Pages

Pages

Pages

Friday 4 November 2016

HAYA NDIYO MAJIBU YA SERIKALI YA HOJA ZA WABUNGE KUHUSU MPANGO WA MAENDELEO WA TAIFA NA MWONGOZO WA BAJETI YA SERIKALI KWA MWAKA 2017/2018

Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Philip Mpango (Mb) (Kulia wanaoshuka ngazi), akizungumza jambo na Mbunge wa Kasulu Mjini, Mhe. Daniel Nsanzugwanko, baada ya kumalizika kwa mjadala wa mchana kuhusu Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2017/2018 na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2017/2018, Bungeni Mjini Dodoma.


Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Philip Mpango (MB), (kushoto), akijibu hoja mbalimbali za Waheshimiwa wabunge kuhusu Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2017/2018 na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2017/2018, Bungeni Mjini Dodoma.

Baadhi ya Wabunge wakiwapongeza Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Philip Mpango (Mb) (Kulia) na Naibu Waziri wake Mhe. Dkt Ashatu Kijaji (Mb) (Katikati), baada ya kujibu hoja mbalimbali za Waheshimiwa wabunge kuhusu Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka 2017/2018 na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2017/2018, Bungeni Mjini Dodoma.
Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Philip Mpango (Mb), akimpongeza Naibu Waziri wake, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji, baada ya kuwasilisha kwa umahili mkubwa majibu ya serikali kutokana na hoja mbalimbali zilizotolewa na wabunge wakati wa kujadili Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka 2017/2018 na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka  2017/2018, Bungeni Mjini Dodoma.
 Naibu Waziri wa Wizara ya Fedha na Mipango, Mhe. Dkt Ashatu Kijaji (Mb), akizungumza na Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango Bibi Florence Mwanri (kulia) pamoja na maafisa wengine waandamizi wa Tume hiyo baada ya kuwasilishwa kwa majibu ya hoja mbalimbali za Waheshimiwa Wabunge kuhusu Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka 2017/2018 na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2017/2018, Bungeni Mjini Dodoma.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bibi Dorothy Mwanyika, akifurahia jambo na Kamishna wa Bajeti wa Wizara hiyo, Bw. John Cheyo, baada ya kujibiwa kwa hoja mbalimbali za Waheshimiwa Wabunge kuhusu Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2017/2018 na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka  2017/2018, Bungeni Mjini Dodoma.

Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Philip Mpango (MB), (kushoto), akipongezwa na Mbunge wa Liwale, George Huruma Mkuchika, baada ya Waziri huyo kujibu hoja mbalimbali za Waheshimiwa wabunge kuhusu Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2017/2018 na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka  2017/2018, Bungeni Mjini Dodoma.
Baadhi ya Maafisa waandamizi wa Wizara ya Fedha na Mipango pamoja na Tume ya Mipango, wakiwa katika picha ya pamoja baada ya Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Philip Mpango (MB), na Naibu waziri wake Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) kujibu hoja mbalimbali za Waheshimiwa Wabunge kuhusu Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2017/2018 na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka  2017/2018, Bungeni Mjini Dodoma.
Kamisha wa Bajeti kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. John Cheyo (kulia), akibadilishana mawazo na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Profesa Joyce Ndalichako (katikati) na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Susan Kolimba, nje ya ukumbi wa Bunge baada ya Serikali kupitia Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango (Mb) na Naibu Waziri wake Mhe. Dkt Ashatu Kijaji (Mb), kujibu hoja mbalimbali za Waheshimiwa wabunge kuhusu Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2017/2018 na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2017/2018, Bungeni Mjini Dodoma.

 (Picha zote na Benny Mwaipaja-Wizara ya Fedha na Mipango)


JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
  
UFAFANUZI WA HOJA ZA WAHESHIMIWA WABUNGE WAKICHANGIA HOTUBA YA WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO, MHE. DKT. PHILIP I. MPANGO (MB), AKIWASILISHA BUNGENI MAPENDEKEZO YA MPANGO WA MAENDELEO WA TAIFA
KWA MWAKA 2017/18 NA MWONGOZO WA KUANDAA
MPANGO NA BAJETI YA SERIKALI KWA
MWAKA 2017/18
  
DODOMA                                                   NOVEMBA, 2016

A.          UTANGULIZI

1.           Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii kukushukuru wewe binafsi, Naibu Spika na Wenyeviti wa Bunge kwa kuendesha majadiliano kwa ufanisi kuhusu Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti kwa Mwaka 2017/18.

2.           Mheshimiwa Spika, napenda kutambua mchango mzuri uliotolewa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, chini ya Mwenyekiti wake Mhe. Hawa Abdulrahman Ghasia, Mbunge wa Mtwara Vijijini na Makamu Mwenyekiti, Mhe. Josephat Sinkamba Kandege, Mbunge wa Kalambo. Ninatambua pia mchango wa waziri kivuli na msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kuhusu wizara ya Fedha na Mipango, Mhe. Halima James Mdee, Mbunge wa Kawe. Aidha, ninawashukuru kwa dhati Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia mjadala huu kwa kuzungumza (45) na kwa maandishi (30).

