizi kwa kurusha mabomu na risasi iliyompata Aloyce mguuni,” alisema.

“Hali ilikuwa ngumu risasi zilirindima ovyo kila mmoja aliogopa na kujificha alikoweza ikiwamo kufunga biashara,” alisema mwananchi huyo.

Aidha, walisema hali hiyo inashangaza kwa kuwa kazi za vyombo hivyo zinafanana na kwamba vyote ni vyombo vya usalama vinavyotegemewa na raia katika ulinzi.

Mwenyekiti wa Chama Cha MAapinduzi (CCM) Wilaya ya Rorya,   Samwel Kiboye, alilaani tukio hilo na kusema ni la kushangaza kwani kila chombo kina majukumu yake ya kisheria kimoja kulinda mipaka ya Tanzania na kingine usalama wa raia na mali zake.

Alisema ni vyema wangezungumza na kumaliza badala ya kutumia jazba kwani wanaiharibu taswira ya JWTZ na Jeshi la Polisi kwa kushambuliana na kujeruhiana hadharani kwa kutumia silaha za moto.

Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya Tarime, Dk. Benard  Makonyu, alithibitisha kupokea majeruhi Filbert na Dominic wakiwa na majeraha waliyoyapata katika vurugu hizo.

Alisema Polisi waliodaiwa kujeruhiwa na kupatiwa matibabu na kuondoka ni Ally Guma (26), Makoye Kitula (25), Sylivester Michael (31), Abdallah Khalid, Over Msabita na Deo Tryphone.

NIPASHE ilimtafuta Msemaji wa JWTZ, Luteni Kanali Erick Komba, kueleza kuhusiana na tukio hilo ambapo alisema yuko mkoani Shinyanga na kumwelekeza mwandishi kuwasiliana na msaidizi wake, Meja Masanja, ambaye naye alidai yupo kwenye foleni kuelekea Lugalo, jijini Dar es Saalam.

Meja Masanja alisema asingeweza kuzungumza kwa kuwa alikuwa anaendesha gari na kutaka atafutwe baadaye.

Hata hivyo, hadi tunakwenda mitamboni Meja Masanja hakupatikana.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment