Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Thursday, 12 June 2014

LEO NI BAJETI KUU YA TANZANIA 2014/2015

Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum


Dodoma. Macho na masikio ya wananchi leo yatahamia bungeni mjini Dodoma wakati Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum atakapokuwa akisoma Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha wa 2014/15.
Mwelekeo wa Bajeti hiyo umekuwa na usiri mkubwa kutokana na Serikali kutokuwa wazi kuieleza Kamati ya Bunge ya Bajeti, vyanzo vyake vipya vya mapato licha ya kukutana mfululizo tangu Juni 5, mwaka huu.
Licha ya wabunge kutaka kufahamu Serikali itazipataje Sh19 trilioni kugharimia Bajeti ya 2014/15, wakati imeshindwa kutimiza malengo ya kukusanya Sh18.2 trilioni kwa mwaka huu wa fedha unaomalizika Juni 30 mwaka huu, vyanzo hivyo vimekuwa siri kubwa. Bajeti ya mwaka huu wa fedha ina upungufu wa Sh1.8 trilioni.
Hata hivyo, habari kutoka katika kikao hicho zinaeleza kuwa usiri huo unatokana na Serikali kutokuwa na vyanzo vya uhakika vya mapato, jambo ambalo limewafanya kutotaka kuliweka wazi.
“Hakutakuwa na jipya katika upande wa vyanzo vipya vya mapato, tutarajie vyanzo vilevile vya Bajeti ya mwaka 2013/14 ambavyo vilitokana na kuongeza kodi katika vinywaji baridi; soda, bia na maji, pia katika sigara,” kilisema chanzo hicho.
Kutokuwa na vyanzo vya uhakika vya mapato kumekwamisha utekelezaji wa shughuli za maendeleo katika wizara zote kwani Bajeti ya mwaka 2013/14 imetekelezwa kati ya asilimia 25 hadi 35.Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba alisema hivi karibuni kuwa wizara yake inakusudia kupitia upya bajeti za wizara zote ili kuhamisha fedha kutoka katika matumizi yasiyo ya lazima ili zielekezwe katika mahitaji muhimu.
Katika kuthibitisha hilo, Kamati ya Bajeti na Serikali zilikubaliana kukata asilimia 7.5 ya fedha katika baadhi ya mafungu ya matumizi mengineyo (OC) kutoka katika wizara zote ili kuwezesha kupatikana kwa Sh230 bilioni ambazo zinahitajika kwa ajili ya maendeleo, hasa katika sekta tatu; afya, miundombinu na kilimo.
“Tunajibana ili fedha zipelekwe katika maji, elimu, miundombinu na afya. Zitakazobaki zitapelekwa katika maeneo mengine,” alisema Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji na Uwezeshaji), Dk Mary Nagu.
Katika Bajeti ya mwaka 2014/15, huenda Serikali ikaja na tozo mpya ili kupata fedha za kuanzisha mfuko wa maji kutokana na kelele zilizopigwa na wabunge, kwa maelezo kuwa ni idadi ndogo ya Watanzania wanaopata maji salama.
Jambo jingine linalosubiriwa kwa hamu ni ahadi ya Rais Jakaya Kikwete aliyoitoa katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi), ya kupandisha mishahara ya wafanyakazi.
Pia Rais aligusia kupunguzwa kwa Kodi ya Mapato ya Wafanyakazi (Paye) na kuahidi kuipunguza kutoka asilimia 13 ya sasa na kufikia tarakimu moja.

Wafanyabiashara wakubwa nao wanaisubiri Bajeti hiyo kujua kama watapata unafuu wa kodi ya mapato, huku wafanyabiashara wadogo wakitaraji kuondolewa kodi.
Hotuba ya Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti, Andrew Chenge kuhusu vyanzo vipya vya mapato nayo inasubiriwa na wananchi kujua kile kilichokuwa kikizua mjadala kati yake na Serikali.

