Pages

Pages

Pages

Friday 2 May 2014

MAONI: MSHIKAMANO NDIYO UTAWAKOMBOA WAFANYAKAZI


Wafanyakazi wa Shirika la Madini la Taifa (Stamico) wakipita mbele ya Rais wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi), iliyofanyika kitaifa Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam jana
Wafanyakazi kote duniani jana waliungana kuadhimisha Siku ya Wafanyakazi Duniani. Hapa nchini maadhimisho hayo yalifanyika kitaifa jijini Dar es Salaam kwa maandamano ya wafanyakazi kuelekea Uwanja wa Uhuru ambako Rais Jakaya Kikwete alilihutubia Taifa. Maadhimisho hayo pia yalifanyika katika ngazi ya mikoa kwa maandamano, hotuba za viongozi na burudani za kila aina.
Kama ilivyotegemewa na wengi, maadhimisho hayo hayakuwa na shamrashamra wala msisimko uliokuwa ukishuhudiwa miaka kadhaa iliyopita, kutokana na matatizo mengi yanayowakabili wafanyakazi, yakiwamo ya kiuchumi na mikwaruzano isiyoisha kati yao na Serikali.
Vyama vya wafanyakazi, chini ya Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (Tucta), vimekosa ushawishi kwa wanachama kutokana na kushindwa kuishinikiza Serikali kutekeleza madai yao ya muda mrefu kama nyongeza za mishahara na kuwapo mazingira mazuri katika sehemu zao za kazi.
Kihistoria, maadhimisho hayo ambayo hufanyika Mei Mosi kila mwaka, hulenga kukumbuka harakati za wafanyakazi na kuwahamasisha kudai haki zao kutoka kwa waajiri wao. Siku hiyo pia hutoa fursa kwao kufanya tathmini jadidi kuhusu matatizo waliyokumbana nayo katika kazi zao, lakini pia hupata fursa ya kuangalia mafanikio yaliyopatikana katika uzalishaji na kutafuta mbinu na mikakati mipya ya kuongeza ufanisi ili pande zote mbili za waajiri na wafanyakazi zifaidike. Wafanyakazi hutumia siku hiyo kujadili misimamo ya pamoja kuhusu namna ya kudai na kupata haki zao kwa njia zinazokubalika kisheria.
Hakika, siku hiyo hutoa fursa kwa wafanyakazi kukuza mshikamano miongoni mwao. Mshikamano huchukuliwa kama silaha na mkakati maalumu wa kujadiliana na wakati mwingine kukabiliana na waajiri, kwa kuwa wanatambua kwamba wasipopambana kwa pamoja watasambaratishwa. Lakini pia wafanyakazi hutumia siku hiyo kubadilishana mawazo na uzoefu na wenzao, kwani kuna waliopata mafanikio makubwa zaidi katika kazi zao kuliko wengine.
Hapa nchini wafanyakazi bado hawajawa na mazingira mazuri ya kusherehekea Mei Mosi katika muktadha tulioutaja hapo awali. Pamoja na kukabiliwa na hali ngumu ya kiuchumi, kwa maana ya mishahara midogo mno isiyolingana na gharama za maisha kutokana na mfumuko wa bei usioisha na wafanyakazi kuzungukwa na mazingira magumu katika sehemu zao za kazi. Pia bado vyama vya wafanyakazi siyo tu ni dhaifu katika kusimamia haki na stahili za wanachama wao, bali pia bado vinashindwa kusimama kidete kujadiliana na Serikali. Vyama hivyo siyo tu vinaitetemekea Serikali, bali pia  vinashindwa kutambua kwamba sheria za nchi, ikiwamo Sheria ya Kazi zinavipa mamlaka ya kusimamia haki za wafanyakazi.
Ndiyo maana vyama hivyo vimeshindwa kuwaongoza wafanyakazi kuadhimisha siku yao ya Mei Mosi iliyoadhimishwa jana kwa kukaa nao na kujadiliana kuhusu masuala yanayowagusa na kuyatafutia suluhisho. Badala yake wanasiasa ndiyo wameachiwa jukumu la kupanda majukwaani na kuwahutubia. Matokeo yake ni waajiri, ikiwamo Serikali kujiona wako juu ya vyama vya wafanyakazi na wana haki ya kuwadharau viongozi wake.
Tunadhani umefika wakati kwa waajiri, hasa Serikali  kuvisikiliza na kuviheshimu vyama hivyo, kwa maana ya kutekeleza ahadi lukuki ambazo miaka nenda miaka rudi wamekuwa wakizitoa bila kuzitekeleza. Kwa hali hiyo, tunadhani kauli mbiu ya Siku ya Wafanyakazi mwaka huu kwamba “Utawala Bora Utumike Kutatua Kero za Wafanyakazi”, ni kejeli.
CHANZO, MWANANCHI

No comments:

Post a Comment