Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Saturday 17 May 2014

HOTUBA YA DK. ASHA-ROSE MIGIRO

HOTUBA YA WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA MHESHIMIWA ASHA-ROSE MTENGETI MIGIRO (MB) AKIWASILISHA BUNGENI MPANGO NA MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA FEDHA KWA MWAKA 2014/2015

A.   UTANGULIZI

1.    Mheshimiwa Spika, kufuatia taarifa iliyowasilishwa leo ndani ya Bunge lako tukufu na Mwenyekiti wa Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako tukufu likubali kupokea, kujadili na kupitisha Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa mwaka 2014/2015.

2.    Mheshimiwa Spika, ninasimama mbele ya Bunge lako tukufu kwa mara ya kwanza toka niteuliwe na Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, kuwa Waziri wa Katiba na Sheria. Kwa hiyo kabla ya kuwasilisha Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa mwaka 2014/2015, naomba nichukue fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kunipa heshima hii kubwa. Ninapenda kumhakikishia Mheshimiwa Rais na Watanzania wenzangu wote kwamba nitafanya kazi kwa bidii, uadilifu na kujituma kwa uwezo wangu wote.

3.    Mheshimiwa Spika, naomba sasa uniruhusu nitoe pole zangu za dhati kwako kufuatia vifo vya wabunge mahiri, Mheshimiwa Dkt. William Augustao Mgimwa, aliyekuwa Mbunge wa jimbo la Kalenga na Waziri wa Fedha wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania; na Mheshimiwa Saidi Ramadhani Bwanamdogo, aliyekuwa Mbunge wa jimbo la Chalinze. Mungu azilaze roho za marehemu mahali pema peponi.

4.    Mheshimiwa Spika, ninayo furaha  kuwapongeza wabunge wenzangu ambao ni wapya, Mheshimiwa Yusuf Salim Hussein, kwa kuchaguliwa kuwa Mbunge wa jimbo la Chambani; Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa kwa kuchaguliwa kuwa Mbunge wa jimbo la Kalenga; na Mheshimiwa Ridhiwani Jakaya Kikwete kwa kuchaguliwa kuwa Mbunge wa jimbo la Chalinze. Ninawatakia kheri na mafanikio katika majukumu yao mapya.

5.    Mheshimiwa Spikakwa namna ya pekee natoa pongezi na shukurani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda, Mbunge wa jimbo la Mpanda Mashariki, na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, kwa hotuba yake ambayo imetoa mwelekeo wa ujumla wa shughuli za Serikali kwa mwaka wa fedha 2014/2015.

6.    Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa hii pia kutoa shukurani zetu za dhati kwa Waheshimiwa Wajumbe wote wa Kamati ya  Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala chini ya uongozi mahiri wa Mwenyekiti wake Mheshimiwa William Mganga Ngeleja, Mbunge wa jimbo la Sengerema. Maoni, ushauri na maelekezo yao yameiwezesha Wizara yangu kutekeleza majukumu yake kwa mafanikio. Tutaendelea kuzingatia ushauri wa  Kamati hii wakati tukitekeleza malengo yetu kwa mwaka huu wa fedha na katika siku zijazo kwa ujumla.

7.    Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kumpongeza sana Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Mheshimiwa Jaji Joseph Sinde Warioba na Makamu wake Mheshimiwa Jaji Augustino Ramadhani kwa kuiongoza vema Tume hiyo. Ninawapongeza pia  wajumbe wote kwa kazi kubwa waliyoifanya. Rasimu ya Katiba waliyoiwasilisha imetuwekea msingi mzuri wa kujadili uandishi wa Katiba mpya, jambo ambalo lina mchango wa pekee katika kujenga mustakabali wa taifa letu. Ni matumaini yangu kwamba tutapata Katiba bora itakayotuongoza kwa miaka mingi  ijayo, itakayoimarisha umoja wetu na itakayoleta utangamano wa kitaifa na ustawi wa nchi yetu.
B.         MUUNDO NA MAJUKUMU YA WIZARA

8.        Mheshimiwa Spika, Wizara yaKatiba na Sheriainajumuisha Mahakama ya Tanzania, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Tume ya Kurekebisha Sheria,Tume ya Utumishi wa Mahakama, Wakala wa Usajili, Ufilisi, na Udhamini (RITA)Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo, na Chuo cha Uongozi wa Mahakama. Kwa pamoja taasisi hizi ndizo zinazotekeleza majukumu ya Wizara kama yalivyoainishwa kwenye Tangazo la Serikali Namba 20 la mwaka 2010.

9.        Mheshimiwa Spika,Wizara ya Katiba na Sheria kwa kuzingatia dira yake ya upatikanaji haki kwa watu wote na kwa wakati, inasimamia na kutekeleza majukumu yafuatayomasuala ya kikatiba na kisheria;  shughuli za uendeshaji wa mashauri na utoaji haki; utekelezaji wa haki za binadamu na utawala bora; shughuli za utafiti, urekebu na uandishi wa sheria; kuishauri na kuiwakilisha Serikali katika masuala ya kisheria ndani na nje ya nchi; shughuli za usajili, ufilisi na udhamini; kuratibu taasisi za mafunzo zilizo chini yake na kusimamia maslahi na maendeleo ya watumishi.


C.   MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA MPANGO NA BAJETI KWA MWAKA 2013/2014

10.       Mheshimiwa Spikakatika mwaka wa fedha 2013/2014 Wizara yangu ilitekeleza malengo iliyojiwekea ambayo ni yafuatayo: kuratibu mchakato wa mabadiliko ya Katiba; kusikiliza na kuendesha mashauri nchini;kusimamia masuala ya haki za binadamu na utawala bora; kutoa huduma za kisheria; kuhakiki na kushiriki majadiliano ya mikataba mbalimbali; uandishi wa sheria na hati za Serikali; kufanya tafiti na tafsiri ysheria;kuendesha shughuli za usajili, ufilisi na udhamini; na kuratibu mafunzo ya uanasheria kwa vitendo na uongozi wa Mahakama. Pia, Wizara iliboresha miundombinu ya utoaji haki; ilitoa elimu na habari kuhusu upatikanajihaki kwa jamii; iliratibu shughuli za maboresho ya Sekta ya Sheria na kuimarisha usimamizi na uwajibikaji katika matumizi ya rasilimali za ummaUtekelezaji wa majukumu hayo umefanyika kwa mafanikio na viwango mbalimbali vya utekelezaji.

Kuratibu Mchakato wa Mabadiliko ya Katiba

11.       Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha kwamba nchi yetu inakuwa na mfumo imara wa sheria unaozingatia mahitaji ya wakati tulionao, Wizara ya Katiba na Sheria ilisimamia na kuratibu mchakato wa kihistoria wa kuandika Katiba. Tofauti na michakato miwili iliyopita (mwaka 1965 na mwaka 1977), safari hii mchakato wa kuandika Katiba ulihusisha watu wengi zaidi. Wananchi wameshiriki moja kwa moja kwa kutoa maoni yaombele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba au kwa maandishi. Hali kadhalika watashiriki kufanya uamuzi wa mwisho kuhusu Katiba inayopendekezwa kupitia kura ya maoni. Aidha, wananchi walipata fursa ya kupendekeza majina ambayo Mheshimiwa Rais aliyazingatia katika kufanya uteuzi wa wajumbe wa Tume.

12.       Mheshimiwa Spika, Tume hii ilifanya kazi ya kukusanya maoni kutoka kwa wananchi moja kwa moja na kupitia mabaraza ya Katiba ya wilaya na ya kitaasisi. Baada ya zoezi hili Tume iliandaa Ripoti iliyojumuisha Rasimu ya Katiba. Ripoti hiyo iliwasilishwa kwa Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, na Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi mnamo tarehe 30 Desemba, 2013.

13.       Mheshimiwa Spika, baada ya kupokea Ripoti ya Tume, Mheshimiwa Rais aliitisha Bunge Maalum ambalo lilianza kazi rasmi kwa kupokea Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Mheshimiwa Jaji Joseph Sinde Warioba tarehe 18 Machi, 2014. Tume ilihitimisha kazi zake na kuvunjwa rasmi kwa Tangazo la Serikali Namba 81 la tarehe 21 Machi, 2014.


14.           Mheshimiwa Spika,Bunge Maalum lilizinduliwa rasmi na Mheshimiwa Rais tarehe 21 Machi 2014. Hadi sasa Bunge Maalum limefanya kazi ya kuandaa Kanuni za kusimamia uendeshaji wa shughuli zake za kila siku. Aidha, Bunge Maalum limejadili Sura ya Kwanza na Sura ya Sita ya Rasimu ya Katiba kama hatua za awali za uchambuzi wa Rasimu hiyo.

Kuimarisha Haki za Binadamu na Utawala Bora

15.    Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2013/2014 Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora imetoa elimu kwa umma katika masuala ya haki za binadamu na utawala bora. Elimu iliyotolewa ilihusu sheria za ardhi na umiliki wa mali, ambapo wananchi 8,529 kutoka katika kata 69 na Shehia 7 walifikiwa. Pamoja na kutoa elimu, Tume ilipokea malalamiko 923 ya aina mbalimbali katika kipindi hicho yakiwemo yale yanayohusu migogoro ya ardhi. Kati ya malalamiko hayo, malalamiko 324 yalishughulikiwa na kutolewa uamuzi.

16.    Mheshimiwa Spika, Tume iliandaa Mwongozo wa Utawala Bora wenye lengo la kukuza uelewa katika eneo hili. Jumla ya nakala 25,000 za Mwongozo huo zilisambazwa kwa watendaji wa ngazi za vijiji na kata ili waweze kuzingatia misingi ya utawala bora na haki za binadamu wakati wanapotekeleza majukumu yao.

17.    Mheshimiwa Spika, hadhi ya Tanzania kuhusu haki za binadamu imeendelea kuwa nzuri ndani na nje ya nchi yetu. Ni wajibu wa Wizara yangu kukuza na kuendeleza mafanikio yaliyokwishapatikana. Wizara imekamilisha Rasimu ya Taarifa ya utekelezaji wa masuala ya haki za binadamu hapa nchini ambayo itawasilishwa kwenye Kamisheni ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu. Taarifa hiyo inaeleza namna ambavyo Serikali yetu inatekeleza mikataba mbalimbali ya kitaifa, kikanda na kimataifa katika kukuza na kulinda haki hizo.

18.    Mheshimiwa Spikakatika kipindi cha 2013/2014, Wizara iliandaa Mpango Kazi wa Kitaifa wa Haki za Binadamu (2013–2017) uliozinduliwa na Makamu wa Rais Mheshimiwa, Dkt. Mohamed Gharib Bilal, tarehe 10 Desemba, 2013. Wizara yangu ina wajibu wa kusimamia na kuratibu utekelezaji wa Mpango Kazi huu katika taasisi kadhaa za umma na za kijamii. Kupitia Mpango huu wadau mbalimbali watapata fursa ya kujadili na kutekeleza masuala ya haki za binadamu. Pia ni fursa kwa Wizara kuimarisha usimamizi na ufuatiliaji wa masuala mbalimbali yanayohusu haki za binadamu na utawala bora.

19.    Mheshimiwa Spika, uzinduzi huo ulikwenda sambamba na uzinduzi wa Mpango Mkakati wa Miaka Mitano wa Haki za Watoto (2013-2017). Mpango huo uliandaliwa kutokana na tafiti mbili zilizofanywa juu ya upatikanaji haki kwa watoto wanaokutana na mkono wa sheria na hali ya watoto wanaokinzana na sheria. Matokeo ya tafiti hizo yaliwezesha kubaini vipaumbele vya kimkakati ndani ya mkakati wenyewe na hatua madhubuti zinazopaswa kuchukuliwa katika kipindi cha miaka mitano ya utekelezaji wa Mpango huo.

20.    Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inaratibu shughuli za Kamati ya Kitaifa ya Kuzuia Mauaji ya Kimbari iliyoundwa chini ya Itifaki ya nchi za Maziwa Makuu ya kuzuia mauaji ya kimbari. Kamati hii ina jukumu la kujenga uelewa na kuishauri Serikali juu ya viashiria vinavyoweza kuathiri amani na kusababisha vitendo vya ukatili kwa binadamu. Katika kipindi cha mwaka 2013/2014, pamoja na kutoa elimu kwa umma juu ya masuala ya amani kupitia redio na luninga, Wizara imewajengea uwezo viongozi wa dini na madhehebu mbalimbali katika kulinda amani katika mikoa ya Arusha, Mbeya, Mwanza, Mjini Magharibi, Morogoro na Tanga. Katika mikoa hii, viongozi wa dini waliunda Kamati za amani zenye wajumbe kutoka dini na madhehebu mbalimbali. Kamati hizi zina jukumu la kuhakikisha amani inadumishwa katika mikoa hiyo.

21.    Mheshimiwa Spika, katika uendeshaji wa shughuli zake, azma ya Serikali ni kuongeza uwazi katika ngazi zote za utendaji. Ili kufikia lengo hilo Serikali ilijiunga na Mpango wa Kimataifa wa uendeshaji wa Serikali kwa Uwazi (Open Government Partnership) mwaka 2011. Tamko la Tanzania katika kutelekeza matakwa ya ubia huu ni kuweka mazingira ya upatikanaji wa taarifa kuhusu shughuli zinazofanywa na Serikali. Wizara yangu iliandaa Rasimu ya Waraka wa Baraza la Mawaziri wa mapendekezo ya kutunga sheria ya haki ya kupata taarifa kutoka  katika taasisi za umma kwa lengo la kuongeza uwazi na uwajibikaji wa Serikali.

22.    Mheshimiwa Spika, pamoja na hali nzuri ya utawala bora na kuzingatiwa kwa haki za binadamu katika nchi yetu, hivi karibuni kumekuwa na tuhuma nzito kuhusu ukiukwaji wa haki za binadamu. Tuhuma hizo zilitokana na utekelezaji wa “Operesheni Tokomeza” ambayo ililenga kuwasaka na kuwafikisha kwenye vyombo vya Sheria watu wote waliokuwa wanajihusisha na vitendo vya ujangili katika hifadhi za taifa na mapori tengefu. Kwa kuzingatia uzito wa tuhuma hizo Mheshimiwa Rais ameunda Tume ya Uchunguzi chini ya Sheria inayohusu uundwaji wa Tume za Uchunguzi (Commissions of Inquiry Act, Cap. 32). Kuundwa kwa Tume hiyo kulitangazwa katika Gazeti la Serikali na. 131 la tarehe 2 Mei, 2014. Tume hiyo yenye makamishna watatu (3) imepewa hadidu za rejea ambazo ni:

(i)                 Kuchunguza namna Operesheni Tokomeza ilivyofanyika;
(ii)              Kuchunguza kama maofisa walioendesha Operesheni hiyo walifuata sheria, taratibu na hadidu za rejea walizopewa;
(iii)            Kuchunguza endapo maofisa walioendesha Operesheni hiyo walivunja sheria, taratibu na hadidu za rejea zilizotolewa;
(iv)            Kuchunguza kama kuna watu waliovunja sheria wakati wa Operesheni hiyo na kuona kama hatua walizochukuliwa wenyewe au mali zao zilikuwa sahihi;
(v)               Kushauri hatua zinazopaswa kuchukuliwa kwa mtu yeyote aliyevunja sheria, taratibu na kwenda kinyume na hadidu za rejea zilizokuwepo katika kutekeleza Operesheni hiyo;
(vi)            Kushauri mambo yanayopaswa kuzingatiwa wakati wa kuandaa Operesheni nyingine kama hiyo ili mambo yaliyojitokeza katika Operesheni hii yasijirudie.

