Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Saturday 24 May 2014

WWF YAKABIDHI VIFAA KWA WAKULIMA WA MPUNGA PAWAGA

 Vifaa vya kupalilia mpunga vikiandaliwa kabla ya kukabidhiwa.
 Ofisa Elimu ya Mazingira wa Shirika la WWF ambaye pia ni Kaimu Meneja wa Kanda, Mwamini Masanja (wa pili kushoto) akizungumza na akinamama wa Kijiji cha Kinyika katika Kata ya Mlenge wilayani Iringa wanaoshiriki mafunzo ambayo shirika hilo limefadhili. 
 Mwezeshaji wa mafunzo hayo kutoka Shirika la RUDI, Shalimwene Ndondole, akimpa maelezo Mwamini Masanja, Kaimu Meneja wa Kanda wa WWF. Wa pili kushoto ni Edna Luyangi, Ofisa kutoka Mamlaka ya Bonde la Mto Rufiji.
 Diwani wa Kata ya Mlenge, Rashid Matimbwa (wa tatu kushoto) akimsikiliza mwezeshaji wa mafunzo ya kilimo bora cha mpunga, Shalimwene Ndondole. Wa pili kushoto ni Mwamini Masanja, Kaimu Mkurugenzi wa shirika la WWF Kanda ya Nyanda za Juu Kusini. 
 Ofisa Utawala na Fedha wa WWF, Alen (katikati) akimkabidhi Diwani wa Kata ya Mlenge, Rashid Matimbwa, mojawapo ya zana za palizi.
 
 Shalimwene Ndondole akimwelekeza mmoja wa wakulima namna ya kutumia vifaa vya palizi katika shamba la mpunga kwenye Kijiji cha Kinyika wilayani Iringa.
 
 
 

Na Daniel Mbega, Iringa

HATIMAYE Mfuko wa Kimataifa wa Kuhifadhi Mazingira (WWF) mkoani Iringa umekabidhi vifaa vya upaliliaji wa zao la mpunga kwa wakulima wa Kata ya Mlenge, Tarafa ya Pawaga wilayani Iringa leo hii.
Vifaa 12 vilivyotolewa vitakavyosaidia kupalilia pamoja na kuvunia vimegharimu Shs. 960,000, ambapo vitawanufaisha wakulima wa mpunga wa Skimu ya Umwagiliaji ya Mlenge, kutoka vijiji vya Kinyika, Isele, Kisanga na Magombwe.
Mbali ya vifaa hivyo, WWF pia imegharamia mafunzo hasa katika vijiji vya Kata ya Pawaga, mafunzo ambayo yanaendeshwa na Shirika lisilo la kiserikali la Rural Urban Development Initiative (RUDI) la mjini Iringa.
Mafunzo na vifaa hivyo, pamoja na gharama nyingine za uendeshaji, vimegharimu Shs. 8 milioni, ambazo ndizo zilizoombwa na Idara ya Kilimo kufanikisha zoezi hilo.
Katika mafunzo hayo, wakulima wanaelekezwa namna ya kushiriki katika kilimo bora chenye tija kwa uchaua mbegu bora kwa kuzingatia kanuni bora za kilimo shadidi na kupanda kwa nafasi ya 25sm mstari kwa mstari na mche kwa mche.
Mbegu zinazopendekezwa kwa kilimo chenye tija ni aina ya Saro 5 (TXD 306) ambayo imeonekana bora zaidi, hairefuki, inatoa machipukizi mengi, ina uwezo wa kutoa mavuno mengi kutoka magunia 30 hadi 40 kwa ekari moja ambazo zina ujazo wa 80kg.
Inaelezwa kwamba, mbegu hiyo tayari imeanza kuonyesha matunda mazuri hasa kwa wakulima wa Skimu ya Tungamalenga ambao tayari wamekwishapatiwa mafunzo na shirika hilo la RUDI tangu mwaka 2013.
Shirika la WWF limejikita katika kuhamasisha shughuli za utunzaji wa mazingira pamoja na maendeleo ya jamii, ikiwemo kilimo, ambapo limekuwa likishiriki kikamilifu katika utoaji wa elimu na vifaa kwa wanajamii.
Shalimwene Kombo Ndondole kutoka shirika la RUDI ndiye aliyekuwa mwezeshaji wa mafunzo hayo katika vijiji vinne vya kata hiyo ambapo amesema mafanikio yameonekana kutokana na semina hizo ambapo washiriki wameonekana kubadilika kimtazamo.
Amesema ikiwa wakulima watazingatia mafunzo na maelekezo ya kilimo bora, wanaweza kuvuna magunia 40 kwa kutumia mbegu aina ya Saro 5 na ikiwa watatumia mbegu yao ya Fire Dume, wanaweza kupata mpaka magunia 30 kwa ekari moja.
“Kwa kufuata misingi ya kilimo bora, wakulima watapata mavuno mengi kwa ajili ya chakula na ziada, hivyo kuliwezesha taifa kuwa na akiba ya kutosha ya chakula,” alisema Ndondole.
Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Mlenge, Rashid Ibrahim Matimbwa, amesema amefarijika kwa ujio wa shirika la RUDI na WWF kutoa mafunzo na kuwapatia vifaa, kwani utakuwa msaada mkubwa wa kubadili kilimo kwa wananchi wake.
Amesema wakulima wa kata hiyo walikuwa wakitumia kilimo cha kienyeji ambacho hakikuwa kikitoa mavuno mengi, lakini kwa mafunzo waliyopata kuna dalili njema za mafanikio kwa misimu ijayo.
“Kwa kweli ninawashukuru RUDI na WWF kwa msaada huu ambao wameutoa kwa wakulima wetu ambao hawakuwa na elimu yoyote kuhusiana na kilimo bora cha mpunga, tunaahidi kutoa ushirikiano wa kutosha na tunawaomba waendelee kutusaidia,” amesema.
Naye Kaimu Meneja wa WWF wa Nyanda za Juu Kusini, ambaye pia ni Ofisa Elimu ya Mazingira wa shirika hilo, Mwamini Masanja, amesema walikuwa wakitafuta fursa ya kutoa mafunzo kwa wakulima kuhusu kilimo shadidi, hivyo wanaona ni sehemu muhimu ya kuisaidia jamii kupata maendeleo.
“Tulikwenda Halmashauri ya Wilaya kuomba eneo la kusaidia elimu hii, wakasema tayari shirika la RUDI linafanya shughuli hiyo, hivyo kutuomba tusaidia kugharamia mafunzo pamoja na vifaa, ambavyo leo hii tumevikabidhi,” amesema.
Amesema maendeleo yoyote yanakuja kutokana na ushirikiano na kwamba hata mafanikio waliyofikia ni kutokana na ushirikiano baina ya mashirika hayo mawili pamoja na serikali.
Hata hivyo, ameshauri wakulima wakae katika vikundi ili waweze kujikwamua, vinginevyo wanaweza kushindwa kujinunulia vifaa vya kilimo.
Ofisa wa Bonde la Mto Rufiji, Edna Luyangi amesema mafunzo wanayopata wakulima yatasaidia hata uhifadhi wa maji na matumizi bora bila kuathiri shughuli nyingine za kijamii.
“Kilimo shadidi kitasaidia kupunguza matumizi holela ya maji hasa katika kipindi hiki cha mabadiliko ya tabia nchi ambayo yamesababisha ukame,” amesema.


No comments:

Post a Comment