3.           Mheshimiwa Spika, kwa ujumla mjadala ulikuwa mzuri, baadhi ya maoni yakitolewa kwa hisia kali. Mimi naamini kwamba kwa kuzingatia umuhimu wa uchumi katika nchi ni jambo jema tukachambua, tukabishana na hatimaye turidhiane juu ya vipaumbele, mikakati na hatua stahiki za kukuz auchumi kwa namna endelevu zitakazowezesha kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025.

4.           Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia kuwa tumepokea michango na hoja nyingi sana kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge, naomba niahidi hapa kuwa nitawasilisha Bungeni taarifa ya maandishi inayofafanua hoja zote zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge.

B.          MAONI NA USHAURI ULIOSISITIZWA NA WAHESHIMIWA WABUNGE WENGI

5.           Mheshimiwa Spika, yapo maoni/ushauri mbalimbali uliotolewa na Waheshimiwa Wabunge ambayo Serikali itazingatia katika kuandaa Mpango wa Maendeleo  na Bajeti kwa Mwaka 2017/18. Ushauri huo ni:-
   (i)        Serikali ijielekeze kubuni vyanzo vingine vya mapato (Non-tax revenue) vitakavyosaidia kugharamia Bajeti ya Serikali;
  (ii)        Serikali ipunguze kukopa zaidi kutoka vyanzo vya ndani;
(iii)        Kukamilisha haraka zoezi la Sovereign Rating ili kuwezesha kukopa kutoka vyanzo vya nje;
(iv)        Ujenzi wa Reli ya Kati kutoka Dar – Tabora - Kigoma (km 1,251) kwa Standard Gauge na matawi yake;
  (v)        TRA iandae mapema awamu ya pili ya ukusanyaji wa kodi ya majengo katika halmashuri na miji midogo iliyosalia;
(vi)        Kutenga fedha za kutosha za matumizi mengineyo (OC) kwa mafungu husika ili kuweza kugharamia mpango wa Serikali kuhamia Makao Makuu – Dodoma hususan kwa upande wa malipo ya stahili za watumishi watakaohamishwa;
(vii)        Kukamilisha mifumo ya ukusanyaji wa mapato ya Serikali kwa njia za kielektroniki;
(viii)        Kuhamasisha na kuongeza matumizi ya mashine za EFD na wananchi kwa ujumla kudai risiti  halali pale wanaponunua bidhaa;
(ix)        Kudhibiti mianya ya upotevu wa mapato hususan bandari bubu na biashara za magendo;
  (x)        Kuboresha mazingira ya kufanya biashara na uwekezaji ili kuiwezesha sekta binafsi kutoa mchango unaostahili katika kukuza uchumi wa nchi yetu;
(xi)        Kuweka mkakati wa kujenga zahanati katika kila kijiji na kituo cha afya kwa kila kata na kuimarisha upatikanaji wa madawa na vifaa tiba,
(xii)        Kukamilisha utaratibu wa matumizi ya shilingi milioni 50 kwa kila kijiji/mtaa/shehia na kuongeza kiasi kinachotengwa;
(xiii)        Kuendeleza maeneo ya viwanda vidogo, na EPZ/SEZ;
(xiv)        Kutoa kipaumbele kwa miradi ya makaa ya mawe - Mchuchuma na chuma Liganga;
(xv)        Kuboresha elimu ya juu na kuongeza wigo wa utoaji wa mikopo kwa wanafunzi; na
(xvi)        Kuendelea kuboresha miundombinu ya barabara.





C.          UFAFANUZI WA HOJA MBALIMBALI

Hoja Na. 1: Uchumi una hali mbaya (Umedorora) na kuna manung’uniko mengi ya wananchi mtaani.

Hali ya Uchumi (Januari – Juni 2016)
·        Ukuaji wa Pato la Taifa: 6.7% (Jan-Jun 2016) Vs 5.8% (Jan-Jun 2015).

·        Sekta zilizokua zaidi: uchukuzi, uhifadhi wa mizigo (17.4%), uchimbaji wa madini na gesi (13.7%), mawasiliano (13.0%) na sekta ya fedha & bima (13.0%).

·        mfumuko wa bei: 6.5% (Jan 2016), 5.5% (Jun 2016) na 4.5% (Sept 2016).

·        Akiba ya fedha za kigeni: 4 months of imports cover (USD 4.1 bn) Sept 2016

·        Urari wa Biashara ya Nje: current account deficit USD 601.8 (Jan – Sept 2016)  Vs USD 1,207.7 (Jan – Sept 2015)

Mwenendo wa sekta ya kibenki (Januari – Septemba 2016).
·        Sekta imeendelea kukua na ina mitaji na ukwasi wa kutosha.

a)   Mitaji ikilinganishwa na mali iliyowekezwa (Total Capital to Total Risk Weighted Assets and Off-balance Sheet Exposures) ni 19.08% Vs kiwango cha chini kinachotakiwa 12.0%.
b)   Mali inayoweza kubadilishwa kuwa fedha taslimu ikilinganishwa na kiwango cha amana zinazoweza kuhitajika katika muda mfupi (liquid assets to demand liabilities) 34.18% Vs  kiwango cha chini kinachohitajika 20%.

But: mikopo chechefu imeongezeka (6.7% Sept 2015, 9.1%  Sept 2016)

Mabenki yaliyopata Hasara Jul – Sept 2016: CRDB & TIB Development Bank.
Sababu: mikopo chechefu (provision for loan losses);
Twiga Bancorp imewekwa chini ya uangalizi wa BOT;
NB: Crane Bank Ltd ya Uganda imewekwa chini ya usimamizi wa Benki Kuu Oct 2016; Imperial Bank Kenya, Oct 2015
Benki nyingi incl. CRDB na TIB Devt, zimekuwa na mitaji na ukwasi wa kutosha. Matarajio ni kuwa benki hizi zitafanya vizuri katika kipindi kilchobaki cha 2016/17.

Kwa mwaka ulioshia Sept 2016 Sekta ya Kibenki kwa ujumla ilipata faida: pato kwa rasilimali (Return on Assets) 2.53%; pato kwa mtaji (Return on Equity) 12.05%. Mtaji na kiwango cha mali inayoweza kubadilishwa kuwa fedha taslimu Vs amana zinazoweza kuhitajika katika muda mfupi (liquid assets to demand liabilities) viliendelea kuwa juu ya viwango vinavyotakiwa.

Riba za mikpo zimepungua: 16.18% Sept 2015 – 15.83% Sept 2016
Riba za amana zilibakia wastani wa 9.0%;
Tofauti kati ya riba za mikopo na amana za mwaka mmoja ilipungua 1.77% pts (Sept 2016) kutoka 3.32 % pts (Sept 2015);
Mwenendo huu umeimarisha mazingira ya kufanya biashara na ushindani.

Viwango vya Ubadilishaji fedha
Hatua za kuimarisha thamani ya Shilingi:
   (i)        kuongeza mauzo ya bidhaa nje;
  (ii)        kuimarisha uzalishaji wa nishati; na
(iii)        kupunguza matumizi ya fedha za kigeni yasiyo na tija.

Wastani wa Shs. 2,172.38: USD 1 (Jan 2016), Shs. 2,180.54 (Jul 2016); Shs. 2,188.1: USD 1 (Sept 2016)







MWENENDO WA BAJETI YA SERIKALI


Ulipaji wa Madeni ya Ndani
6.           Mheshmiwa Spika, Katika kipindi cha Julai hadi Oktoba 2016 Serikali imelipa madeni mbalimbali yaliyohakikiwa na Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali yenye jumla ya shilingi bilioni 187.521. Madeni haya yanajumuisha madeni ya wakandarasi wa barabara, maji, umeme pamoja na wazabuni mbalimbali. Aidha, madeni ya watumishi wa umma yanaendelea kulipwa kupitia mafungu yao.

Ulipaji wa Deni la Nje
7.           Mheshimiwa Spika, Katika kipindi kuanzia Novemba 2015 hadi kufikia Oktoba, 2016 Serikali imetumia jumla ya shilingi bilioni 1,196.9 kwa ajili ya kulipia madeni ya nje. Kati ya kiasi hicho, malipo ya mtaji ni shilingi bilioni 709.7 na malipo ya riba ni shilingi bilioni 487.2. Malipo ya deni la Taifa yamekuwa yakiongezeka mwaka hadi mwaka kutokana na mikopo mipya, kumalizika kwa kipindi cha kabla ya kuanza kulipa mtaji (Grace Period) kwa mikopo ya muda mrefu pamoja na kushuka kwa thamani ya shilingi dhidi ya Dola ya Kimarekani.

8.           Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kulipa kwa wakati mikopo yote ya nje inayoiva kwa mujibu wa mikataba. Kwa kuwa kutofanya hivyo kutahatarisha mahusiano yaliyopo kati yetu na nchi wahisani, taasisi za fedha za kimataifa na mabenki ya nje. Aidha, nchi isipolipa kwa wakati inaweza kushitakiwa kwenye mahakama za kimataifa na kuisababishia nchi hasara na kupelekea kutopata mikopo tena kutoka nje. Kadhalika, kutokulipa kwa wakati kutasababisha Serikali kulipa gharama za ziada (penalty) kulingana na makubaliano na hivyo kuongeza mzigo kwa taifa.
9.           Mheshmiwa Spika, Serikali imejiwekea mikakati mbalimbali ili kuhakikisha kwamba Deni la Taifa linadhibitiwa na linaendelea kuwa himilivu na linalipwa kwa wakati.

Ruzuku ya Pembejeo za Kilimo
10.       Mheshmiwa Spika, Katika mwaka wa fedha 2016/17 jumla ya shilingi bilioni 25.0 zimetengwa kwa ajili ya ununuzi wa pembejeo ambapo hadi kufikia mwezi Oktoba 2016 jumla ya shilingi bilioni 10.0 zimetolewa.
                               
Ununuzi wa Chakula cha Hifadhi ya Taifa
11.       Mheshmiwa Spika, Katika mwaka wa fedha 2016/17 jumla ya shilingi bilioni 15.0 zimetengwa kwa ajili ya ununuzi wa chakula cha hifadhi ya Taifa ambapo hadi kufikia mwezi Oktoba 2016 jumla ya shilingi bilioni 9.0 zimetolewa.

Utoaji wa Fedha za Mfuko wa Jimbo
12.       Mheshmiwa Spika, Katika mwaka wa fedha 2016/17 Serikali imetenga shilingi bilioni 10.4 kwa ajili ya Mfuko wa Kuchochea Maendeleo Jimboni. Kati ya fedha hizo shilingi bilioni 9.0 ni kwa ajili ya Tanzania Bara na shilingi bilioni 1.4 ni kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Serikali inatarajia kutoa fedha hizo mwezi Novemba 2016.

13.       Mheshmiwa Spika, katika nusu ya kwanza ya mwaka 2016, kasi ya ukuaji wa Pato la Taifa imeongezeka na kufikia asilimia 6.7 ikilinganishwa na asilimia 5.8 kwa nusu ya kwanza ya mwaka 2015.

14.       Mheshimiwa Spika, manung’uniko mtaani yapo na kwa kiasi kikubwa yametokana na jitihada na hatua zilizochukuliwa na Serikali kurudisha nchi kwenye utaratibu wa nidhamu ya kazi katika Utumishi wa Umma, kurejesha nidhamu ya matumizi/kuondoa matumizi ya Serikali yasiyo ya lazima, kupambana na wizi/ubadhirifu wa fedha na mali za umma, kuhimiza ulipaji kodi na ukusanyaji wa mapato yasiyo ya kodi n.k. Hata hivyo, Serikali inaamini kuwa hatua hizi ni kwa maslahi mapana ya Taifa na maumivu ni ya kipindi cha mpito cha kuweka mambo sawa/kurejesha mifumo kwenye utaratibu unaokubalika na endelevu.  “There is no game without pain”.

15.       Mheshimiwa Spika, upo utaratibu wa Serikali, Taasisi binafsi na Mashirika ya Kimataifa kufanya tathmini ya uchumi wa nchi na kutoa maoni yao juu ya kile walichokiona. Shirika la Fedha la Kiamtaifa – IMF ambalo lilikuwa hapa wiki moja iliyopita, limekamilisha tathmini ya mwenendo wa uchumi wa nchi yetu ambapo kiujumla wameridhika na hali ya uchumi wa Tanzania.

Hoja Na. 2: Misingi ya Mpango (premises) iliyowekwa inatujengea kushindwa.

16.       Mheshimiwa Spika, neno ‘Misingi’  katika Mapendekezo ya Mpango lililenga kumaanisha “assumptions”.  Hakika Serikali inajua kwamba hali halisi ya mazingia wezeshi kwa uwekezaji nchini na nafasi ya Tanzania kama ilivyotathminiwa na Benki ya Dunia katika Doing Business report.  Serikali inajua utabiri wa hali ya hewa na maoteo ya upungufu wa chakula n.k.  We are not naïve.  Assumptions si lazima ziwe halisi bali ziliwekwa hapa kurahisisha uwekaji wa malengo kwa mwaka 2017/18.  Utaratibu huu ni wa kawaida kabisa kwa wachumi.  Mathalani tunapotaka kuchambua biashara baina ya mataifa tunaweka assumption kwamba dunia ina nchi 2 tu zinafanya biashara ili kurahisisha uchambuzi japo kila mtu anafahamu dunia ina nchi nyingi zinafanya biashara baina yao.

Hoja na 3: Fedha kutopelekwa kwenye Halmashauri kwa wakati

17.       Mheshmiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2016/17 Mamlaka za Serikali za Mitaa ziliidhinishiwa bajeti ya shilingi bilioni 5,434.7. Kati ya kiasi hicho shilingi bilioni 3,593.9 ni kwa ajili ya mishahara, shilingi bilioni 598.2 ni kwa ajili ya matumizi mengineyo (OC) ikijumuisha shilingi bilioni 266.2 za mapato yatokanayo na vyanzo vya ndani vya Halmashauri  na shilingi bilioni 332.0 ni ruzuku kutoka Serikali Kuu. Aidha, shilingi bilioni 1,242.6 ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo ambapo shilingi bilioni 588.5 ni fedha za nje na shilingi bilioni 654.1 ni fedha za ndani ikijumuisha shilingi bilioni 399.2 zinazotokana na mapato ya ndani ya Halmashauri na shilingi bilioni 254.9 ni ruzuku kutoka Serikali Kuu.