Kusikiliza na kuendesha mashauri nchini

23.       Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia Dira ya upatikanaji haki kwa watu wote na kwa wakati, Wizara yangu imeongeza kasi ya kuendesha na kusikiliza mashauri yaliyosajiliwa Mahakamani. Kasi hiyo imetokana na mikakati mbalimbali na malengo mahsusi ambayo Mahakama ya Tanzania imejiwekea ya kusikiliza mashauri kwa ngazi zote za Mahakama. Utaratibu huu unaweka wastani wa idadi ya mashauri yatakayosikilizwa na kila ngazi ya Mahakama kwa kila mwaka. Katika Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu lengo ni kumaliza mashauri mapya ndani ya miezi 24, Mahakama ya Hakimu Mkazi katika muda usiozidi miezi 18 na Mahakama ya Mwanzo  kumaliza mashauri mapya ndani ya miezi 12.

24.       Mheshimiwa Spika, mkakati huu umesaidia kupunguza mlundikano wa mashauri kwa kiasi kikubwa ambapo hadi kufikia Desemba, 2012 Mahakama ya Tanzania ilikuwa na jumla ya mashauri 114,278 yaliyohusu masuala ya madai, jinai na ardhi. Katika mwaka 2013 Mahakama ilisajili mashauri mapya ya aina hiyo 168,068 na kufanya idadi ya mashauri yaliyokuwepo kufikia 282,346. Hadi mwezi Desemba 2013 jumla ya mashauri 182,237 yalisikilizwa na kutolewa uamuzi, sawa na asilimia 65 ya mashauri yote yaliyosajiliwa mahakamani. Mashauri yaliyobaki Mahakamani ni 100,109. (Kiambatisho “A”).

25.       Mheshimiwa Spika, mkakati huu umeanza kwa mafanikio ambapo hivi sasa mashauri mengi yanayosajiliwa Mahakamani yamekuwa yakimalizika katika kipindi kisichozidi miaka miwili. Wizara yangu itaendelea kubuni njia mbalimbali zitakazosaidia kuondokana na tatizo la mlundikano wa mashauri na ambalo linaathiri utoaji haki. 

26.       Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inaratibu na kusimamia utekelezaji wa mpango wa kutenganisha kazi ya upelelezi wa jinai na uendeshaji wa mashtaka. Baadhi ya mafanikio yaliyopatikana hadi sasa ni pamoja na kupungua kwa tuhuma za wananchi za kubambikiziwa kesi katika Mahakama ambazo Mawakili wa Serikali wanaendesha mashauri ya jinai na kupungua kwa idadi ya wafungwa na mahabusu magerezani. Kabla ya kuanza kwa mpango huu, mwaka 2007 kulikuwa na wafungwa 22,622 na mahabusu 20,210. Tangu wakati huo idadi ya wafungwa na mahabusu imekuwa ikipungua kadri Wizara inavyoendelea kueneza utekelezaji wa mpango huu katika mikoa na wilaya mbalimbali. Katika mwaka wa fedha wa 2013/2014 idadi ya wafungwa ilipungua kutoka 16,869 mwezi Juni 2013 hadi wafungwa 15,659 mwezi Machi 2014 na idadi ya mahabusu ilipungua kutoka 17,046 mwezi Juni 2013 na kufikia mahabusu 16,647 mwezi Machi 2014.

27.       Mheshimiwa Spika,  Kurugenzi ya Mashtaka pamoja na Mahakama ya Tanzania zimeanza kutekeleza utaratibu maalum wa kukamilisha usikilizaji wa mashauri 28 ya dawa za kulevya yaliyosajiliwa Mahakama Kuu. Mashauri haya yamepangwa kusikilizwa katika kikao maalumu cha Mahakama Kuu kitakachofanyika kuanzia mwezi Juni 2014. Mashauri 110 yapo Mahakama za wilaya na mikoa kwa hatua za awali za kuyaandaa ili yahamishiwe Mahakama Kuu kwa ajili ya kusikilizwa. Mashauri haya ni yale yenye thamani inayoanzia shilingi milioni kumi na kuendelea.

28.       Mheshimiwa Spika, Wizara inaendelea na utekelezaji wa mkakati maalumu wa kusikiliza mashauri 9 yajinai ya wizi wa shilingi bilioni 29.8 zilizokuwa katika akaunti ya madeni ya nje (external payments arrears account - EPA) iliyokuwa Benki Kuu. Hivi sasa Kurugenzi ya Mashtaka inaendesha jumla ya mashauri 14 yanayotokana na makosa ya utakatishaji wa fedha kiasi cha shilingi bilioni 56zilizopatikana kwa njia ya uhalifu,na mashauri mengine 70 ya kukutwa na nyara za Serikali, zenye thamani ya shilingi bilioni 45 kinyume cha sheria.

29.       Mheshimiwa Spika, kufikia mwezi Aprili 2014 kulikuwa na jumla ya majalada 404 ya uchunguzi wa makosa mbalimbali ya rushwa yaliyowasilishwa katika Kurugenzi ya Mashtaka kutoka TAKUKURU.  Kati ya hayo, majalada 202 yaliandaliwa hati za mashtaka, 103 yalirudishwa TAKUKURU  kwa ajili ya uchunguzi zaidi, na majalada 98 yanaendelea kufanyiwa uchambuzi.

30.       Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/2014 Wizara ikishirikiana na taasisi mbalimbali iliongeza jitihada zake za kukabiliana na vitendo viovu wanavyofanyiwa watu wenye ulemavu wa ngozi. Jitihada hizi zimechangia kiasi kikubwa kupungua kwa idadi ya matukio ya aina hii katika kipindi cha Julai 2013 hadi Mei 2014, ambapo hakuna tukio lolote lililoripotiwa Polisi. Hali hii ni tofauti na mwaka wa fedha 2012/2013 ambapo matukio matatu yaliripotiwa Polisi. Hivi sasa Wizara yangu inaendelea na mashauri 9 ya aina hiyo yanayotokana na matukio ya miaka ya nyuma.

31.       Mheshimiwa Spika, kuhusu mashauri ya ukiukwaji wa  Haki za Binadamu, Wizara yangu  iliendesha mashauri 6 kwenye Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu iliyopo Arusha. Mashauri haya yanajumuisha mashauri 4 mapya ambayo bado yanaendelea na mashauri 2 ambayo yametupiliwa mbali na Mahakama hiyo kutokana na waombaji kutotimiza matakwa ya sheria.

32.       Mheshimiwa Spika, jumla ya mashauri ya madai ambayo Serikali ilishitaki au kushitakiwa, na yale yanayohusu Katiba yaliyokuwa Mahakama Kuu, Mahakama ya Rufani na katika mabaraza ya usuluhishi (mediation and arbitration)  katika kipindi cha Julai 2013 hadi Aprili 2014 ni 750. Kati ya  hayo mashauri yaliyosikilizwa na kutolewa uamuzi ni 89. Serikali ilishinda mashauri 77 yenye thamani ya Shilingi 2,216,502,356,629 na kuokoa kiasi hicho cha fedha. Serikali ilishindwa mashauri 12 yenye thamani ya Shilingi 25,986,416,661.

33.       Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada za Serikali za kupambana na vitendo vya uhalifu, bado kumekuwepo na matukio ambayo baadhi ya watu wamejipatia mali kinyume cha sheria. Kwa kutambua hilo, Wizara yangu imekuwa ikitenga fedha kwenye mipango yake ya mwaka kwa ajili ya kujenga uwezo wa Kitengo cha utaifishaji na urejeshaji wa mali zilizopatikana kwa njia ya uhalifu (Assets Recovery and Forfeiture Section).Kati ya Julai 2013 na Machi 2014, Mahakama iliamuru kurejeshwa  Serikalini jumla ya mali na fedha zinazofikia thamani ya zaidi ya shilingi milioni 233 baada ya watuhumiwa kutiwa hatiani.

Kuimarisha utoaji wa huduma za kisheria

34.       Mheshimiwa Spika, Wizara imeboresha mazingira ya upatikanaji haki kwa wananchi ikitambua kuwa uwakilishi mbele ya vyombo vya sheria ni haki ya msingi. Katika kipindi cha Julai 2013 hadi Machi 2014 Wizara iliandaa Rasimu ya Waraka wa Kutunga Sheria ya Huduma ya Msaada wa Kisheria ili kuwapa fursa wananchi kupata msaada wa kisheria. Rasimu ya Waraka huo imewasilishwa Serikalini. Sheria hii itakapotungwa itawawezesha wananchi wengi wasio na uwezo kupata ushauri na kuwakilishwa katika vyombo vya sheria.

35.       Mheshimiwa Spika,  wakati utaratibu wa kutunga sheria hii ukiwa unaendelea, Wizara imeanzisha chombo cha mpito kijulikanacho kama Sekretarieti ya Msaada wa Kisheria, ili kuratibu utoaji wa msaada wa kisheria kwa wananchi. Katika kipindi cha mwaka wa fedha 2013/2014 jumla ya wananchi 12,809 walipata huduma ya msaada wa kisheria kupitia Sekretarieti hii.

Kuhakiki na kushiriki majadiliano ya mikataba mbalimbali

36.       Mheshimiwa Spika, kwa upande wa mikataba, Wizara yangu imetoa ushauri wa kisheria kwa Serikali unaozingatia ubora na weledi, na pia imeendelea kushiriki katika majadiliano mbalimbali ya mikataba ya kibiashara, mikutano ya kitaifa, kikanda na kimataifa kwa manufaa ya nchi. Katika kipindi cha Julai 2013 hadi Machi 2014, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ilitekeleza jukumu hili kwa kushiriki katika mikutano ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika, Nchi za Umoja wa Afrika, Jumuiya ya Ulaya na Umoja wa Mataifa.

37.       Mheshimiwa Spika, ili kulinda maslahi ya nchi katika mikataba kati ya Serikali na wadau mbalimbali, Serikali imefanya mabadiliko ya Sheria ya Ununuzi (Public Procurement Act, 2011).  Pamoja na mambo mengine, Sheria hii inazitaka wizara, taasisi na idara za Serikali kupata ushauri wa kisheria kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kabla ya kufunga mkataba wowote wenye thamani ya zaidi ya Shilingi milioni 50. Mabadiliko haya yamechangia kuongezeka kwa mikataba inayowasilishwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa ajili  ya kuhakikiwa, kutoka mikataba 120 mwaka 2013 hadi mikataba 375 kufikia Machi 2014. Hali hii imeiepusha Serikali na mikataba isiyo na maslahi kwa taifa.

Uandishi wa sheria na hati za Serikali

38.       Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2013/2014, Wizara yangu iliandaa jumla ya miswada 11 iliyojadiliwa na kupitishwa na Bunge lako tukufu kuwa sheria. Miswada hiyo ilihusu: Sheria ya Fedha na Sheria ya Matumizi ya Fedha inayopitishwa wakati wa Bunge la Bajeti; Sheria ya Taifa ya Umwagiliaji; Sheria ya Vyama vya Ushirika; Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na Sheria ya Kura ya Maoni. Miswada mingine ni Sheria ya Mfuko wa Akiba ya Wafanyakazi Serikalini, Sheria ya Takwimu, Sheria ya Marekebisho ya Ushuru na Bidhaa na Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 1) na (Na. 2). Aidha, Sheria Ndogo 136 zilitayarishwa na kuchapishwa katika Gazeti la Serikali tayari kuanza kutumika.

Kufanya utafiti na tafsiri ya sheria

39.        Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2013/2014, Tume ya Kurekebisha Sheria ilifanya mapitio na utafiti wa mifumo ya sheria mbalimbali. Utafiti wa kwanza ulihusu mfumo wa sheria wa utatuzi wa migogoro ya ardhi. Utafiti huu umekamilika na Ripoti yake imekabidhiwa kwa Waziri wa Katiba na Sheria. Ni azma ya Wizara yangu kuipitia Ripoti hii kwa kushirikiana na Wizara nyingine zinazoshughulika na utatuzi wa migogoro ya ardhi. Utafiti wa pili ulihusu mfumo wa sheria inayosimamia huduma ya hifadhi ya jamii kwa wazee. Mwisho, Tume ilifanya utafiti kuhusu sheria zinazolinda watumiaji wa bidhaa na huduma ili kubaini upungufu uliopo.

40.       Mheshimiwa Spika,  ufanisi katika utekelezaji wa sheria unategemea sana uelewa wa wananchi kuhusu sheria hizo. Kwa kutambua hiloWizara imetafsiri Sheria 7 kutoka Kiingereza kwenda lugha ya Kiswahili.Wizara itaendelea kutafsiri Sheria nyingi zaidi kwa kuzingatia mahitaji ya jamii na uwezo uliopo. Wizara inapenda kutoa mwito kwa wadau mbalimbali ndani na nje ya Serikali kuchangia katika kuhamasisha wananchi kuwa na mwamko wa kupenda kusoma na kuzifahamu sheria za nchi. (Kiambatisho “B”).

41.       Mheshimiwa Spikakatika kuimarisha ustawi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Wizara yangu kwa kushirikiana na nchi wanachama imeendelea kufanya mapitio ya Sheria zinazosimamia haki za ubunifu na haki miliki (Intellectual property laws). Lengo ni kuhakikisha kuwa sheria za nchi wanachama zinawiana na sheria za Jumuiya hiyo kama ambavyo  nchi hizo zimekubaliana katika kutekeleza Itifaki ya Soko la Pamoja.

Kuimarisha shughuli za Usajili, Ufilisi na Udhamini

42.       Mheshimiwa Spika, usajili wa matukio muhimu ya binadamu (vizazi, vifo, ndoa, talaka na watoto wa kuasili) unalenga kulinda na kuhifadhi haki za binadamu na za uraia. Aidha, usajili huu unaiwezesha Serikali kupata takwimu sahihi kwa ajili ya mipango mbalimbali ya maendeleo. Katika kipindi cha kuanzia Julai 2013 hadi Machi 2014 Wizara imeboresha mfumo wa usajili wa vizazi kwa kusogeza huduma  hii hadi ngazi za chini kama vile kata na vituo vya tiba. Maboresho haya yamefanyika kupitia Mpango wa usajili wa vizazi kwa watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano uliozinduliwa rasmi mkoani Mbeya mwezi Julai 2013.

43.       Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa mpango huu umeongeza idadi ya watoto wa umri chini ya miaka mitano waliopatiwa vyeti vya kuzaliwa kutoka watoto 37,090 kabla ya mpango huu kuanza, hadi 169,477 Machi 2014.  Hii ni sawa na ongezeko la  asilimia 31.4 la watoto wote wa umri wa chini ya miaka mitano mkoani humo. Mbali na usajili huu mkoani Mbeya, Wizara imefanya usajili wa kawaida katika sehemu nyingine za Tanzania bara wa jumla ya vizazi 493,887, ndoa 14,031, talaka 53, vifo 34,460, na watoto wa kuasili 30. Hali kadhalika jumla ya hati 182 za wadhamini wa vyama vya siasa, makanisa, misikiti na mali za vikundi vya kijamii zilisajiliwa.(Kiambatisho “C”)


Kuimarisha Taasisi za Mafunzo ya Sheria

44.       Mheshimiwa Spika,  kwa mwaka wa fedha 2013/2014 Wizara imeimarisha  taasisi ya mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo na Chuo cha Uongozi wa Mahakama. Hadi kufikia Machi 2014, jumla ya wanafunzi 293 walihitimu mafunzo ya uanasheria kwa vitendo na kustahili kusajiliwa kuwa mawakili, ikilinganishwa na mwaka 2012/2013 ambapo wahitimu walikuwa 272. Jumla ya wanafunzi 896 walihitimu mafunzo kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama, kati ya hao wahitimu 267 walitunukiwa Stashahada ya Sheria na 629 Cheti cha Sheria. Vile vile, Wizara imeanzisha Tawi la Chuo cha Uongozi wa Mahakama katika jiji la Mwanza na kudahili wanafunzi 95 kwa mara ya kwanza mwaka 2013/2014. Jitihada hizi zitaongeza idadi ya watalaam wenye sifa za kuajiriwa katika fani mbalimbali za sheria.

Kuboresha miundombinu ya utoaji haki

45.       Mheshimiwa Spika, ubora wa huduma unaotolewa na taasisi za sheria unategemea ubora wa mazingira na miundombinu ya utoaji haki. Kwa kuzingatia umuhimu huo, katika kipindi cha Julai 2013 hadi Machi 2014, Wizara imefanya yafuatayo:-
·        Imekarabati masijala kwenye Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu Kanda za Dar es Salaam na Mtwara;
·        Imepata washauri elekezi kwa ajili ya kukarabati Mahakama  za Mwanzo 10, na kujenga Mahakama za Mwanzo 25. Utaratibu wa kupata wakandarasi  umetangazwa kwenye magazeti ya tarehe 11 na 12 Mei 2014;
·        Imejenga uzio wa Mahakama Kuu Kanda ya Bukoba; kutenga vyumba vya ofisi za majaji na makatibu muhtasi; na kuziba sehemu ya wazi ya paa;
·        Imeboresha masijala 71 za Mahakama za Mwanzo kwa kuziwekea mfumo wa kielektroniki wa kutunza kumbukumbu za majalada;
·        Imekamilisha ukarabati wa Mahakama za Mwanzo za Mgandu na Mwamagembe katika mkoa wa Singida;
·        Inakamilisha ujenzi wa bweni la wanafunzi katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama;
·        Imefungua ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali katika mkoa  wa Geita; na inakamilisha taratibu za kuanza ukarabati wa Ofisi katika mikoa ya Simiyu na Katavi;
·        Imekamilisha ujenzi wa jengo la Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini;
·        Imekamilisha upembuzi yakinifu wa  mradi wa mfumo mpana wa mawasiliano (Wide Area Network) utakaounganisha Makao Makuu ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Kurugenzi ya Mashtaka na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali mkoa ya Dar es Salaam.

46.       Mheshimiwa Spika, upembuzi yakinifu kuhusu mradi wa e-justiceutakaorahisisha uendeshaji wa mashauri ya jinai umekamilika.  Mradi huu utaunganisha Mahakama, Magereza na Ofisi za mikoa za Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa njia ya mtandao. Ripoti ya zoezi hili imewasilishwa Ofisi ya Rais -Tume ya Mipango na Wizara ya Fedha kwa hatua za maamuzi.

47.       Mheshimiwa Spika, Wizara imetumia fursa za maendeleo zinazotokana na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika kuboresha huduma zinazotolewa. Mahakama ya Tanzania imejiimarisha katika matumizi ya TEHAMA kwa kuanzisha mfumo endelevu wa upatikanaji wa takwimu mbalimbali za Mahakama. Mfumo huo umeanza kufanya kazi katika Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu katika Divisheni za Biashara, Kazi na Ardhi, na Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam. Itakapofika Desemba 2014 Mahakama Kuu zote nchini, mahakama za mikoa na mahakama zote za wilaya zitatumia TEHAMA katika ukusanyaji na utunzaji wa takwimu.

48.       Mheshimiwa Spika, Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini umeanzisha utaratibu wa kupokea taarifa za usajili wa vizazi kupitia simu za mkononi mara tu mtoto anaposajiliwa kwenye kata au kituo cha tiba. Hivi sasa utaratibu huu unafanyika mkoani Mbeya kupitia mpango wa kusajili watoto walio na umri wa chini ya miaka mitano (U5BRI). Sambamba na hilo mwananchi yeyote nchini anaweza akapata taarifa za huduma za RITA kupitia simu za mkononi kwa kutuma neno RITA kwenda namba 15584 na Tovuti  ya Wakala (www.rita.go.tz).

Elimu kwa Umma

49.       Mheshimiwa Spika, Wizara inatambua kuwa wananchi wana nafasi muhimu katika kuimarisha utawala wa sheria, misingi ya haki za binadamu na utawala bora. Kwa kuzingatia hilo, Wizara imetoa elimu kwa umma kwa njia mbalimbali zikiwemo redio na luninga. Katika kipindi cha mwaka wa fedha 2013/2014 Wizara ilirusha vipindi 35 vya redio na vipindi 9 vya luninga vilivyotoa elimu kuhusu mapambano na rushwa; haki za watoto na misingi ya haki za binadamu na utawala bora. Vile vile, Wizara iliandaa mikutano ya wadau katika mikoa ya Rukwa na Tanga kwa lengo la kuwajengea uelewa wa sheria. Pia Wizara ilishiriki maonesho ambapo jumla ya vitabu 25,000 na vipeperushi 2,800 kuhusu haki za binadamu na misingi ya utawala bora vilisambazwa. Katika mikutano hiyo, vitabu 500 na vipeperushi 1000 kuhusu historia ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania na majukumu ya Wizara vilisambazwa.

Uratibu na Utekelezaji wa Maboresho ya Sekta ya Sheria

50.       Mheshimiwa Spika, Wizara yangu imetekeleza na kuratibu programu na miradi mbalimbali ya kuboresha Sekta ya Sheria. Utekelezaji wa Programu ya Maboresho ya Sekta ya Sheria unalenga kuimarisha mifumo ya utoaji haki na kukuza uwezo wa taasisi za sheria katika kutoa huduma bora. Hadi sasa Programu hii imewezesha, pamoja na mambo mengine, kutenganishwa kwa shughuli za upelelezi na mashtaka, kufanya mapitio ya sheria mbalimbali na kuanzishwa kwa Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo.

