Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), Samia Hassan Suluhu akiwasilisha bunge makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira kwa mwaka fedha 2014/15, mjini Dodoma jana. Picha na Edwin Mjwahuzi.
Dodoma. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), Samia Suluhu Hassan alikataa kueleza walipo waasisi sita wa Muungano ambao kambi ya upinzani ilidai kuwa waliuawa na kuzikwa handaki moja, badala yake akatumia nafasi hiyo kumshambulia mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu akidai hizo ni propaganda na upotoshaji.
Juzi wakati akiwasilisha hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani,
Lissu aliitaka Serikali kutoa maelezo bungeni kuhusu sababu za kuuawa kwa
waasisi sita wa Muungano wa Tangayika na Zanzibar na kuzikwa katika handaki
moja visiwani Zanzibar.
Lissu aliwataja waasisi hao kuwa ni Abdalah Kassim Hanga,
aliyekuwa waziri mkuu, Abdul Aziz Twalam aliyekuwa Waziri wa Fedha na Abdulaziz
na Saleh Akida aliyekuwa mjumbe wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar.
Pia aliwataja Othman Shariff, Mdungi Ussi na Jaha Ubwa ambao
alisema nao waliuawa na kuzikwa katika handaki moja eneo la Kama nje kidogo ya
Zanzibar.
“Tunataka kujua ukweli kama walifanya makosa, walishtakiwa
katika mahakama gani iliyowahukumu adhabu ya kifo... tunataka kuambiwa ukweli
kwanini mchango wao kuhusu Muungano umefichwa,” alisema Lissu juzi.
Lakini alipoulizwa kuhusu madai hayo, Waziri Hassan alionekana
kuzigeuza hoja hizo kuwa ni za Lissu pekee badala ya kambi ya upinzani na
kumshambulia mbunge huyo akidai kuwa ni mpotoshaji, anayepiga propaganda na
mchochezi.
Waziri huyo, ambaye ni Mzanzibari, alisema alipuuza maswali yote
kuhusu waasisi hao akisema mbunge huyo wa Chadema alipotoka katika hotuba yake
na ndio maana hakutaka kuzungumzia katika majumuisho ya bajeti ya ofisi yake
bungeni.
“Yule Lissu sio mkweli na ndio maana sisi tulimpuuza,” alisema
waziri huyo.
“Hakuna kitu kama hicho na endapo kingekuwepo sisi Serikali
tungeshatoa ufafanuzi ili watu wapate kujua ukweli wake,” aliongeza Waziri
Samia bila kutoa ufafanuzi wa nini kiliwatokea watu hao walioshika nafasi za
juu serikalini mara baada ya Mapinduzi na Muungano wa Zanzibar na Tanganyika.
Pamoja na kudai kuwa aliona hoja hizo ni upotoshaji, Waziri
huyo, ambaye pia ni makamu mwenyekiti wa Bunge la Katiba, aliwasihi wabunge wa
upinzani kupeleka hoja zao katika Bunge Maalumu la Katiba linalojadili uundwaji
wa Katiba Mpya, ambalo pia limetawaliwa na suala la muundo wa Muungano na kero
zake.
Waziri Samia alisema hoja hizo zinalenga kuwaaminisha Watanzania
mambo ambayo hayapo ili kuwajaza chuki dhidi ya Serikali yao na pia alidai zina
uchochezi ndani yake.
Waziri Samia aliwashauri wabunge pamoja na Watanzania kupuuza
kauli hizo akidai mbunge huyo hautakii mema Muungano na ndio maana anaibua
mambo aliyodai kuwa ni ya uongo na ya uchochezi.
Madai ya Lissu
Lissu alitoa madai hayo akinukuu kitabu cha Kwaheri Ukoloni,
Kwaheri Uhuru kilichoandikwa na Harith Ghassany ambacho kinaonyesha jinsi
ambavyo viongozi hao wa SMZ waliuawa na kuzikwa katika kaburi moja.
“Sisi wa kizazi cha Muungano tunataka kujua ukweli juu ya makosa
waliyoyafanya hawa waasisi wa Muungano hadi wakauawa na kuzikwa katika kaburi
au handaki moja,” alisema Lissu.
Jitihada za kumpata Makamu wa Pili wa Rais wa SMZ, Balozi Seif
Ali Idd na Waziri wa Nchi katika ofisi yake, Mohamed Abood kuzungumzia msimamo
wa SMZ kuhusu kauli hiyo hazikuzaa matunda kwa kuwa simu zao ziliita bila
majibu.
Akizungumzia suala hilo, mbunge wa viti maalumu, Anna Abdallah
alisema naye alidai hoja hizo za Lissu ni za uchochezi ambao usipopuuzwa,
unaweza kusababisha chuki kwa jamii.
“Ule ulikuwa ni uchochezi, na upinzani wa aina hiyo ni wa ajabu
sana… kwa mtazamo wake yeye anafikiri anawafurahisha Wazanzibari, lakini
wamemuona ni mtu wa ajabu,” alisema mwanasiasa huyo mkongwe.
Pamoja na uzito wa tuhuma hizo, baadhi ya wabunge waliohojiwa na
gazeti hili jana walionekana kuzungumza kimkakati kwamba hawakusikiliza hotuba
hiyo.
Utata mkubwa bado umezunguka kutoweka kwa Hanga na wenzake
machapisho mbalimbali yanawatambua kama watu waliokuwa mstari wa mbele katika
Mapinduzi ya Zanzibar na ambao waliunga mkono Muungano mara baada ya mapinduzi
hayo.
CHANZO, MWANANCHI
No comments:
Post a Comment