Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Monday, 16 June 2014

RIWAYA TAMU: JUDITH…JUDITH…! - 10


INNOCENT A. NDAYANSE (ZAGALLO)

0755 040 520 / 0653 593 546 


Simulizi zimemnogea Makella na sasa anaamua kunywa pombe. Anamlazimisha Judith naye anywe. Kwa woga na hofu, anaamua kunywa pombe kwa mara ya kwanza maishani mwake. Makella anasimulia mengi na kuwaponda wanawake wa Tanzania. Anajiuona yuko huru zaidi. Hatimaye anaamua kwenda kuoga. Je, nini kitaendelea hali Judith naye akiendelea kunywa pombe? Ungana na msimulizi wako…

NJE ya Kiyovu Hotel, Judith alitembea kwa mwendo uleule wa kawaida huku kwa macho ya wizi akiwatazama askari watatu wenye silaha waliokuwa wakiilinda hoteli hiyo. Askari hao hawakumjali wala kumshuku, zaidi walimtazama kwa namna nyingine kabisa, umbo lake lililotengeneza robota kubwa chini ya nyonga yake likiwa ni kivutio kikubwa machoni mwa askari hao kiasi cha kujikuta wakitikisa vichwa kwa matamanio na kutabasamu kisirisiri.
Judith aliwaona jinsi walivyomtazama. Akaijua sababu ya kufanya hivyo. Hakushangazwa na macho hayo, wanaume wengi walishamkodolea macho hususan kwenye makalio yake makubwa pale inapotokea akavaa nguo yoyote iliyomshika vilivyo maungoni. Hawa askari walikuwa kama hao wanaume wengine wengi waliokwishapita, hivyo hakuwajali. Akaendelea kutembea taratibu vilevile, kama mtu anayejiamini ilhali ni Mungu tu aliyejua hali aliyokuwa nayo moyoni mwake.
Muda mfupi baadaye alikuwa kando ya Barabara ya 17/18. Barabara hiyo ilikuwa maarufu, yenye kutumiwa na magari mengi, makubwa kwa madogo, kuingia na kutoka nchini Rwanda. Kwa dakika chache tu, kama mbili alizosimama kando ya barabara hiyo tayari magari mawili makubwa ya mizigo, yenye nambari za usajili za Tanzania yalipita.
Akilini mwake, Judith aliamini kuwa, kwa kutumia magari hayo ya mizigo atafanikiwa kufika mbali na mkono wa Makella. Hivyo, aliamua kuhakikisha anafikia makubaliano na mmoja wa madereva wa magari hayo.
Lakini kuna wepesi gani katika kulifanikisha suala hilo? alijiuliza. Hakuwa zaidi ya hatua mia mbili kutoka Kiyovu Hotel ambako ametoroka huku kaiba fedha kutoka katika mifuko ya suruali ya ‘mpenzi’ wake aliyemleta humo.
Hakupenda kujipa matumaini kuwa Makella atatulia tu pindi atakapogundua kuwa dola zake 2,000 za Marekani zimeibwa. Hatatulia! Judith alilitambua fika hilo jambo. Atakachofanya Makella ni kulivalia njuga suala hilo. Atawakimbilia wahudumu wa hoteli ambao nao wataharakisha kuwasiliana na walinzi. Walinzi nao katika kutaka kuhakikisha kuwa siyo wafanyakazi ‘wachovu’, watahaha huku na kule, nje na ndani ya hoteli wakimsaka mithili ya msako wa gaidi au haini!
Usingepita muda mrefu kabla hawajamkuta  pale kando ya barabara na kumsulubu kwa jinsi watakavyo kabla ya hatua yoyote nyingine kuchukuliwa na labda hatua hiyo ikiwa ni kumchinja kama kuku!
Hakuwa tayari kutiwa mbaroni na watu hao na kwa kuwa alijua kuwa ana pesa, hakutaka kusababisha uzembe utakaowafaidisha hao watakaomsaka. Alijua kuwa mbele ya pesa lolote linawezekana hata kama ni gumu kiasi gani.
Mbele kidogo,  kiasi cha hatua hamsini hivi, kulikuwa na duka kubwa lililosheheni bidhaa mbalimbali. Lilikuwa wazi, wateja wakiingia na kutoka. Kando ya duka hilo kulikuwa na teksi kadhaa zilizokuwa zikiwasubiri wateja. Judith aliichangamsha akili yake katika kufanya kila jambo kwa haraka na kwa umakini, hivyo aliifuata teksi moja na kuingia haraka.
********** 
AWALI ilimwia vigumu Makella kuamini kuwa Judith hayumo chumbani. Kwa sekunde kadhaa aliduwaa katika mlango wa bafu akikodoa macho chumbani. Kaenda wapi? Swali hilo lilirandaranda akilini mwake kwa mshangao.
Taratibu akatoka bafuni humo na kuufunga mlango taratibu vilevile. Akahisi kengele ya hadhari ikilia kichwani mwake. Nywele zikamsimama, na mara hima akaufuata mlango mkubwa wa kutokea chumbani humo. Akajaribu kuufungua.
Haukufunguka!
“Umefungwa!” akaropoka kwa sauti iliyojaa fadhaa na kugeuka huku na kule kama atazamiaye kuupata ufumbuzi wa tatizo lililojitokeza. Akashusha pumzi ndefu, macho kayatoa pima!
Akageuka na kurudi haraka kwenye nguo zake. Akainyanyua suruali iliyokuwa sofani ili  aivae. Lakini jambo jingine likamshtua; kitambulisho cha uraia kilikuwa sofani huku mifuko ya nyuma ikiwa  ikining’inia nje.
Hakuhitaji kukisumbua kichwa kufikiria ni kipi kilichomsibu. Ameibiwa! Ndiyo, ameibiwa! Hilo halikuwa jambo la siri tena. Mmoja wa mifuko ya suruali ulikuwa umehifadhi pesa nyingi, dola 2,000 za Marekani, pesa alizozipata mchana katika harakati zake za uwajibikaji dhidi ya Watutsi.
Sasa hazimo!
“Mungu wangu!” aliropoka tena. Mara akakurupuka kuitwaa bunduki na kuishika mikononi mithili ya mtu aliye tayari kuitumia dakika hiyohiyo! Kwa takriban dakika nzima akabaki kaduwaa, akili imedumaa!
Mara kama aliyezinduliwa, akaitupa bunduki hiyo pale kitandani. Akili mpya ikamjia. Akaifuata simu na kubonyeza tarakimu kadhaa, akilenga mapokezi.
“Tukusaidie?” sauti ya kike ilipenya masikioni mwake baada ya muda mfupi.
“Njooni mnifungulie!” Makella alibwata simuni. “Njooni haraka nimefungiwa mlango kwa nje!”
Ulikuwa ni ujumbe uliomshtua na kumshangaza mhudumu wa mapokezi. “Chumba namba ngapi?” aliuliza.
“Kumi na moja!”
Papohapo mhudumu akautwaa ufunguo wa akiba wa chumba namba 11 na kutoka hima. Akaiona lifti ya kupandia huko ghorofani ni kama vile itamchelewesha. Akazikwea ngazi mbili, mbili hadi huko katika ghorofa ya kwanza. Punde akawa ameshaufungua mlango wa chumba namba 11. Akakutana uso kwa uso na Makella.
“Umemwona yule malaya?” lilikuwa ni swali lililomtoka Makella kwa jazba, akimtazama mhudumu huyo kama aliyehusika na kufungiwa kwake.
“Malaya! Malaya gani?”
“Yule niliyekuja naye!”
Mhudumu akatokwa macho pima. Kisha akauliza, “Kwani imekuwaje?”
Makella akazidi kughadhibika. Akamkwida mhudumu huyo. “Umeshirikiana naye, siyo?” alimuuliza huku akiendelea kumkwida.
“Kwani vipi…?”
Kofi kali lililotua katika shavu lake la kulia lilimkata kauli.
“Sema! yule malaya yuko wapi?”
“Ametoka!” binti yule alijibu.
Kofi la pili!
“Jamani utaniua bure!” mhudumu huyo alilalamika kwa sauti iliyoashiria kilio.
“Nitakuua kweli!” Makella aliwaka. “Sema yuko wapi…sema…sema au nakuua!”

“Subiri nikwambie!” mhudumu alisihi.

Itaendelea kesho...

No comments:

Post a Comment