Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Monday, 9 June 2014

RIWAYA TAMU: JUDITH…JUDITH…! - 6


INNOCENT A. NDAYANSE (ZAGALLO)
 0755 040 520 / 0653 593 546 


Judith anaulizwa swali gumu na Makella aliyeamuru wazazi na ndugu zake wauawe. Lakini anaona jibu lolote atakalolitoa ama litaokoa maisha yake au litamfanya Makella amuue na yeye ingawa anadai anampenda. Je, atafanyaje? Ungana na msimulizi wako…

“Hakuna tatizo,” ni jibu lililomtoka baada ya kuzitafakari kwa kina kauli za Makella. Na alijibu hivyo huku akijua kuwa ilimpasa kutumia akili katika kufanya lolote lile la kumtoa katika mikono ya jahili huyo.
Kwamba ni kipi atakachokifanya katika kujinusuru, hilo lilikuwa ni suala la kutekelezwa kwa umakini wa hali ya juu. Hakupaswa kuwa na papara, hakutaka kumfanya Makella agundue mapema kuwa kuna jambo tofauti na matarajio yake.
Lilikuwa ni jibu lililomfariji na kumsisimua Makella kwa kiwango kikubwa. Papohapo akamvuta Judith na kumkumbatia, kisha akambusu kwenye paji la uso wake huku mikono yake iliyokosa uvumilivu ikitalii hapa na pale katika mwili wake mwororo uliovutia.
Miongoni mwa mambo ambayo Judith hakuyapenda na yalikuwa ni kero zaidi ya kero, ni kitendo cha kukumbatiwa-kumbatiwa, kupapaswa, kutomaswa, kupigwa busu au kufanywa vyovyote vile kwa namna ya kimahaba na mtu, mwanamume asiye mpenzi wake wa dhati.
Makella alikuwa ni mmoja wa watu hao, na alimkera! Lakini afanye nini? Hakuwa na budi kufuata ule usemi wa “mtaka cha uvunguni sharti ainame.”
Ok, twen’zetu,” Makella alimwambia Judith huku akimshika mkono na kuanza kutembea tena. Dakika tano baadaye walikuwa Kiyovu Hotel, wakiwa wamesimama kaunta, na kwa sauti ambayo haikutofautiana na amri alimwambia mhudumu wa kike aliyekuwa mbele yao: “Chumba tafadhali.”
Single au double?”
Single.
“Kipo.”
Dakika chache zilizofuata  zilikuwa za kukamilisha taratibu za upangaji, kisha mhudumu akawapeleka chumbani.
********** 
KILIKUWA ni chumba kilichostahili kuitwa chumba cha daraja la kwanza. Kitanda kikubwa, zulia zito sakafuni, jokofu lililosheheni vinywaji na televisheni ndogo iliyoegeshwa ukutani katika kijisanduku cha aina yake zilikuwa ni samani zilizotosha kukifanya chumba hicho kuwa maridadi. Isitoshe, simu kwa ajili ya kuwasiliana na utawala wa hoteli ilikuwa juu ya kimeza kidogo kilichokuwa kando ya sofa mbili.
Mpangaji hahitaji kuhangaika kuuliza wapi bafu na choo vilipo. Ni kiasi cha mtu kujua kusoma, ama Kiingereza, Kiswahili, Kinyarwanda au Kifaransa. Milango miwili yenye maandishi ya lugha hizo, yenye  maelekezo kuhusu matumizi ya vyumba hivyo ilikuwa kulia mwa chumba hicho.
“Karibu..karibu mpenzi,” Makella alimwambia Judith huku akimtazama kwa namna iliyoashiria hitaji kamili la starehe ya mapenzi.
Ilikuwa ni tazama ambayo Judith hakuhitaji mtu wa kumfafanulia kuwa tayari Makella yuko mbali na yu taabani, uroho wa fisi ukiwa umekwishamtawala. Lakini hakuhofu. Aliyaepuka macho hayo huku moyoni akisema, tutaona. Akalifuata sofa moja na kuketi kwa kujiachia kihasarahasara, nusu kaketi, nusu kalala.
Makella alimtazama kidogo kisha akaurudisha mlango na kumfuata pale sofani. “ Nakupenda Judith,” alinong’ona huku akimpapasa katika paja la kulia.
Kwa Judith, upapaswaji huo haukumletea msisimko wowote. Zaidi, alihisi kupapaswa na popobawa, kiumbe wa ajabu ambaye miaka kadhaa iliyopita aliviteka vyombo mbalimbali vya habari hususan yale magazeti pendwa akidaiwa kuwa alikuwa na tabia ya kuwaingilia wanaume  na wanawake kimiujiza usiku wakiwa wamelala.
Hakuwa radhi kuuachia mwili wake utumiwe na mtu huyu ambaye hakumtofautisha na shetani,  achilia mbali huyo popobawa. Alimwogopa, na zaidi alimchukia. Haikumwingia akilini asilani kumwachia Makella apenye katikati ya miguu yake na kustarehe. Hapana, hakuwa tayari kwa hilo, labda maiti yake ndiyo inajisiwe.
Hivyo, wakati Makella akimpapasa huku akimtazama kwa matamanio makubwa, yeye alikuwa mbali kifikra, akipanga namna ya kujiokoa.

Alishakichunguza chumba hicho kwa makini. Kumtoroka Makella kwa kupitia dirishani lilikuwa ni jambo lisilowezekana. Dirisha kubwa lililokuwa kaskazini mwa chumba hicho, lilisheheni nyavu imara na nondo madhubuti, hivyo isingekuwa rahisi kufanya chochote katika kujiokoa.
Itaendelea kesho...

No comments:

Post a Comment