Pages

Pages

Pages

Friday 9 May 2014

BAJETI ITOE KIPAUMBELE KWENYE KILIMO, ELIMU NA AFYA


Na Daniel Mbega

BUNGE la Bajeti limeanza mjini Dodoma, ambako tunaambiwa kwamba serikali imepanga kutumia kiasi cha trilioni 19 kwa shughuli za utawala na maendeleo.
Ingawa bajeti halisi haijasomwa, lakini makadirio yaliyotangazwa awali yanaonyesha wazi kuna ongezeko la bajeti hiyo ikilinganishwa kwa mwaka unaoishia Juni 30 mwaka huu.
Fedha hizi ni nyingi, ingawa kwa uhalisi kushuka kwa thamani ya Shilingi nako kunaifanya bajeti hiyo ionekane ndogo zaidi.
Hata hivyo, bajeti hii ni muhimu sana kwa maendeleo ya taifa, hivyo hatutarajii kabisa kuona ngonjera, majigambo, tambo na hata kususa kwa wabunge kwenye mijadala ya bajeti hiyo kama ambavyo tumeshuhudia katika vikao vingi tu, likiwemo Bunge Maalum la Katiba.
Watanzania wametega masikio yao huko Bungeni kuona wawakilishi wao wanajadili vipi bajeti ambayo inaweza kuwakomboa, siyo ablakhadabla ambazo haziwasaidii chochote katika maisha yao ya kila siku.
Tumemsikia wenyewe Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Kikwete, akitangaza wakati wa kilele cha Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi) kwamba mishahara ya wafanyakazi itaongezwa na pia kodi ile ya P.A.Y.E itapunguzwa ili kuwapunguzia mzigo mkubwa wa makato.
Hata hivyo, hatujawahi kusikia serikali ikitangaza unafuu kwa wananchi wa vijijini, hasa wakulima na wajasiriamali wengine, ambao asilimia 83 iko huku vijijini.
Wananchi hawa wanalitazama Bunge la Bajeti kama linaweza kuwaletea unafuu katika huduma mbalimbali za maendeleo, zikiwemo afya, elimu na hasa kilimo ambacho ndicho kinachochukua sehemu kubwa ya ajira ya Watanzania walio wengi.
Tumeshuhudia wenyewe serikali ikizindua Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN) katika sekta kadhaa nchini, lakini matokeo hayo hayawezi kuja bila kuwa na bejeti zinazoweza kuwakomboa wananchi wa vijijini, vininevyo tutajidanganya kwa kutaka ‘Kuibadili Tanzania iwe Singapore’!
Elimu yetu haiwezi kupanda kiwango ikiwa mitaala yenyewe ni mibovu isiyokidhi viwango vya kimataifa, huku shule zetu za msingi na zile za kata zikiwa hazina walimu, achilia mbali watoto wetu kuendelea kuketi chini na walimu kulilia madai yao yasiyosikilizwa kwa miaka mingi sasa.
Lakini taifa haliwezi kuwa na wazalishaji imara ikiwa huduma za aya ni duni, huku wajawazito wakijifungua kwa kutumia mwanga wa tochi na wanaobahatika kwenda hospitalini lazima wakodishe ambulance za umma ambazo sehemu nyingine zimekuwa vitegauchumi vya wakubwa wa halmashauri.
Hatuwezi kusema tunaleta matokeo makubwa sasa ikiwa mkulima, ambaye ndiye mzalishaji mkuu nchini, anaendelea kutumia jembe la mkono miaka 53 baada ya Uhuru. Huko ni kujidanganya.
Ikiwa leo hii ruzuku ya pembejeo katika kijiji chenye wakulima 2,500 zinaletwa vocha 200, tunawezaje kujidanganya kwamba tunaongeza uzalishaji? Zile fedha zetu walizorudisha wale wezi wa EPA si tuliambiwa zinaelekezwa kwenye kilimo? Sasa zinafanya kazi gani?
Halafu zile chenji za Rada nazo tuliambiwa zimeelekezwa kwenye elimu kwa ajili ya ununuzi wa vitabu, lakini huko tumeshuhudia uhuni usio na kifani kwa darasa moja kuwa na vitabu zaidi ya viwili vya somo moja. Kisa, soko huria ambalo limekuwa holela na lisilojali maendeleo ya elimu.
Kwa mukhtadha huo basi, Watanzania wanatamani sana kuona bajeti ya mwaka huu ikielekezwa katika maeneo hayo matatu nyeti, huku kilimo kikipewa kipaumbele cha kutosha na kuwawekea wakulima mazingira mazuri zaidi ya masoko ya bidhaa zao tofauti na sasa ambapo mazao yao ama yanaozea shambani kwa kukosa soko au wanapunjwa kutokana na kutokuwepo kwa mfumo mzuri.
Hakika, maendeleo ya Tanzania yanategemea zaidi bajeti na kwa maana hiyo mjadala katika Bunge la Bajeti ni muhimu mno ili uweze kuleta taswira njema ambayo itawanufaisha Watanzania wote.
Kelele za ‘Wanafiki waseme Ndiyoooo’ zimewachosha Watanzania, lakini pia zile tabia za baadhi ya waunge, hasa wa upinzani kususa vikao kama ‘watoto wa mwisho’ haziwasaidii Watanzania na inabidi zikome mara moja.
Kama mambo hayaendi sawa ndani ya Bunge, ni vyema wakakomaa humo humo ili tuweze kuona nani ni mkorofi anayekwamisha maendeleo ya Watanzania, lakini wanapotoka nje ya Bunge mwisho wa siku Watanzania watawaona kwamba wao ndio wakorofi.
Waheshimiwa hawa wakumbuke kwamba, fedha zinazotolewa kama posho na mishahara yao ni kodi ya Watanzania wanayokatwa kuanzia kwenye pipi mpaka kwenye bia. Yaani kila bidhaa ambayo Mtanzania anainunua lazima akatwe kodi, na kodi hiyo ndiyo inayowaia jeuri wengine wanafanya mambo ya ajabu Bungeni.
Hakika Watanzania wanataka kuona bajeti inatoa vipaumbele kwenye afya, elimu na kilimo, sekta ambazo zinabeba dhima kubwa ya maisha yao.
Kinyume chake, matokeo makubwa sasa ni ndoto za mchana kama mkulima au mwananchi wa kijijini hajakombolewa.

Alamsiki.

No comments:

Post a Comment