Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Monday 9 May 2016

ALIYOSEMA ZITTO KABWE KUHUSU BAJETI YA WIZARA YA VIWANDA NA BIASHARA 2016/17


Mheshimiwa Spika, Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji amewasilisha maombi ya Fedha ili Bunge lako Tukufu limuidhinishie Jumla ya Tshs 82 Bilioni (Tshs 42 Bilioni za Matumizi ya Kawaida na Tshs 40 Bilioni za Maendeleo). Waziri anaomba tumpe idhini kutumia Fedha hizi ili aanze kutekeleza Mpango wa Pili wa Miaka Mitano ambao lengo lake kubwa ni kuwezesha Tanzania ya Viwanda. Bajeti ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji ni sawa na 0.3% ya Bajeti nzima ya Serikali ya mwaka 2016/17.
Mheshimiwa Spika, Waziri Kivuli wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji ameibua hoja nzito sana kwenye hotuba yake ambazo naamini Serikali hainabudi kuzipatia majibu yanayostahili. Hoja kubwa ni ile inayohusu kuwepo kwa matamko 3 tofauti, yenye tarakimu tofauti kutoka Serikali moja. Mfano uliotolewa ni kufufua Kiwanda cha General Tyre ambapo Vitabu vya Bajeti vinaonyesha kutengwa tshs 150 milioni, randama za Wizara zinaonyesha tshs 500 milioni na mpango wa Maendeleo unaonyesha tshs 2 bilioni zimetengwa. Kisheria za Bajeti, kilichomo kwenye vitabu vya Bajeti ndio kitakachoidhinishwa na Bunge. Kwamba Serikali inataka kufufua Kiwanda cha General Tyre kwa kutenga tshs 150 milioni, ni kichekesho cha karne. Mambo haya yanadhihirisha kuwa Serikali hii haitembei kwenye maneno yake. Wananchi wapatiwe majibu ya uhakika kuhusu masuala haya. Ni muhimu sana Serikali kuhakikisha kuna uratibu miongoni mwa Wizara za Serikali ili kuwa na sauti moja inayokwenda kwa wananchi.

Kufungamanisha Sekta ya Viwanda na Sekta ya Kilimo
Mheshimiwa Spika, adhma ya nchi yetu kuwa ya Viwanda ni adhma yetu sote. Jambo hili ni jambo la Maendeleo na halina ushabiki wa kivyama. Tumepitisha Mpango wa Maendeleo katika Bunge hili na kwa hiyo ni Mpango wa Nchi sio mpango wa vyama tena. Hivyo sote kwa pamoja tunafanya kazi ya kuhakikisha tunafikia malengo. Sisi tulio kwenye upinzani jicho letu pamoja na kushauri na kupendekeza ni kukosoa pale ambapo walio kwenye Serikali wanakosea. Kukosoa ni tendo la kizalendo na walio Serikalini wawe tayari kukubali kukosolewa ili kuboresha zaidi. Kwa maoni yangu, kama tusipofanya marekebisho ya kimkakati mapinduzi ya Viwanda itakuwa ni nyimbo na ngonjera za kisiasa. Watakaoumia ni Wananchi ambao hawatapata ajira na Serikali yenyewe itakosa kodi kuweza kutoa huduma kwa wananchi. Kama nilivyosema hapo awali Serikali inahitaji kufanya uratibu ili kufikia malengo. Sekta ya Viwanda au Maendeleo ya Viwanda yanapaswa kufungamanishwa na sekta nyengine za uchumi kwa sababu kuna kutegemeana. Kwa Tanzania unahitaji Sekta ya Kilimo inayokua kwa kasi ili kuzalisha malighafi kwenye viwanda. Sekta nyingine kama Elimu, Afya, Nishati, Mazingira nk zinahusiana na Viwanda pia. Kwa leo tutazame Sekta Kilimo na Viwanda kwa muktadha wa Hotuba ya Waziri wa Viwanda na kulinganisha na Hotuba ya Waziri wa Kilimo.