51.       Mheshimiwa Spika,  katika kipindi cha Julai 2013 hadi Machi 2014, shughuli nyingine muhimu za kuboresha sekta ya sheria zilizotekelezwa ni pamoja na:- kufanya tathmini ya hali ilivyo sasa na kuishauri Serikali namna ya kuendeleza maboresho katika sekta ya sheria; kuimarisha utendaji wa Sekretarieti ya Huduma ya Msaada wa Kisheria; kuratibu uanzishwaji wa maeneo ya kuhifadhi watoto waliokinzana na sheria ili kulinda haki zao, na kuimarisha madawati ya jinsia na watoto katika vituo vya Polisi na Magereza.

52.       Mheshimiwa Spika, maboresho ya sekta ya sheria ni pamoja na mapambano na rushwa. Wizara yangu ni moja ya taasisi zinazotekeleza mradi wa Uimarishaji wa Mapambano na Rushwa Tanzania (Strengthening Tanzania Anti-Corruption Action - STACA) unaolenga kuziba mianya ya rushwa katika taasisi zake. Mradi huu ulianza kutekelezwa mwaka wa fedha 2011/2012 na unatarajia kukamilika mwaka 2014/2015. Kwa kipindi cha mwaka wa fedha 2013/2014 jumla ya pikipiki 214 zilinunuliwa kwa ajili ya Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo kwa nia ya kuondoa kero ya usafiri na kuongeza kasi ya usikilizaji wa mashauri. Pia jumla ya masijala 68 za Mahakama za Mwanzo ziliboreshwa kwa kuwekewa mfumo wa kielektroniki wa kutunza kumbukumbu za majalada. Mfumo huo umerahisisha upatikanaji wa taarifa za kimahakama na hivyo kuondoa mianya ya rushwa.

53.       Mheshimiwa Spika, kupitia mradi huu kitengo cha utaifishaji na urejeshaji wa mali zilizopatikana kwa njia ya uhalifu (Assets Recovery and Forfeiture Section) kimeimarishwa kwa kupatiwa vitendea kazi ambavyo vimesambazwa katika ofisi za Mikoa na Wilaya za Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Vifaa hivyo ni kompyuta 35, mashine za uchapishaji, vitabu vya rejea na samani za ofisi. Hali kadhalika  mawakili 64 wa Serikali  wamepatiwa mafunzo kuhusu stadi za kuendesha mashauri ya rushwa na namna ya kushughulikia mali zinazopatikana kwa njia ya rushwa. Kwa kuwa Kurugenzi ya Mashtaka ni kiungo muhimu katika uendeshaji wa kesi na upelelezi, Kurugenzi iliandaa mikutano ya kikazi na kiutendaji na wadau mbalimbali chini ya Jukwaa la Haki Jinai. Vikao hivyo vilikuwa kati ya Mawakili wa Serikali Wafawidhi, Wakuu wa Upelelezi wa Mikoa na Vikosi Tanzania Bara, TAKUKURU, Mkemia Mkuu wa Serikali, Idara ya Uhamiaji, Idara ya Wanyamapori na Tume ya Uratibu wa Dawa za Kulevya. Lengo la mikutano hiyo lilikuwa ni kuboresha uchunguzi na uendeshaji wa mashtaka. Ubia huu unasaidia kukusanya  nguvu pamoja ili kuleta ufanisi zaidi katika utendaji.

54.       Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/2014, Wizara yangu ilichukua hatua za kuziimarisha Kamati za Maadili za Mahakama za mikoa na wilaya. Tume ya Utumishi wa Mahakama ilifanya ukaguzi wa Kamati za Maadili za Mahakama kwenye ngazi ya mkoa na wilaya katika mikoa ya Iringa, Njombe na Ruvuma. Katika ukaguzi huo, Tume ya Utumishi wa Mahakama ilibaini changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na ukosefu wa fedha. Wizara imeanza kukabiliana na changamoto hiyo kwa kuzipatia fedha Kamati za Maadili za Mahakama ngazi za mikoa na wilaya. Katika mwaka wa 2013/14 jumla ya shilingi 36,000,000 zilitolewa kwa mikoa 18 na shilingi 136,500,000 kwa wilaya 91.

Kwa upande wa mawakili, Kamati ya Maadili ya Mawakili wa Kujitegemea (Advocates’ Committee) ilishughulikia malalamiko 18 katika kipindi cha Julai 2013 hadi Aprili 2014. Kati ya hayo, malalamiko 6 yamekwishatolewa uamuzi.

55.       Mheshimiwa Spika, Wizara yangu imewajengea uwezo watumishi waliopo na kuajiri watumishi wapya ili kuleta tija na ufanisi katika kutekeleza majukumu yake. Katika kipindi cha Julai 2013 hadi Machi, 2014 Wizara iliajiri watumishi wapya 541; ilipandisha vyeo watumishi 487; na kuwezesha watumishi 1,081  wa kada mbalimbali kupata mafunzo ya muda mrefu na mfupi ndani na nje ya nchi.

Utekelezaji wa masuala mtambuka

56.       Mheshimiwa Spika, Wizara ya Katiba na Sheria inazingatia masuala mtambuka katika utekelezaji wa majukumu yake. Haya ni kama vile kuingiza masuala ya jinsia katika sera, mipango na uendeshaji; kuzingatia mahitaji ya watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI; na masuala yanayohusu maadili. Kwa upande wa kuzingatia jinsia katika ajira jumla ya watumishi 541 waliajiriwa. Kati yao wanawake ni 241 (44.5%) na wanaume ni 300 (55.5%). Vile vile, jumla ya watumishi 487 walipandishwa vyeo ambapo wanawake walikuwa 217 (44.56%) na wanaume walikuwa 270 (55.44%).  Aidha, jumla ya watumishi waliopata mafunzo ni 1,081 kati yao wanawake  ni 588 (54%) na wanaume 493(46%) (Kiambatisho ”G”). Aidha, Wizara imeendelea kujenga mazingira mazuri ya kuwawezesha watumishi wake wa kike na wa kiume kuweka uwiano muafaka wa kutekeleza kazi zao na vilevile kumudu majukumu ya uzazi na ulezi.

57.       Mheshimiwa Spika, kuhusu masuala ya UKIMWI, watumishi wa Wizara walipata mafunzo ya jinsi ya kujikinga na maambukizi ya virusi vya UKIMWI kupitia Kamati za UKIMWI zilizopo katika Wizara na taasisi zake. Wizara inawahudumia watumishi wanaoishi na virusi vya UKIMWI kwa matibabu na lishe.

58.       Mheshimiwa Spika, kuhusu masuala ya maadili, mafunzo yametolewa kwa watumishi 100 wa kada mbalimbali kutoka Kurugenzi ya Mashtaka kwa nia ya kutoa uelewa wa masuala ya rushwa,  kujenga maadili na uhusiano wenye staha kazini.

MAPATO NA MATUMIZI YA FEDHA KWA MWAKA 2013/14

Ukusanyaji wa Maduhuli ya Serikali

59.       Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/2014, Wizara yangu ilipanga kukusanya jumla ya Shilingi 5,250,454,700 kama maduhuli ya Serikali kutoka vyanzo mbalimbali vya mapato. Hadi kufikia mwezi Machi 2014 Wizara ilikusanya jumla ya Shilingi 6,007,714,285, sawa na  asilimia 114 ya lengo. Tofauti hii inatokana na ongezeko la makusanyo ya ada za wanafunzi wa Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo na maduhuli ya Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA).
            