Bajeti 2013/14
Katika Bajeti ya 2013/14, Serikali iliongeza kiwango cha ushuru wa mafuta kutoka Sh200 kwa lita hadi Sh263 kwa lita sawa na ongezeko la Sh63 kwa lita.
Pia ilipandisha kodi katika vinywaji baridi kutoka Sh83 kwa lita hadi Sh91; ongezeko la Sh8 kwa lita. Pia ilianzisha tozo ya mafuta ya petroli ya Sh50 kwa lita ambayo inakusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa ajili ya Mfuko wa Nishati Vijijini (Rea).
Mafuta ya dizeli yalipanda kutoka kiwango cha sasa cha Sh215 kwa lita hadi Sh217 kwa lita ikiwa ni ongezeko la Sh2, petroli ilipanda kutoka kiwango cha Sh339 kwa lita hadi Sh400. Maji ya matunda yaliyotengenezwa kwa matunda yanayozalishwa nchini yalipanda kutoka Sh8 kwa lita hadi Sh9 sawa na ongezeko la shilingi moja; huku juisi iliyotengenezwa kwa matunda yasiyozalishwa nchini ikipanda kutoka Sh100 hadi Sh110 kwa lita.
Bia inayotengenezwa kwa nafaka ya nchini na ambayo haijaoteshwa, ilipanda kutoka Sh310 hadi Sh341 kwa lita, sawa na ongezeko la Sh31, huku bia nyingine zote zikipanda kutoka Sh525 hadi Sh578 kwa lita.
Mvinyo uliotengenezwa kwa zabibu za ndani ya nchi kwa kiwango kinachozidi asilimia 75, ulipanda kutoka Sh145 hadi Sh160 kwa lita.
Vinywaji vikali, vilipanda kutoka Sh2,392 hadi Sh2,631 kwa lita.
Sigara zisizo na kichungi na zinazotengenezwa kutokana na tumbaku ya nchini kwa kiwango cha angalau asilimia 75, zilipanda kutoka Sh8,210 hadi Sh9,031 kwa sigara 1,000; sawa na ongezeko la senti 82 kwa sigara.
Zenye kichungi na zinazotengenezwa kutokana na tumbaku inayozalishwa nchini kwa kiwango cha angalau asilimia 75 kutoka Sh19,410 hadi Sh21,351 kwa sigara 1,000; likiwa ni ongezeko la Sh moja na senti 94 kwa sigara.
Sigara nyingine zenye sifa tofauti na zilizotajwa juu zilipanda kutoka Sh35,117 hadi Sh38,628 kwa sigara 1,000; ikiwa ni ongezeko la Sh tatu na senti 50 tu kwa sigara moja.


Wahisani kutoa Sh904 bilioni
Katika Bajeti hiyo, nchi wahisani zimeahidi kutoa Sh904 bilioni kwa ajili ya utekelezaji wake.
Ahadi hiyo ilitolewa jana na wahisani hao walipokutana na Kamati za Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Bajeti na Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), katika ukumbi wa bunge wa Pius Msekwa.
Mwenyekiti wa LAAC, Rajabu Mbarouk Mohamed alisema katika kikao cha wahisani hao kutoka nchi sita na Benki ya Dunia (WB), waliahidi kutoa fedha hizo.
“Kila mwaka tuna utaratibu wa kukutana na nchi wahisani ili kujua utekelezaji wa bajeti na kama tumefikia kwa kiwango gani katika utekelezaji,” alisema Rajabu.
Alisema katika mazungumzo hayo wafadhili hao walisema kwa miaka 10 mfululizo wamekuwa wakitoa fedha zote wanazoahidi kusaidia katika bajeti.

“Tuliwahoji kuhusiana na utekelezaji wa ahadi zao, wakatuambia kwa kipindi cha miaka 10 mfululizo wamekuwa wakitoa asilimia 100 ya kile wanachoahidi,” alisema.

CREDIT: http://www.mwananchi.co.tz/habari/Kitaifa/Kitendawili-cha-Bajeti-kuteguliwa-leo/-/1597296/2345250/-/item/2/-/hu37tcz/-/index.html

No comments:

Post a Comment