18.       Mheshmiwa Spika, katika kipindi cha Julai hadi Oktoba 2016, fedha zilizotolewa zinajumuisha mishahara shilingi bilioni 1,181.0 sawa na asilimia 33, matumizi mengineyo shilingi bilioni 192.8 sawa na asilimia 32.2 na fedha za maendeleo shilingi bilioni 177.3 sawa na asilimia 14.3. Aidha, mbali na fedha za ruzuku kutoka Serikali Kuu na makusanyo ya ndani ya Halmashauri kiasi cha shilingi bilioni 271 zilitumika kutekeleza miradi ya maji vijijini (shilingi bilioni 51.1), umeme vijijini (shilingi bilioni 132.4), Mfuko wa barabara (shilingi bilioni 78.1) na utoaji wa pembejeo kwa wakulima (shilingi bilioni 10.0) katika Halmashauri mbalimbali nchini.

Hoja Na. 4: Mradi wa Mchuchuma na Liganga uko kwenye Mpango wa maendeleo kila mwaka lakini utekelezaji wake haujaanza

19.       Mheshimiwa Spika, Sio kweli kuwa utekelezaji wa Mradi wa Makaa ya Mawe, Mchuchuma na Chuma Liganga haujaanza. Utekelezaji wa mradi huu utakaogharimu Dola za Marekani bilioni 3 umeanza na kufikia hatua mbalimbali ikiwa ni pamoja na:
·        Kukamilika kwa upembuzi yakinifu wa mradi ikiwa ni pamoja na kutambua kiasi cha mashapo ya makaa ya mawe na chuma, usanifu wa migodi na kiwanda cha chuma na kituo cha kuzalisha umeme;
·        kupatikana kwa leseni za uchimbaji na matumizi ya madini, leseni ya matumizi ya maji na leseni ya uzingativu wa mazingira;
·        Kukamilika pia kwa mkakati wa ushirikishi wa wananchi wanaouzunguka mradi na njia ya kusafirishia umeme;
·        Kukamilika kwa ujenzi barabara kwa kiwango cha changarawe ili kuruhusu usafirishaji wa mitambo kwenda kwenye eneo la mradi;
·        kuendelea na usanifu wa ujenzi wa reli ya liganga hadi Mtwara na uwezekano wa kuiunganisha na reli ya TAZARA na kuendelea na usanifu katika bandari ya Mtwara; na
·        kukamilika kwa tathmini ya fidia kwa wananchi watakaopisha eneo la mradi imekamilika.

Hoja Na. 5: Utaratibu wa Taasisi za Umma kuweka fedha zao katika Mabenki ya kibiashara urejeshwe ili kuwezesha mabenki kukopesha fedha hizo kwa wafanyabishara na pia kuziwezesha Taasisi hizo kunufaika na riba zitokanazo na amana.

20.       Mheshimiwa Spika, uamuzi wa Serikali kuzitaka taasisi za umma kufungua akaunti ya mapato Benki Kuu utaendelea kubaki kama ulivyo. Utaratibu uliokuwa umejengeka ulizinufaisha benki chache na haukuwa na maslahi mapana kwa Taifa. Benki hizo zimekuwa zikipata faida  kwa kutumia migongo ya maskini na hivyo sasa basi! Benki zifanye kazi kwa kurejesha ushindani.
Mfano:
Taasisi moja ilikuwa na amana za muda maalum (fixed deposit) za shilingi bilioni 440 ambazo ziliwekwa katika baadhi ya benki. Kiasi hiki kilizaa faida ya shilingi bilioni 17 ambayo inamaanisha riba ya wastani wa asilimia 4 kwa mwaka. Ijapokuwa ukweli ni kwamba, amana za chini ya shilingi milioni 100 zinakuwa na riba ya kati ya asilimia 8 na 10 na kiasi cha amana kinapokuwa kikubwa zaidi riba inaongezeka hadi kufikia asilimia 15. Kama riba ingekuwa asilimia 13, taasisi hiyo ingepata faida ya bilioni 57.2 kabla ya kodi. Hivyo, kwa taasisi hiyo moja tu, watanzania wamekuwa wakiibiwa shilingi bilioni 40 kila mwaka.

Si hivyo tu, fedha hizo (bilioni 440) zilizokuwa katika benki za biashara zilitumika kuikopesha Serikali kupitia hati fungani kwa riba ya asilimia 15, hivyo wananchi hulipa benki hizi riba ya hadi shilingi bilioni 66 kwa fedha ambazo ni za kwao wenyewe. Maana yake ni kuwa, wananchi waliendelea kulipa riba kwa fedha zao wenyewe sawa na hasara ya shilingi bilioni 106 kwa mwaka. Hatuwezi kuendelea na utaratibu huu.

