Pages

Pages

Pages

Friday 15 August 2014

MJAMZITO ATEMBEA KILOMETA 100 KUJINUSURU KIPIGO CHA MUMEWE


Binti mwenye umri wa miaka 16 na mimba ya miezi mitatu, Esther Jilaa, ametembea kwa miguu umbali wa kilomita 100 kwa muda wa siku mbili kutoka katika Kijiji cha Ighombwe hadi mjini Singida kuomba msaada kwa wasamaria wema baada ya mume aliyekuwa akiishi naye kumyanyasa kwa kipigo kila siku.

Akielezea mkasa huo kwa shida, Jilaa mwenye asili ya Wilaya ya Maswa, mkoani Shinyanga, alisema alifunga ndoa na mumewe miezi tisa iliyopita na kwamba, mpaka anavyoondoka kwenye ndoa yake ana ujauzito wa miezi mitatu.

Kwa mujibu wa Esther, sababu zilizomfanya achukue maamuzi ya kutoroka nyumbani kwake ni baada ya kupata kipigo cha mbwa mwizi kutoka kwa mwanandoa mwenzake huyo kutokana na kuwaachia ndama kunyonya maziwa yote kabla ya wao kukamua. Alitaja sababu nyingine ya kukimbia kwenye ndoa yake kuwa ni umri wake mdogo kulinganishwa na mumewe.

Baadhi ya wasamaria wema waliomuokota walisema Esther alikuwa ametoroka na kwamba, alikuwa akienda nyumbani kwao Wilaya ya Maswa, mkoani Shinyanga kwa miguu kutokana na kutokuwa na fedha.

Hata hivyo, wasamaria hao, Maria Daudi na Elizabethi Lazaro, waliweka wazi kwamba, licha ya Esther kutokuwa na fedha za nauli wala chakula, hakuwa tayari kurudi nyumbani kwake ili aendelee kuishi na mumewe.

Mratibu wa Kituo cha Usaidizi wa Kisheria cha Singida, Paralegal Aid Centre, Fatuma Amiri, alisema baada ya ofisi yake kupata taarifa za kufanyiwa ukatili huo, waliamua kumtafuta na kumfikisha katika kituo kikuu cha polisi mjini Singida kumtafutia msaada kwa sababu yeye binafsi hakuwa tayari kurudishwa kwa mumewe.

Alisema baada ya kumfikisha polisi kikosi cha usalama barabarani, walimpa kibali cha kupata msaada wa usafiri wa kufika kwao mkoani Shinyanga.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment