Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Monday, 9 June 2014

POLE ZITTO KABWE, BURIANI MAMA SHIDA BINTI SALUM!

  
Ndugu zangu,
Leo hii sina kingine cha kusema zaidi ya kwanza kumpa pole za dhati Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Zuberi Kabwe, kwa kuondokewa na mzazi wake mpendwa Mama Shida binti Salum.
Ni msiba mzito kwa Zitto na wanafamilia. Majonzi yetu sisi katu hayataweza kuyafikia yale ya walengwa.
Zitto yuko katika kipindi kigumu, pengine kuliko vyote katika maisha yake, kwa sababu haombolezi msiba wa mama peke yake, bali anayo mengi na ni fundo kubwa moyoni mwake ambalo wa kulifungua ni Mungu pekee.
Mama Shida binti Salum hakuwa mzazi tu, bali alikuwa rafiki kwa Zitto na mshauri wake katika masuala mbalimbali ya maisha, yakiwemo ya siasa.
Tukumbuke kwamba, hakuwa tu mwanachama na mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, bali pia alikuwa Mwenyekiti wa Chama cha Walemavu Tanzania (Chawata), hivyo alikuwa mtetezi mkubwa wa walemavu wote nchini.
Mama huyu atakumbukwa kwa jinsi alivyokuwa akimpa moyo Zitto tangu mwaka 2009 wakati Zitto alipotangaza nia yake ya kugombea uenyekiti wa Chadema, uamuzi ambao ulimfanya akatukanwa na wanachama wengi wa chama hicho waliokuwa wakimuunga mkono mwenyekiti wa sasa Freeman Mbowe.
Ingawa alishauriwa na watu wengi wenye busara, lakini pengine ushauri wa mama yake aliuzingatia zaidi na akaamua kujitoa katika kinyang’anyiro kile.
Akahusishwa na kashfa mbalimbali za kukihujumu chama, kubwa zaidi ni ile kashfa ya mwaka 2013 iliyosababisha Chadema imsimamishe uanachama na kumvua nafasi zote za uongozi hadi Bungeni.
Kile kilikuwa kipindi kigumu sana kwa mwanasiasa kijana kama Zitto ambaye bado hajafikisha hata miaka 40. Lakini kwa hekima ya mama yake, mwanasiasa huyu ameendelea kupambana na kusimama imara kwa kipindi chote hicho.
Maumivu makali zaidi aliyoyapata Zitto ni katika kipindi anamuuguza mama yake, ambapo siku chache tu kabla ya mauti kumfika mzazi wake huyo, yeye alizushiwa kashfa Bungeni, tena kupitia kwenye Hotuba Kivuli ya Wizara ya Habari, Utamaduni na Vijana, iliyosomwa na waziri kivuli Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ kwamba alitafuna mamilioni ya fedha kutoka Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) na Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa) kupitia LekaDutigite na Gombe Advisors.
Nakumbuka Zitto mwenyewe aliamua kujibu tuhuma hizo kwa majonzi makubwa na uchungu mwingi akasema, namkunukuu: Nasikitika kwamba katika hali niliyonayo ya kumwuguza mama yangu naingizwa kwenye siasa za majitaka. Kampuni ya LekaDutigite inamilikiwa na wasanii. Gombe Advisors ni kampuni isiyofanya faida (Company limited by guarantee) na haina maslahi yeyote ya kibiashara.
Wasanii wa Kigoma wamefanya kazi na TANAPA na NSSF, kazi ambazo zinajulikana na zipo. Leo mpigie simu mfanyakazi yeyote wa NSSF utasikia kazi ya wasanii hao.Kwa namna yeyote ile hii ni ishara ya kukosa ubinaadam maana waliyoyasema wanajua sina faida yeyote ya kifedha, leo wala kesho kwa LekaDutigite na Gombe Advisors.
Kipindi ambacho mama yangu yupo mahututi, tena mjumbe wa kamati kuu ya chama chao, pole ninayopewa ndiyo hiyo. Hakuna namna ya kukosa ubinaadamu zaidi ya hivi.
Hata hivyo, ni vema CAG afanye ukaguzi haraka sana na Mimi binafsi nitawajibika iwapo itaonekana kwa namna yeyote ile nina maslahi ya kifedha katika LekaDutigite na gombe advisors..
Ni ushetani. Ni roho mbaya. There are limits to political attacks.” Mwisho wa kunukuu.
Haya yalikuwa maneno mazito mno ya Zitto, na kwa hakika siku mbili tu baada ya kuyasema hayo, yaani Juni 2, mama yake akakata roho.
Yapo mengi yaliyosemwa kuhusiana na msiba huo, sikuwepo mimi lakini nawanukuu wanaosema, kwamba wakati Shida binti Salum akiwa mahututi, hakuna hata kiongozi yeyote wa Chadema – ngazi ya juu – ambaye alikwenda kumjulia hali. Lakini tulimuona Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete ‘Mtu wa Watu’, akimtembelea mama huyo Mei 28 pale hospitali ya Ami.
Tumesikia pia kwamba, hata katika mazishi ya mama huyo, hakuna kiongozi yeyote wa juu wa Chadema aliyekwenda kushiriki! Pengine mwenyekiti wake Freeman Mbowe na Katibu Mkuu Dk. Wilbrod Slaa wanayo maelezo ya kutosha.
Binafsi hili la viongozi hawa wa juu kutohudhuria msiba wa Shida binti Salum haliniingii akilini kabisa hasa kwa kuwa alikuwa ni mwanachama wao na mjumbe wa Kamati Kuu ya chama hicho. Tunafahamu Chadema ina mgogoro na Zitto, lakini hatujui kama kumbe ilikuwa na mgogoro na mama yake pia ndiyo maana hata kwenye msiba viongozi hao wakuu hawakwenda.
Najiuliza tu jambo moja, kwamba mwaka 2012 baada ya mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Iringa (IPC) Daudi Mwangosi, kuuawa kwa bomu pale Nyororo kwenye mkutano wao, hawa jamaa walikuja mbio na wakataka ‘kuuteka’ msiba huo. Busara zaidi ilitumika.
Wakatoa ahadi nyingi za kuwasomesha watoto wa marehemu ambazo sidhani kama zimetekelezwa, japo kwa uchache wake.
Wakati wa kumbukumbu ya mwaka mmoja wa kifo cha Mwangosi Septemba 2, 2013, Chadema wakateka suala la kujenga mnara wa kumbukumbu pale Nyororo, licha ya Umoja wa Klabu za Wanahabari Tanzania (UTPC) kugoma.
Sasa ilikuwaje wakalivalia njuga suala la Mwangosi ambaye hata katika vikao vya chama alikuwa haingii lakini wakamtelekeza mtu aliyekuwa akitetea na kuzinadi sera za chama hicho?!
Walikuwa na maslahi gani kwa Mwangosi? Au walitaka kutumia kivuli cha kwamba alikuwa mwandishi wa habari ili waandikwe sana na vyombo vya habari na kupongezwa?
Ndiyo. Siyo lazima kufanya kazi za misiba kama watu wengine wanavyosema kupitia mitandao ya kijamii, lakini sidhani kama ni busara kulala kiyoyozi wakati unaposikia mwanao ameanguka na kuvunjika mkono, achilia mbali kufariki!
Nichukue fursa hii tena kukupa pole nyingi Zitto Kabwe na kushauri kwamba rehema ya Mungu iwe juu yake, akupe ujasiri wa kukabiliana na magumu yote katika kipindi hiki, akujaalie hekima na busara ili uweze kuyakabili hata yale ambayo ulikuwa huwezi peke yako.
Mungu ni mwema, na hakika atampumzisha kwa amani Shida Binti Salum. Japo wengine hatukuhudhuria msiba huo, lakini sote tumeguswa na msiba huo. Amen!

Daniel Mbega
Iringa - Tanzania
0656-331974

No comments:

Post a Comment