Mheshimiwa Spika, Sekta ya Viwanda na Sekta ya Kilimo kwa pamoja zinachangia nusu ya Pato la Taifa ( GDP) na nusu nyingine ni sekta ya Huduma. Nadharia za Uchumi zinatuambia kuwa Tija ikiongezeka kwenye ya Kilimo inawezesha sekta ya Viwanda kukua na kisha sekta ya Huduma. Hapa Tanzania na nchi nyengine nyingi za Afrika, sekta ya huduma iliruka hatua hizi na hivyo kuchangia kwa kiasi kikubwa sana kwenye Pato la Taifa. Ndio maana tuna Kitendawili nchini kwetu kuwa Uchumi unakua lakini umasikini haupungui; ni kwa sababu sekta ya huduma haijiri watu wengi kama sekta ya Kilimo na hivyo uchumi unaokuzwa na sekta ya huduma ni nadra kuondoa umasikini. Tanzania bado inapambana na umasikini. Juhudi zote tunazofanya lengo lake ni kuondoa umasikini kwa watu wetu. Sekta za kuondoa umasikini ni Kilimo na Viwanda hivyo lazima mikakati ya Serikali iendane na kufungamanisha haya. Ndio Maana Nchi nyengine Wizara ya Kilimo hujumuisha uongezaji thamani ( Ministry of Agriculture and Agro-processing ). Hatuhitaji kufanya hivyo, tunachohitaji ni kufungamanisha. Hata hivyo Serikali imeshindwa kufanya hivyo katika mwaka wake wa kwanza tu wa Bajeti. Nitaeleza kwa kutumia changamoto tuliyonayo kuhusu Sukari, Mafuta ya Kula na Nguo.
Mheshimiwa Spika, Malengo ya Serikali kwenye Viwanda yapo uk.140 ibara ya 191 ya Hotuba ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji. Serikali imepanga kutekeleza mambo 9 na katika mambo yote hayo hakuna hata moja linalohusiana na Viwanda vya kuzalisha bidhaa zinazohudumiwa na wananchi wengi zaidi kama Sukari na Mafuta ya kula. Bidhaa hizi ni bidhaa zinazoleta maneno ya kisiasa ndani ya nje ya Bunge. Nadhani baada ya madawa ya kulevya, bidhaa zenye mizengwe mingi zaidi katika duru za kisiasa ni Sukari na Mafuta ya kula. Sukari na Mafuta ya kula imeangusha Mawaziri kadhaa hapa nchini katika kipindi cha miaka 20 iliyopita. Hata hivyo Wizara ya Viwanda na Biashara haina mkakati kabisa kushughulika na Bidhaa hizi licha ya uwezo wake wa kutenegenza ajira na kuokoa fedha za kigeni kuziagiza. Wizara imezungumza kuhusu viwanda vya nguo lakini haijafafanua changamoto kubwa zinazoikabili sekta ya nguo nchini na hasusan biashara haramu ya magendo ya Nguo inayoathiri sana ukuaji wa sekta ya nguo nchini.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, ukitazama hotuba ya Waziri wa Kilimo ambayo Bunge lako tukufu limeshapitisha bajeti yake kuna ‘mikakati’ ya kulima Miwa kwa ajili ya Sukari. Ukurasa wa 44 ibara ya 107 ya Hotuba ya Wizara ya Kilimo na ukurasa wa 25 ibara za 63 na 64 zinaeleza ‘mikakati’ ya kukabiliana na uhaba wa Sukari nchini. Kiambatanisho namba 6 cha Hotuba hiyo kimeeleza kwa kina changamoto nzima ya Sukari na miradi inayopaswa kutekelezwa ili kumaliza kabisa suala la uhaba wa Sukari nchini. Nimejumlisha miradi ile kutoka kona mbalimbali za nchi na nimekuta ni takribani Hekta 300,000 za kulima Miwa. Kwa Hesabu ya chini ya wastani wa kuzalisha Sukari kwa kila Hekta, miradi hii ikitekelezwa Tanzania itaweza kuzalisha Tani 1.5 milioni za Sukari. Ukiondoa Sukari tunayotumia nchini, ziada itakayouzwa nje inaweza kuliingizia Taifa Fedha za Kigeni USD 500 milioni, sawa na 30% ya malengo ya Mpango wa Maendeleo kwa sekta ya Viwanda katika mapato ya Fedha za kigeni ya USD 3bn. Hapo sijaeleza kiwango cha Ajira kitakachopatikana, ukuaji wa biashara kwenye sekta nyengine na Umeme utakaozalishwa ( Multiplier effect ).
Mheshimiwa Spika, swali la kujiuliza, chukulia Wizara ya Kilimo inalima hiyo miwa hekta 300,000 halafu Wizara ya Viwanda haina mpango wa hivyo viwanda, hii miwa itakwenda wapi? Sio kwamba inapaswa kufungaminisha Kilimo cha Miwa na Viwanda vya Sukari? Ni kwa nini Wizara 2 zilizo chini ya Serikali moja zinashindwa kusomana? Baraza la Mawaziri linajadili nini? Ndio maana Rais anajikuta akitoa matamshi ya Mawaziri barabarani. Suala la Rais kutoa matamko kuhusu Sukari sio sawa, hii ni Kazi ya Mawaziri maana mnamuexpose Rais. Rais sio mtu wa kuhangaika na masuala ya kunywa Chai na Uji.
Mheshimiwa Spika, nashauri Bunge lako tukufu leo lisipitishe Bajeti ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji ili Wizara hii ikakae na Wizara ya Kilimo wawianishe mipango hii na kisha walete hapa Bungeni ndio tupitishe. Sukari ni mfano mmoja tu katika suala hili. Hebu tumuunge mkono Rais kwa kuwarejesha mezani Wizara hizi mbili.
Mheshimiwa Spika, kwenye sukari kuna suala la ‘low hanging fruits’. Hivi tunavyozungumza kila Mwaka miwa yenye uwezo wa kuzalisha tani 50,000 ya Sukari huoza hapa nchini uko Kilombero na Mtibwa. Wakulima wanalima miwa mingi kuliko uwezo wa Viwanda kununua. Bodi ya Sukari inapaswa kutoa leseni ili vikundi vya wakulima au wawekezaji wadogo wazalishe Sukari. Bodi ya Sukari haijatoa leseni na wala Serikali haijahamasisha Watanzania kuwekeza kwenye viwanda vidogo vya Sukari ili kuwezesha miwa yote inayozalishwa kutoa Sukari. Kama hili lingefanyika, leo tusingekuwa na ukali huu wa uhaba wa Sukari. Waziri wa Viwanda, hii ni ‘low hanging fruits’.
Mheshimiwa Spika, uwekezaji wa bidhaa kama Sukari unahitaji vivutio maalumu kutoka Serikalini. Kule Uganda, Rais Museveni tangu aingie madarakani aliweka vivutio maalumu kwa Viwanda kama Kakira Sugar ili wazalishe Sukari ya kutosha. Viwanda vya Sukari Uganda hata umeme hulipiwa na Serikali kwa Asilimia 50 ili kupunguza gharama za uzalishaji na kuokoa kutokana na ushindani wa Sukari kutoka nje inayotupwa nchini ( dumping). Subsidies kwa ajili ya kupunguza gharama za uzalishaji ili kuwezesha kuzalisha Sukari, kutengeneza ajira na kupata faida nyengine ni jambo ambalo Lazima Serikali ianze kulifikiria. Sisi Kigoma kuna mtu anataka kuzalisha Sukari tani milioni 1 kwa mwaka. Wizara ya Fedha na Wizara ya Viwanda wanabishana kuhusu vivutio. Rais anahangaika na kuwafanya Watanzania wanywe Chai na Uji kwa bei rahisi, Mawaziri wake wanabishana kuhusu vivutio vya mitambo ya kupanda miwa nakuzalisha Sukari na kuzalisha Umeme. Serikali, hebu mtawale. Hebu muongoze. Utawala sio kutoa matamshi ya barabarani. Uongozi ni kufanya maamuzi yanayomaliza shida za wananchi kwa muda mrefu zaidi na sio matamko ya kupata Kurasa za Mbele za magazeti ya siku moja au mbili.
Mheshimiwa Spika, suala la Mafuta ya Kula halina tofauti na suala la Sukari. Ukipanda gari ukapita njia ya Singida unaona wananchi wamepanga madumu ya mafuta ya Alizeti wanauza. Nguvu kazi hii ya Wananchi inapotea kwa sababu Serikali imetoa unafuu mkubwa wa kodi kwa wanaoagiza mafuta ya kula kutoka nje ya Nchi. Leo kodi kwenye mafuta ya kula kutoka nje ni 18% tu. Tukiendelea hivi tutaendelea kuwaona wananchi wetu wanapigwa na jua kuuza mafuta ya Alizeti. Tunaposema mapinduzi ya Viwanda tunataka kumsaidia nani kama sio huyu Mwananchi anayeshinda juani? Kama tunataka kubadilisha hali ya Wananchi ni lazima tuwawekee mazingira mazuri. Ni Aibu kubwa nchi hii kuagiza mafuta ya kula kutoka nje ya nchi. Tunatumia USD 340 milioni kila mwaka kuagiza mafuta ya kula kutoka nje. Leo hii bei ya lita ya mafuta ya Alizeti ni kubwa kuliko bei ya lita ya petroli kwenye soko la dunia. Lakini wazalishaji wetu, wananchi wetu masikini tunawatazama tu tukipita na mashangingi yetu barabarani. Hali hii lazima ibadilike. Serikali ndio yenye wajibu wa kubadili hali hii kwa kuweka kodi kubwa zaidi dhidi ya Mafuta ya kula kutoka nje na kuwekeza kwenye viwanda vya kukamua Mafuta kwa kutumia Alizeti na Mawese.
Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kigoma kuna Mradi tunaotaka kuanza wa kupanda Michikichi ili kuzalisha Mafuta ya Mawese. Tuna mpango wa kila familia 1 kupanda hekta 1 ya michikichi kwa lengo la kufikia familia 100,000. Uzalishaji huu wa Mawese unaweza kuondoa kabisa suala la Tanzania kuagiza mawese kutoka nje maana tutaweza kuzalisha Tani 200,000 za Crude Palm Oil (CPO) kwa mwaka, kuzalisha ajira nyingi, kupandisha hali ya maisha ya wananchi wakulima na kukuza biashara nyengine. Tunahitaji watu watakaowekeza kwenye Viwanda vya kuzalisha mawese. Wizara ya Viwanda ishirikiane na Uongozi wa Mkoa wa Kigoma kuhakikisha tunazalisha mafuta ya Kula ya kutosha ili kuondokana na uagizaji huu. Mawese na Alizeti ndio suluhisho la kudumu la suala la Mafuta ya kula. Bunge liitake Serikali ikae upya kuandaa Bajeti ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji ili kuifungamanisha na Bajeti ya Wizara ya Kilimo.
Mheshimiwa Spika, Suala la Mwisho ni sekta ya Nguo. Nchi nyingi duniani ambazo zimefanikiwa kuondokana na umasikini zimetumia sekta ya nguo ( textile industry). Mnyororo wa thamani wa Sekta ya Nguo ni mrefu kuanzia kwa Mkulima mpaka kwenye nguo tunazovaa. Hii inapaswa kuwa sekta ongozi kwenye suala zima la uchumi wa viwanda. Hata hivyo tuna tatizo la Pamba.
Mheshimiwa Spika, uzalishaji wa Pamba umeporomoka kwa asilimia 47. Tutapata wapi Pamba ya kulisha viwanda vya nguo? Wizara ya Kilimo na Wizaara ya Viwanda lazima zikae pamoja ili kuhakikisha kuwa tunafufua zao la Pamba. Vinginevyo nchi hii itaishia kuagiza pamba kutoka nje au tutajikuta tunaunganisha nguo za kutoka China tu.
Mheshimiwa Spika, Viwanda vya Nguo nchini vinapata shida kubwa sana kutokana na magendo ya nguo. Kuna ukwepaji mkubwa sana wa kodi kwenye bidhaa za nguo zinazoingizwa hapa nchini na hivyo kuua viwanda vya ndani. Viwanda vinapata shida kubwa ya matumizi ya Umeme maana umeme hauna uhakika na ni bei kubwa. Matokeo yake viwanda vingi vinafungwa na watu wetu kukosa ajira. Serikali lazima ifanye kazi ya ziada ya kuzuia magendo ya nguo vinginevyo viwanda vilivyopo vitakufa na hakuna atakayekubali kujenga kiwanda hapa nchini kwani atajua kuwa Serikali haifanyi ziada kuhakikisha tunalinda viwanda.
Mheshimiwa Spika, hakuna nchi duniani isiyolinda viwanda vyake. Leo Taifa kubwa kama Uingereza linahangaika na kiwanda cha Chuma na kutaka hata kuingiza mtaji wake ili kulinda ajira za Wanananchi wake. Tujifunze kwa wenzetu. Kama tunataka kupata ajira kwa watu wetu ni lazima kulinda viwanda vyetu. Viwanda vya nguo nchini vipo kwenye tishio kubwa sana kutokana na magendo ya nguo. Serikali ichukue hatua stahiki. Nguo "zitatutoa" kuanzia kwa mkulima mpaka kwa wenye viwanda.
Mheshimiwa Spika, Naomba kutoa hoja kwamba Tuahirishe mjadala wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji ili kuiruhusu Serikali kuwianisha mipango ya Wizara ya Kilimo na Wizara ya Viwanda. Wakiwa tayari ndio Bunge lije kupitisha Bajeti ya Wizara hiyo.

Zitto Zubeir Ruyagwa Kabwe
Mbunge Kigoma Mjini (ACT Wazalendo)
Mei 9, 2016



No comments:

Post a Comment