Simba wapandao miti wanapatikana katika Hifadhi ya Manyara tu hapa duniani
Na Mwandishi wa brotherdanny5.blogspot, Arusha
ZIWA Manyara lililopo ndani ya hifadhi ya Manyara, lipo hatarini kutoweka kutokana na uharibifu wa mazingira unaofanywa na wananchi wa maeneo hayo kwa kulima kando na kulisha mifugo pembezoni mwa ziwa hilo, na hivyo kupelekea sehemu kubwa ya ziwa hilo kujaa matope.
Aidha ziwa hilo ambalo kwa kipindi cha miaka 50 iliyopita lilikuwa na urefu wa kina cha mita nne lakini hadi sasa kutokana na athari hizo za kujaa matope kina urefu wa kina moja na nusu ,huku mbili na nusu yote zikiwa zimejazwa na matope.
Hayo yalisemwa jana na Kaimu Mhifadhi hifadhi ya ziwa Manyara, Yustina Kiwango wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kuhusiana na hali halisi ya ziwa hilo hivi sasa.
Alisema kuwa,endapo hali hiyo itaendelea huku wadau mbalimbali wakishindwa kuchukua hatua za haraka kunusuru ziwa hilo, miaka hamsini ijayo ziwa hilo halitakuwepo hali ambayo italeta athari kubwa kwa jamii na hata hifadhi hiyo.
Alifafanua kuwa, ziwa hilo limekuwa ni kivutio sana kwa watalii wa ndani na nje ya nchi hali ambayo limekuwa likiipa umaarufu mkubwa hifadhi hiyo.
"Kwa kweli hifadhi hii ya ziwa Manyara ni kivutio kikubwa sana kwa watalii lakini tunasikitika sana kwani miaka hamsini ijayo halitakuwepo kabisa kutokana na athari mbalimbali, hivyo ni jukumu la wadau mbalimbali wakiwemo wa wizara ya kilimo,mifugo na hata maliasili katika kuweka nguvu zao kwa pamoja ili kunusuru ziwa hilo," alisema Kiwango.
Hata hivyo alitaja athari nyingine ambazo zimekuwa zikichangia ziwa hilo kupotea ni kipindi cha kiangazi ambacho matumizi ya maji yanakuwa makubwa sana na hivyo asilimia kubwa ya wananchi kutegemea ziwa hilo.
Aidha alitaja faida zitokanazo na ziwa hilo ambazo zimekuwa ni kivutio kikubwa kwa watalii kuwa ni pamoja na kuongezeka kwa idadi kubwa ya ndege aina ya flamingo ambao wamekuwa wakiiishi ndani ya ziwa hilo na hivyo kufanya kuendelea kuwa kivutio kwa watalii.
No comments:
Post a Comment