Mapato na Matumizi ya Fedha 2013/2014

60.       Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/2014 Wizara iliidhinishiwa jumla ya Shilingi 260,656,733,000 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na miradi ya maendeleo. Kati ya fedha hizo Shilingi 205,397,547,000 ni matumizi ya kawaida na Shilingi 55,259,186,000 ni fedha za miradi ya maendeleo. Kati ya fedha za matumizi ya kawaida, Shilingi 42,537,099,000 ni kwa ajili ya mishahara na Shilingi 162,860,448,000 ni kwa ajili ya matumizi mengineyo. Kati ya fedha za matumizi ya maendeleo Shilingi 44,000,000,000 ni fedha za ndani na Shilingi 11,259,186,000 ni fedha za nje.

61.    Mheshimiwa Spika, kufikia Machi 2014, Wizara imepokea kiasi cha Shilingi 120,363,046,912 sawa na asilimia 46 ya fedha zilizoidhinishwa. Kati ya fedha hizo Shilingi 110,763,667,097 ni fedha za matumizi ya kawaida, sawa na asilimia 54. Kati ya fedha hizi za matumizi ya kawaida, shilingi 36,312,510,030 ni mishahara ya watumishi; na Shilingi 74,451,157,067 ni kwa ajili ya matumizi mengineyo. Fedha za maendeleo zilizopokelewa ni Shilingi 9,599,379,815, sawa na asilimia 17 ya fedha zote za Maendeleo. Kati ya fedha hizo, Shilingi 5,157,500,000 ni fedha za ndani na Shilingi 4,441,879,815 ni fedha za nje. Ufafanuzi wa taarifa hizi unapatikana katika (Kiambatisho ”D”).


D.       CHANGAMOTO ZILIZOPO

62.       Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio ambayo Wizara yangu imeyapata, zipo changamoto mbalimbali zilizojitokeza wakati wa kutekeleza majukumu yake. Changamoto hizi  ni pamoja na:
·        Bajeti ndogo inayotengwa ikilinganishwa na mahitaji halisi ya Wizara na taasisi zake;
·        Mapokezi ya fedha kidogo zilizoidhinishwa hayatabiriki na hivyo kuifanya Wizara na taasisi zake kushindwa kutekeleza Mipango Kazi yao kwa namna endelevu;
·        Wizara kutotengewa fedha za maendeleo za ndani kwa ajili ya ujenzi wa ofisi na makaazi. Hali hii inazilazimu baadhi ya taasisi za Wizara kutumia pesa nyingi kwa ajili ya kulipia  kodi ya pango, na hivyo kuathiri utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki na mazingira ya kazi;
·        Wanafunzi wa Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo kutopatiwa mikopo kutoka Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu kunachangia kuwepo kwa malalamiko ya mara kwa mara kutoka kwa wanafunzi na kuathiri utulivu masomoni;
·        Uhaba wa vitendea kazi na rasilimali watu;
·        Ongezeko la matukio ya makosa ya jinai pamoja na mbinu mpya za kutenda uhalifu;
·        Kuwepo kwa mazingira yanayoweza kuhatarisha usalama wa majaji, mahakimu na mawakili wa Serikali na hivyo kuathiri utendaji kazi wao; na
·        Kuongezeka kwa mmonyoko wa maadili miongoni mwa  baadhi ya watendaji wanaoshughulika na utoaji haki katika sekta ya sheria.

E.       MPANGO NA BAJETI YA WIZARA KWA MWAKA 2014/2015

63.       Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2014/2015, Wizara yangu imepanga kuimarisha utekelezaji wa malengo mkakati iliyojiwekea ili kutoa haki kwa watu wote na kwa wakati. Ili kufikia azma hiyo, Wizara itasimamia na kufuatilia utekelezaji wa majukumu yake katika maeneo ya kipaumbele yafuatayo:
                              i.            Utekelezaji wa Katiba ya nchi na Sheria
a)     Kufuatilia mchakato wa kutunga Katiba;
b)    Kufanya  maandalizi ya mapitio na marekebisho ya sheria zitakazoguswa na mabadiliko ya Katiba;
c)     Kutoa elimu ya Katiba kwa wananchi kuhusu taratibu za kimahakama zinazopaswa kuzingatiwa katika kudai haki;
d)    Kushughulikia maswala ya urekebu wa Sheria;
e)     Kushughulikia uandishi wa Miswada ya Sheria, Sera na Hati za Serikali;
f)       Kuhakiki  rasimu za mikataba ya Serikali na kushiriki katika majadiliano yanayohusu mikataba hiyo.

                                       ii.            Kusimamia na kufuatilia utoaji haki
a)     Kusimamia shughuli za uendeshaji na usikilizaji wa mashauri;
b)    Kuziimarisha Kamati za Maadili za Mahakama katika ngazi ya mikoa  na wilaya kwa kuzipa mafunzo na kuzifanyia ukaguzi. Kazi hii itaanzia katika mikoa ya Dodoma,  Katavi,  Mara, Mwanza, Rukwa, Shinyanga, Singida, Tabora;
c)     Kuimarisha utekelezaji wa mpango wa kutenganisha shughuli za upelelezi na mashtaka.

                                    iii.            Kulinda na kuhifadhi haki za binadamu na utawala wa sheria
a)     Kuhakikisha haki za binadamu zinalindwa na kuendelezwa;
b)    Kuwasilisha Bungeni miswada mbalimbali inayohusu upatikanaji wa msaada wa kisheria; kulinda mashahidi na waathirika wa vitendo vya jinai (witness and victims of crime protection law); kulinda watu wanaotoa taarifa kwa siri (whistle blowers) kuhusu vitendo vya uhalifu au vya ukiukwaji wa maadili; marekebisho ya sheria ya usajili wa vizazi na vifo; sheria ya ufilisi;
c)     Kueneza mfumo wa usajili wa watoto walio na umri wa chini ya miaka mitano katika mikoa ya Simiyu na Shinyanga;
d)    Kuimarisha usimamizi na uendeshaji wa taasisi za mafunzo za Wizara.

                                     iv.            Kuimarisha miundombinu ya utoaji haki
a)     Kujenga  nyumba za majaji, majengo ya Mahakama na  majengo ya Ofisi;
b)    Kuimarisha huduma za masjala;
c)     Kufunga mfumo wa kielektroniki wa e-justice kwa ajili ya usikilizaji wa mashauri;
d)    Kuimarisha usimamizi na uendeshaji wa Taasisi za mafunzo za Wizara.

                                        v.            Kuboresha mazingira ya uwekezaji na biashara nchini  kupitia Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa
a)     Kupunguza mlundikano wa mashauri katika Mahakama zote;
b)    Kuharakisha ufunguaji na uendeshaji wa mashauri;
c)     Kufanya mapitio na utafiti wa  sheria zinazohusu uwekezaji na biashara;
d)    Kuhakiki mikataba mapema na kwa weledi.

                                     vi.            Utekelezaji wa Masuala Mtambuka
a)     Kuimarisha Kamati za Amani za Mikoa kupitia Kamati ya Kitaifa ya kuzuia mauaji ya kimbari katika mikoa na wilaya. Vilevile, kutoa elimu na hamasa kwa Wabunge, Wanahabari na wanafunzi wa vyuo vikuu ili kujenga utamaduni wa amani na utangamano kwa kila Mtanzania;
b)     Kuandaa na kuratibu awamu ya pili ya shughuli za maboresho ya Sekta ya Sheria;
c)     Kuimarisha usimamizi wa maadili na uwajibikaji wa watumishi kazini.

64.       Mheshimiwa Spika, Pamoja na changamoto zilizopo, Wizara yangu imejizatiti kufanikisha malengo iliyojiwekea katika kutekeleza mpango na bajeti kwa kipindi cha mwaka 2014/2015.

F.         SHUKRANI

65.       Mheshimiwa Spika, naomba nitumie nafasi hii kuwashukuru sana wadau wetu wa maendeleo kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuboresha Sekta yetu ya Sheria. Kwa namna ya pekee napenda kushukuru nchi za Canada, Denmark, Sweden, Uswisi na Uingereza  kupitia Mashirika yao ya Maendeleo yaCIDA, DANIDA, SIDA na DFID. Vilevile, nayashukuru Mashirika na Taasisisi za Kimataifa zifuatazo:  Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF), Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo (UNDP) na Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki (EADB) katika kuchangia maendeleo ya Sekta ya Sheria.

66.       Mheshimiwa Spika, napenda kutoa shukrani za pekee kwa wadau mbalimbali wa Sekta ya Sheria kwa ushirikiano na ushauri wao uliowezesha kutekelezwa kwa majukumu ya Wizara kwa mwaka 2013/2014 kama yalivyobainishwa katika hotuba hii. Ninapenda kumshukuru Mheshimiwa Angellah Jasmine Kairuki (Mb), Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mheshimiwa Mohamed Chande Othman, Jaji Mkuu, Mheshimiwa Jaji Frederick Mwita Werema, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mheshimiwa Fakih A.R Jundu, Jaji Kiongozi, Ndugu Fanuel E. Mbonde, Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Ndugu Hussein Kattanga, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, na Ndugu George Masaju, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

67.       Mheshimiwa Spika, naomba niwashukuru Mheshimiwa Ignas Paul Kitusi, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. Eliezer M. Feleshi, Mkurugenzi wa Mashtaka, Bi. Winifrida Korosso, Katibu Mtendaji wa Tume ya Kurekebisha Sheria, Bibi. Mary Massay, Katibu Mtendaji Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Mheshimiwa Jaji Dkt. Gerald Ndika, Mkuu wa Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo, Mheshimiwa Jaji Ferdinand Wambali, Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama, Ndugu Phillip Saliboko, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa RITA, Bibi Enzel William Mtei, Katibu Msaidizi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Wakurugenzi wa Idara na Taasisi zilizo chini ya Wizara yangu na Watumishi wote kwa ushirikiano na kazi kubwa waliyoifanya katika kuandaa Mpango na Bajeti hii. Mwisho nitoe shukurani kwa Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali kwa kufanikisha uchapishaji wa hotuba hii.

G.         MAJUMUISHO

68.       Mheshimiwa Spika,  Sekta ya Sheria ina umuhimu wa pekee katika kuchangia maendeleo ya nchi kiuchumi, kisiasa na kijamii. Wizara yangu ina wajibu mkubwa wa kuhakikisha kuwa inakuza na kuimarisha amani, utawala wa sheria na haki za raia. Kwa kuzingatia dhana hii, napenda kutoa mwito kwa wananchi wote pamoja na Waheshimiwa Wabunge kuhakikisha kuwa dhamira ya Serikali ya kulinda amani, utulivu na haki za binadamu inazingatiwa na kupewa kipaumbele kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

H.          MAOMBI YA FEDHA KWA MWAKA 2014/2015

69.       Mheshimiwa Spika, ili kufanikisha utekelezaji wa majukumu yaliyopangwa katika mwaka wa fedha 2014/2015, Wizara yangu inaomba kuidhinishiwa kiasi cha Shilingi  231,372,948,000 kwa ajili ya Taasisi, Idara na vitengo vyake. Kati ya fedha hizo, Shilingi 134,006,144,000 ni kwa ajili ya Matumizi Mengineyo na Shilingi 48,804,234,000 ni Mishahara.  Fedha za  Maendeleo ni Shilingi 48,562,570,000, kati ya hizo Shilingi 44,000,000,000 ni fedha za ndani na Shilingi 4,562,570,000 ni fedha za nje.

Fedha za Matumizi

70.        Mheshimiwa Spika, mchanganuo wa matumizi ya bajeti kwa Mafungu saba ya Wizara ni kama ifuatavyo:-

Fungu 12: Tume ya Utumishi wa Mahakama
Matumizi ya Mishahara    Sh.      208,764,000
Matumizi Mengineyo       Sh.    2,871,716,000
Matumizi ya Maendeleo
(ndani)   -                           Sh.                       0.0
Matumizi ya Maendeleo (nje)  Sh.                0.0
                             Jumla Sh.        3,080,480,000

Fungu 16: Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali
Matumizi ya Mishahara Sh.    2,426,898,000
Matumizi Mengineyo     Sh.    8,332,865,000
Matumizi ya Maendeleo 
(Ndani)                              Sh.                      0.0
Matumizi ya Maendeleo
(nje)                                    Sh.      457,149,000    
                          Jumla Sh.  11,216,912,000

Fungu 35: Kurugenzi ya Mashtaka
Matumizi ya Mishahara- Sh.   5,215,201,000
Matumizi  Mengineyo     Sh. 16,460,826,000 
Matumizi ya Maendeleo
(ndani)                             Sh.                    0.0
Matumizi ya Maendeleo
(nje)                                   Sh.    468,299,000                            Jumla  Sh.  22,144,326,000
                                                                                                                                          
Fungu 40: Mfuko wa Mahakama
Matumizi ya Mishahara  Sh. 35,040,061,000
Matumizi Mengineyo       Sh.  89,660,284,000
Matumizi ya Maendeleo
(ndani)                               Sh.  40,000,000,000
Matumizi ya Maendeleo
(nje)                                   Sh.    1,687,748,000
                   Jumla Sh. 166,388,093,000



Fungu 41: Wizara ya Katiba na Sheria
Matumizi ya Mishahara      Sh.   3,154,642,000
Matumizi  Mengineyo         Sh.   8,028,651,000
Matumizi ya Maendeleo
(ndani)    -                           Sh.    4,000,000,000
Matumizi ya   Maendeleo
(nje)                   -                  Sh.    1,048,621,000
               Jumla -     Sh. 16,231,914,000


Fungu 55:Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora
Matumizi ya Mishahara      Sh.    2,041,593,000
Matumizi  Mengineyo         Sh.    4,795,802,000
Matumizi ya Maendeleo
(ndani)              -                  Sh.                       0.0
Matumizi ya Maendeleo
(nje)                   -                  Sh.       900,753,000    
          Jumla -        Sh.   7,738,148,000

Fungu 59: Tume ya Kurekebisha Sheria
Matumizi ya Mishahara      Sh.       717,075,000
Matumizi  Mengineyo         Sh.    3,856,000,000
Matumizi ya Maendeleo
(ndani)    -                           Sh.                       0.0
Matumizi ya Maendeleo
(nje)         -                           Sh.                       0.0    
Jumla  - Sh.    4,573,075,000


Makusanyo ya Maduhuli ya Serikali

71.       Mheshimwa Spika, kwa mwaka 2014/2015 Wizara yangu inatarajia kukusanya kiasi cha Shilingi 8,577,362,121 kama maduhuli ya Serikali, kama ifuatavyo:-

Fungu 12: Tume ya Utumishi    wa Mahakama
Sh.
0.0
Fungu 16: Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali
Sh.
4,502,000
Fungu35: Kurugenzi ya Mashitaka
Sh.
17,103,000
Fungu 40: Mfuko wa Mahakama
Sh.
4,115,843,000
Fungu 41: Wizara ya Katiba na Sheria
Sh.
4,434,270,121
Fungu 55: Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora
Sh.
5,644,000
Fungu 59:Tume ya Kurekebisha Sheria
    Sh.
0.0
JUMLA
Sh.
8,577,362,121


72.                Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.


No comments:

Post a Comment