Pages

Pages

Pages

Saturday 14 March 2015

KAULI ZA VIONGOZI ZATIKISA NA KUWAKERA WANANCHI


  1. Juma Nkamia: Mwaka 2013: “Sugu naomba ukae kimya, halafu uelewe mimi siongei na mbwa, naongea na mwenye mbwa.”
  2. John Magufuli: Mwaka 2012: “Asiyetaka kulipa nauli hiyo, apige mbizi baharini na kama hawezi azunguke Kongowe kuingia katikati ya jiji au arudi kijijini akalime”.
Dar es Salaam. Kauli kama “kutumia Sh10 milioni kununulia mboga” na ile maarufu ya “vijisenti”, zimetikisa nchi katika siku za karibuni na kuibua hisia tofauti, lakini waliotoa kauli hizo ni sehemu tu ya orodha ndefu ya viongozi wa umma waliowahi kutoa maneno yaliyoibua maoni tofauti.
Kauli ya Profesa Anna Tibaijuka, aliyekuwa Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, ndiyo iliyokuwa gumzo katika siku za karibuni baada ya mbunge huyo wa Muleba Kusini kusema alitumia Sh10 milioni kununulia mboga wakati alipokuwa akihojiwa na Baraza la Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kuhusu Sh1.6 bilioni alizopewa na ambazo zinahusishwa na kashfa ya uchotwaji wa Sh306 bilioni kwenye Akaunti ya Tegeta Escrow.
Akilieleza baraza hilo jinsi alivyotumia baadhi ya fedha zilizoingizwa kwenye akaunti yake, Tibaijuka alisema: “Hivyo nilipolipwa (Shilingi) milioni 117, nilitoa milioni mbili nikachangia Kanisa la Makongo na nikatoa 400,000 nikapeleka kanisani na milioni 10 niliitoa kwa ajili ya matumizi yangu ya kununulia mboga.”
Kauli hiyo iliamsha mjadala mkubwa uliokumbusha kauli nyingine nyingi zilizotolewa na viongozi wa umma kwa nia njema au kujitetea wakati walipokabiliwa na matatizo au kutetea misimamo yao au ya Serikali.
Mkurugenzi wa utetezi, maboresho na sheria wa Kituo cha Haki za Binadamu na Sheria, Harlord Sungusia anaelezea kauli hizo kuwa zinatokana na Katiba kuwalinda viongozi.
“Katiba iliyopo kwa sasa inatoa jeuri kwa viongozi kutoa kauli zozote kutokana na ulinzi waliowekewa. Katiba imewawekea kinga kwa hivyo kwanza, inawapa kiburi cha kuona wako juu ya sheria,” alisema Sungusia.
Sungusia pia alisema kauli hizo zinaweza kuwa zinasababishwa na mtu kutoelewa nafasi yake kwenye jamii.
“Ujinga ni ugonjwa unaotesa nchi nyingi za Kiafrika, yaani kiongozi anaingia kwenye kashfa ya ufisadi, lakini akifika jimboni kwake anatawazwa (kuwa chifu) na wanakijiji, athari zake ni mmomonyoko wa utawala wa sheria na hata kuyumba kwa nchi kama ilivyokuwa Somalia,”  alisema.
Katika sakata la escrow, fedha zilizochotwa kwenye akaunti hiyo zilihusishwa na miamala ya mamilioni ya fedha zilizoingia kwenye akaunti za mawaziri na wabunge waliowahi kushika nafasi nyeti serikalini, maofisa waandamizi serikalini, majaji na viongozi wa kidini ambao walipewa kati ya Sh40.4 milioni na Sh1.6 bilioni.
Mmoja kati ya watu waliopokea Sh80.8 milioni ni msimamizi wa makazi ya Rais, Shabani Gurumo, ambaye alielezea kiasi hicho cha fedha kuwa ni kidogo kwa kuwa anazo fedha nyingi zaidi ya hizo, wakati Mwanasheria Mkuu wa Serikali wa zamani, Andrew Chenge alielezea Sh1.6 bilioni zilizohusishwa na ununuzi wa kifisani wa rada, kuwa ni “vijisenti”.
Alitoa kauli hiyo alipoulizwa na waandishi wa habari kuhusu kuhusishwa kwake na kashfa ya ununuzi wa rada kwa bei ya juu wakati kashfa hiyo ilipoibuliwa na Kitengo cha Uchunguzi wa Makosa Makubwa ya Jinai cha Serikali ya Uingereza.