Benki na baadhi ya watanzania waliozoea  kupiga dili sasa basi! Benki ambazo zimekuwa zikipata faida  kwa kutumia migongo ya maskini sasa basi! Benki zifanye kazi kurejesha ushindani. Mheshimiwa Rais alisema hadharani na ukweli utabaki hivyo, kwamba hizo fedha hazitarudi.
Hoja Na. 6: Serikali ielekeze benki kushusha riba kutoka asilimia 18 hdi 13 kwa wafanyabiashara wadogo na wakubwa ili kuongeza mzunguko wa fedha katika uchumi. (Riba za mikopo bado ziko juu, Serikali ielekeze benki kushusha riba hizo)

21.       Mheshimiwa Spika, Ni kweli riba za mikopo ni kubwa hasa zile zinazotozwa na Taasisi ndogondogo za fedha (microfinance). Katika Sekta ya Huduma Ndogo Ndogo za Fedha (Microfinance) kuna benki, taasisi na asasi za fedha zilizo rasmi na zisizo rasmi ambazo zinatoa huduma za kifedha kwa wateja wadogo wadogo. Pia kuna taasisi na asasi za kifedha ambazo zinatoa huduma za mikopo kwa kutumia mitaji binafsi bila kukusanya na kupokea amana za wateja.

22.       Mheshimiwa Spika, Taasisi na asasi hizo zimeongezeka kwa kiasi kikubwa na zimekuwa sehemu muhimu ya maendeleo ya ujasiriamali na ukuaji wa uchumi wa wananchi na mikopo ya taasisi hizo kwa kiasi kikubwa inategemewa na watanzania walio wengi.

23.       Mheshimiwa Spika, Taasisi na asasi hizo zinapata leseni kutoka katika mamlaka tofauti ikiwemo BRELA, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, RITA, na Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji. Utaratibu huo umesababisha usimamizi na ufuatiliaji wa taasisi hizo kuwa mgumu. Kutokana na hali hii zimejitokeza changamoto nyingi na mapungufu kadhaa katika sekta ya “Microfinance”, ikiwa ni pamoja na kutozwa riba kubwa na kuwa na mikataba yenye mapungufu mengi. Hii inatokana na wakopeshaji kwenye sekta hii kutokuwa na usimamizi imara na elimu ndogo ya maswala ya fedha kwa wateja walio wengi (financial illiteracy).

24.       Mheshimiwa Spika, Serikali inakiri kuwepo na malalamiko kwa wananchi wengi nchini kuhusiana na uendeshaji wa biashara inayofanywa na asasi hizo kama vile viwango vya juu vya riba na ada pamoja na utaratibu mbaya wa ukusanyaji wa marejesho (loan repayment). Hali hii inatokana na ukweli kwamba hakuna mamlaka rasmi na halali ya kisheria yenye wajibu wa kutoa leseni, kuratibu, kusimamia na kuhakikisha ulinzi wa wateja (consumer protection) katika taasisi hizi za fedha.

25.       Mheshimiwa Spika, Katika kutatua mapungufu na changamoto hizi na kwa kuzingatia maendeleo yaliyojitokeza katika huduma za fedha kwa wateja wadogo wadogo, Serikali imekamilisha na kuidhinisha Sera ya Taifa ya ‘Microfinance’ na hatua za ukamilishaji wa sheria ya Microfinance zinaendelea.

26.       Mheshimiwa Spika, Sheria hiyo itaunda mfumo mahususi wa kusimamia na kuratibu shughuli za taasisi na asasi za fedha zilizo na zisizo rasmi ambazo zinatoa huduma za kifedha kwa wateja wadogo wadogo ambazo haziko chini ya Sheria ya Mabenki na Taasisi za Fedha ya mwaka 2006.

27.       Mheshimiwa Spika, Kwa upande mwingine, benki na taasisi za fedha zinazosimamiwa kisheria na Benki Kuu ya Tanzania, zimeendelea kuwa na viwango bora vya riba katika kipindi cha mwaka ulioishia mwezi Septemba 2016.

28.       Mheshimiwa Spika, kuhusu kuweka riba elekezi, uzoefu wa nchi nyingi unaonesha kwamba viwango vya riba huamuliwa na nguvu ya soko. Ni dhamira ya Serikali kuona riba za benki zinazotozwa katika mikopo zinapungu. Hivyo, Serikali itaendelea kuweka mazingira mazuri yatakayosaidia kuleta ushindani utakaopelekea viwango vya riba hizo kuwa nafuu zaidi. Aidha, ikumbukwe kwamba kuna madhara ya kuweka viwango elekezi vya riba ikiwa ni pamoja na uwezekano wa benki kupunguza mikopo kwa sekta binafsi ikiwa kiwango hicho elekezi kitakuwa chini zaidi ya riba ya dhamana na hati fungani za serikali; kuongezeka kwa mikopo chechefu na kupungua kwa ushindani katika sekta ya benki na ufanisi katika utekelezaji wa sera ya fedha.

Hoja Na. 7: TRA wanatumia vitisho, mabavu na mifumo kandamizi katika  kukusanya kodi

29.       Mheshimiwa spika, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inaendelea na jitihada za kuhakikisha kila anayestahili kulipa kodi analipa kodi stahiki na kwa wakati. TRA inatekeleza majukumu yake kwa weledi na ufanisi kulingana na taratibu zilizoainishwa katika sheria na kanuni za kodi.

30.       Mheshimiwa spika, mlipakodi anakadiriwa kodi ya kulipa na kupewa muda wa kuilipa kodi hiyo. Endapo kodi hiyo itakukuwa haijalipwa katika muda ulioonyeshwa kwenye taarifa ya madai (Notice of Assesment), TRA huchukua jukumu la kumkumbusha mhusika (reminder notice) na kumtahadharisha hatua zitakazochukuliwa endapo kodi hiyo itaendelea kutolipwa mpaka tarehe iliyooneshwa kwenye reminder notice. Hatua zinazochukuliwa kwa mlipa kodi aliyekaidi ni kama vile: kukamatwa mali zake na kuuzwa kwa njia ya mnada; na kuiagiza benki ya mlipa kodi kuhamisha fedha kutoka kwenye akaunti yake kwenda TRA ili kulipia deni hilo. Hatua hizi zipo kwa mujibu wa sheria na si vitisho, mabavu wala mifumo kandamizi kwa wafanyabiashara. Ni vizuri walipakodi wakazingatia sheria na kulipa kodi kwa hiari ili kuepuka usumbufu.

Hoja Na. 8: Serikali inasema kuwa imeokoa shilingi bilioni 19 kwa kuondoa watumishi hewa kwenye mfumo wa maliopo. Taarifa ya gharama za watumishi ya Benki Kuu ya Juni 2015 ilionyesha  malipo ya mishahara yaliongezeka kutoka bilioni 456 hadi shilingi bilioni 534 Juni 2016 ambalo ni ongezeko la bilioni 78. Ongezeko hili limetoka wapi wakati Serikali imesimamisha ajira mpya na kuondoa watumishi hewa?

31.       Mheshimiwa spika, Zoezi la kufuta watumishi hewa kufuatia agizo la Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilianza Mwezi Machi, 2016. Hata hivyo, pamoja na kufutwa kwa watumishi hewa malipo ya mishahara katika kipindi   cha Juni 2015 hadi Juni 2016 yameongezeko kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo:
·        Nyongeza ya mishahara iliyoanza kutumika Julai, 2015 ambapo jumla ya Shilingi bilioni 59 ziliongezeka kwa mwezi;
·        Watumishi 25,517 waliajiriwa katika kipindi hicho wenye mshahara wa Shilingi bilioni 16.4 kwa mwezi;
·        Uwianishaji wa mishahara ya watumishi wa Vyuo Vikuu ambapo jumla ya Shilingi bilioni 2.9 ziliongezeka;
·        Ongezeko la posho zinazoambatana na mishahara shilingi bilioni 6.1 kwa mwezi kwa vyombo vya ulinzi na usalama;
·        Upandishwaji vyeo kwa watumishi mbalimbali; na
·        Uwianishaji wa maeneo ya kimishahara ambapo kuanzia mwezi Februari, 2016 mishahara ya shilingi bilioni 33 iliyokuwa inalipwa kupitia kwenye kasma ya matumizi mengineyo ilianza kulipwa kupitia kwenye kasma ya mishahara.

32.       Mheshimiwa spika, Hivyo, endapo watumishi hewa wasingeondolewa matumizi ya Serikali katika eneo la mishahara yangekewa makubwa zaidi ya kiasi hicho kilicholipwa mwezi Juni, 2016.

Hoja Na. 9: Riba kubwa zinazotozwa na mabenki ni kandamizi na  zinaumiza wanyonge

33.       Mheshimiwa spika, Katika mwaka ulioshia mwezi Septemba 2016, riba za mikopo za mabenki zimekuwa zikipungua wakati zile za amana kuimarika kwa viwango tofauti. Riba za mikopo zilipungua hadi kufikia wastani wa asilimia 15.83 mwezi Septemba 2016 kutoka asilimia 16.18 mwezi Septemba 2015. Wakati huo huo, riba za amana zilibakia katika kiwango cha wastani wa asilimia 9.0. Aidha, riba za mikopo ya mwaka mmoja ilipungua kutoka wastani wa asilimia 14.27 hadi asilimia 13.23, wakati riba za amana za mwaka mmoja ziliongezeka kutoka asilimia 10.95 hadi asilimia 11.46. Hali hii ilifanya tofauti kati ya riba za mikopo na amana za mwaka mmoja ipungue hadi kufikia wastani wa asilimia 1.77 mwezi Septemba 2016 kutoka asilimia 3.32 mwezi Septemba 2015. Mwenendo huu wa viwango vya riba unaonesha kuendelea kuimarika kwa mazingira ya kufanya biashara na ushindani nchini hivyo kuvutia zaidi uwekezaji wa sekta binafsi. Aidha, hii inaashiria kuimarika kwa ushindani wa Mabenki ili kuvutia wateja.





MAJIBU YA HOJA ZA WAHESHIMIWA WABUNGE WAKATI WA KUJADILI MAPENDEKEZO YA MPANGO WA MAENDELEO WA TAIFA KWA MWAKA 2017/18 NA MWONGOZO WA KUANDAA MPANGO NA BAJETI YA SERIKALI KWA MWAKA 2017/18

NA.
MTOA HOJA
HOJA
UFAFANUZI WA HOJA

KAMBI RASMI YA UPINZANI BUNGENI
1.    

TRA inavuka lengo kutokana na kukusanya maduhuli na kuyahesabu kama sehemu ya mapato ya kodi.
Maelezo yaliyotolewa na Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni siyo sahihi.

Maelezo sahihi ni kuwa mapato ya kodi yanayokusanywa na TRA hutolewa taarifa peke yake. Mapato yasiyo ya kodi (maduhuli) kwa Mashirika ya Umma na Taasisi za Serikali yanayokusanywa na Taasisi husika na kutolewa taarifa na Msajili wa Hazina. Mapato yanayokusanywa na Wizara hutolewa taarifa na Wizara husika.

WAHESHIMIWA WABUNGE
2.    
Mhe. Josephat Sinkamba Kandege
Pamoja na lengo zuri la kuongeza mapato ya ndani ili ku kugharamia sehemu kubwa ya bajeti, Serikali ihakikishe kuwa vyanzo vipya vya kodi vinavyopendekezwa katika  bajeti ya mwaka wa Fedha 2017/18 havitakuwa  kero kwa  wafanyabiashara na wananchi wote kwa ujumla.
·        Serikali inaendelea kutekeleza azma yake ya kupunguza kodi zinazoleta kero kwa wananchi na kuharibu mpango mkakati wa Serikali kuchochea ari ya ulipaji kodi kwa hiari. 
·        Aidha, Serikali imejikita katika kuimarisha mkakati wa kuboresha usimamizi na utawala wa kodi ili wafanyabiashara na wananchi  waweze kulipa kodi zilizopo kwa hiari kwa maendeleo ya taifa lao.
3.    
Mhe. Ahmed Ally Salum
Mabenki yanapata hasara kutokana na kupungua mzunguko wa fedha. Serikali ichukue hatua kwani endapo mabenki yatafungwa kutakuwa na athari katika uchumi wa nchi
·        Katika kipindi cha Julai hadi Septemba 2016, baadhi ya mabenki ya biashara yalipata faida ndogo na baadhi zilipata hasara ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka uliotangulia. Hali hii imeathiri kasi ya utoaji mikopo na hivyo kupunguza mzunguko wa fedha. Miongoni mwa sababu zilizochangia hali hiyo ni pamoja na Serikali kubaini watumishi hewa ambao miongoni mwao walikopa kwenye mabenki na hivyo kusababisha kuwepo kwa mikopo chechefu; serikali kuhamisha fedha za mashirika ya umma kutoka katika mabenki ambazo zilikuwa zinatumika kukopeshea; na hatua ya serikali ya kubana matumizi yasiyo ya lazima kama vile kufanya mikutano katika mahoteli. Aidha, fedha zilizotumika kugaramia mikopo chechefu (provision for loan losses) zilipelekea baadhi ya benki kupata hasara na nyingine kupata faida kidogo.

·        Hata hivyo, hali hii ni ya mpito na Serikali inashauri mabenki ya biashara kubuni mikakati ya kuongeza amana zao ili kuongeza uwezo wa kukopesha. Aidha, mabenki ya biashara yanatakiwa kuendelea kutumia mfumo wa upashanaji taarifa za wakopaji (Credit Reference System) ili kupunguza uwezekano wa kuongezeka kwa mikopo chechefu.


HITIMISHO

34.       Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia na kutupatia ushauri kuhusu  vipaumbele na mambo muhimu ya kuzingatia katika kazi inayofuata ya kuandaa Mpango na Bajeti ya Mwaka 2017/18.

35.       Mheshimiwa Spika, napenda niliahidi Bunge lako Tukufu kwamba, Serikali itazingatia ushauri tuliopokea kwa kadri inavyowezekana. Hakika haitawezekana kuzingatia kila kitu kilichosemwa hapa. Baadhi yataendelea kuzingatiwa katika mipango ya maendeleo itakayofuata. Ili Bunge lione wazi kwamba Serikali inasikia na inathamini ushauri mzuri wa Waheshimiwa Wabunge, inakusudia kuweka bayana katika kitabu cha Mpango utakapokamilika muhtasari wa ushauri uliozingatiwa, na ule tunaoona unafaa uzingatiwe katika mipango itakayofuata na yale ambayo bado yanahitaji kuchambuliwa kwa kina kabla ya kuzingatiwa kwenye mipango.

36.       Mheshimiwa Spika, Serikali ya awamu ya Tano imedhamiria  kujenga Tanzania mpya ili kuwaondoa watanzania kwenye lindi la umaskini haraka. Uamuzi huu unahitaji kuachana na mazoea, unahitaji sacrifice na unahitaji tufanye kazi kwa bidii, nidhamu na uadilifu. Tunataka uchumi ambao wananchi wengi wananufaika nao. Nirudie tena, Serikali ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli inajali wafanyabiashara lakini budi sheria za nchi zizingatiwe.

37.       Mhe. Spika, naomba kutoa hoja.

No comments:

Post a Comment