“Wanasiasa wengine huathiriwa na mila na desturi za makabila yao na hivyo hushindwa kuchunga kauli zao,” alisema mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar esSalaam (UDSM), Richard Mbunda.
Alisema viongozi wanaotoka kwenye makabila yenye asili ya uchifu, wameingia madarakani na dhana ya kifalme hivyo wanaamini majibu yoyote ni sahihi bila kujali jamii iliyomzunguka,” anasema.
“Tibaijuka angezungumza kauli ile katika jamii ya Kihaya inafahamika kabila lile jinsi lilivyo, lakini tatizo ni pale anapojisahau na kuzungumza kwa jamii nyingine.”
Mwananchi imekusanya baadhi ya kauli zilizowahi kutolewa na viongozi mbalimbali Serikali kuanzia enzi za Serikali ya Awamu ya Kwanza hadi ya Nne.
John Malecela
Wakati tatizo la usafiri linaanza kuwa kubwa na wananchi wakilalamikia hali hiyo, John Malecela, ambaye wakati huo alikuwa Waziri wa Mawasiliano na Uchukuzi, aliulizwa na waandishi wa habari kuhusu matatizo makubwa ya usafiri wa treni na akajibu, “nani anasema Tanzania kuna shida ya usafiri… anayesema kuna shida ya usafiri “he can go te hell”, akiwa na maana “anaweza kwenda kuzimu”. Kauli hiyo aliyoitoa mwaka 1989 ilimsumbua sana kisiasa hadi aliposhindwa ubunge.
Basil Mramba
Wakati akitetea uamuzi wa Serikali ya Awamu ya Tatu kununua ndege ya rais kwa bei kubwa, Basil Mramba, ambaye alikuwa Waziri wa Fedha, alisema ndege hiyo itanunuliwa hata kama “wananchi watakula nyasi”.
Mramba alikwenda mbali kidogo, kwa kauli ya kejeli akasema “Rais hawezi kupanda punda”.
Mchungaji Peter Msigwa
Wakati Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa akichangia kwenye mjadala wa Bajeti ya Serikali, alisikitishwa na kile alichokiita kitendo cha wabunge kutotaka kutumia akili zao kutatua matatizo ya wananchi.
“Wananchi wametuamini tuje tujadili vitu vya maana hapa, lakini tunakubaliana akili ndogo itawale akili kubwa. James Madison mwaka 1822, alisema ‘knowledge forever will govern ignorance (ujuzi utatawala ujinga milele,” alisema Mchungaji Msigwa.
“Tumekubali kwenye Bunge hili knowledge ndogo (ujuzi mdogo) i-govern knowledge kubwa (utawale ujuzi mkubwa, tumekubali ignorance i-govern knowledge (ujinga utawale ujuzi),tunalipeleka wapi taifa?”
Andrew Chenge
Akihojiwa na wanahabari Aprili mwaka 2008, Mwanasheria Mkuu wa zamani wa Serikali, Andrew Chenge kuhusu tuhuma nzito za akaunti yake iliyokuwa kisiwa cha Jersey na ambayo ilikuwa na Dola 1 milioni za Marekani, alijibu kwamba fedha hizo kwa viwango vyake zilikuwa ni vijisenti akisema suala la kumiliki kiasi gani cha fedha si hoja ya kuzungumza kwani kila mtu ana kiwango vyake.
Wiki moja kabla ya kauli yake, gazeti moja la Uingereza, The Guardian liliandika kuwa katika uchunguzi uliofanywa na SFO, ilibaini kuwa Chenge, ambaye wakati wa ununuzi wa rada alikuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, alikuwa na fedha hizo kwenye akaunti hiyo iliyokuwa nje ya nchi. Rada hiyo ilinunuliwa kwa bei iliyokuzwa ya Sh70 bilioni kutoka Kampuni ya Bae Systems ya Uingereza.
Cleopa Msuya
Wakati nchi ikiwa kwenye hali ngumu kiuchumi, Cleopa Msuya, akiwa Waziri wa Fedha aliwasilisha bajeti ambayo ilionekana haimjali mwananchi na baada ya malalamiko, alijibu kwa kusema “kila mtu atabeba msalaba wake”, kauli iliyozua mjadala mkubwa.
Rais Jakaya Kikwete
Julai 18, mwaka 2010, Rais Jakaya Kikwete, ambaye pia ni mwenyekiti wa CCM, alitamba kuwa chama hicho kwa miaka mitano iliyopita kimeinua maisha ya Watanzania akifafanua kuwa foleni kubwa za magari jijini Dar es Salaam ni ishara ya wananchi kuwa na “maisha bora”.
Alitoa kauli hiyo wakati akizungumza katika mkutano ulioandaliwa na CCM Mkoa wa Dar es Salaam kwa ajili ya kumpongeza kuchaguliwa kuwa mgombea pekee wa urais kwa asilimia 99.16.
Mwaka huohuo, Rais Kikwete akihutubia wananchi wa kijiji cha Kisesa wilayani Magu katika ufunguzi wa mashindano ya ngoma kwa Kabila la Wasukuma, alisema matukio ya mimba kwa wanafunzi wa kike nchini yanasababishwa na viherehere vya wanafunzi wenyewe.
Pia, katika hotuba yake ya kuomba ridhaa kwa wananchi mwaka 2010, kati ya mambo aliyozungumzia ni hali ya ugonjwa wa Ukimwi, kwamba wapo wanaoupata kwa bahati mbaya, wanaoambukizwa kutokana na mazingira, lakini wengine wanaupata “kwa viherehere vyao”.
Pius Msekwa
Wakati akiongoza moja ya vikao vya mwisho kabla ya Bunge la Tisa kuanza shughuli zake, Pius Msekwa akiwa spika wa Bunge alilazimika kujibu hoja za wabunge za kumtaka aachie uenyekiti wa Bodi ya Vodacom ili kumfanya aeweze kufanya shughuli za chombo hicho cha uwakilishi wa wananchi bila ya kuwa na maslahi binafsi.
Katika kujibu hoja hizo, Msekwa aliwaelezea walioanzisha hoja hiyo kuwa wana “wivu wa kike”, kauli iliyowatia hasira wanaharakati wa haki za wanawake.
John Magufuli
Mwaka 2012 wakati akizungumza na wakazi wa Kigamboni kuhusu nauli mpya ya Sh200 ya kivuko, alisema “asiyetaka kulipa nauli hiyo, apige mbizi baharini na kama hawezi azunguke Kongowe kuingia katikati ya jiji au arudi kijijini akalime”.
Dk Didas Masaburi
Mwaka 2011 tuhuma za uuzwaji kifisadi wa Shirika la Usafiri Dar es Salaam (Uda) kwa Kampuni ya Simon Group liliibuka bungeni. Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Dk Didas Masaburi alituhumiwa kuhusika. Katika majibu ya tuhuma hizo, Dk Masaburi alisema kuwa wabunge waliokuwa wanazungumzia suala hilo ni wa aina tatu; waliodandia hoja bila ya kujua; wanaotafuta umaarufu na kundi la tatu ni la wabunge ambao wanaujua ukweli lakini wanaupotosha ili kuficha madhambi yao.
“Hawa wanashindwa kufikiri kwa kutumia akili zao, badala yake wanafikiria kwa kutumia makalio,” alisema Dk Masaburi.
Mizengo Pinda
Akijibu swali kuhusu vitendo vya askari wa Jeshi la Wananchi Tanzania kupiga raia, hasa kutokana na vurugu zilizotokea Mtwara, Waziri Mkuu Mizengo Pinda alisema watu wanapokaidi amri halali wanajitakia matatizo kwa vyombo vya dola, watapigwa tu.
“Sasa kama wewe umekaidi, hutaki unaona kwamba ni imara zaidi, wewe ndiyo jeuri zaidi watakupiga tu. Mimi nasema muwapige tu, kwa sababu hakuna namna nyingine, maana tumechoka,” alisema Waziri Pinda wakati wa kipindi cha maswali ya Papo kwa Papo kwa Waziri Mkuu kinachofanyika kila Alhamisi bungeni.
Juma Nkamia
Mwaka 2013, Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema alitoa madai kuwa kuna ukabila mkubwa kwenye Chuo Kikuu cha Dodoma mjini na kwamba ana ushahidi wa mikanda ya video, lakini mbunge wa Kondoa Kusini, Juma Nkamia akasimama na kukanusha habari hizo. Wakati akikanusha, Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi alisema “na ya Rwakatare je?” akimaanisha ile mikanda iliyotumika kumshtaki Mkurugenzi wa Usalama wa Chadema, Wilfred Rwakatare kuwa anahusika na vitendo vya ugaidi.
Kusikia hivyo, Mkamia alimtaka Mbilinyi atulie na akasema: “Sugu naomba ukae kimya, halafu uelewe mimi siongei na mbwa, naongea na mwenye mbwa.” Kauli hiyo ilisababisha mtafaruku bungeni hadi Nkamia alipoomba radhi.
Philipo Mulugo
Aliyekuwa Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo aliwahi kukaririwa akisema kuwa Tanzania imetokana na muungano wa visiwa vya Zimbabwe na Pemba vilivyoungana na Tanganyika.
Kauli hiyo aliitoa mwaka 2012 wakati akiwasilisha mada katika mkutano wa viongozi na wataalamu wa elimu katika Bara la Afrika uliofanyika nchini Afrika Kusini.
Imeandikwa na Fidelis Butahe na Kelvin Matandiko
CREDIT: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment