Pages

Pages

Pages

Thursday 11 August 2016

SERIKALI ZA TANZANIA NA UTURUKI ZASHIRIKIANA KUPATA TAARIFA KUHUSU SHULE ZA FEZA




Na Abushehe Nondo na Immaculate Makilika - MAELEZO
Dar es Salaam
11.8.2016
Serikali imesema kwamba inaendelea kushirikiana na Serikali ya Uturuki ili kupata taarifa zaidi kuhusu wamiliki wa shule za Feza kuhusishwa na jaribio la kuipindua serikali ya Uturuki kama ambavyo imeripotiwa na  baadhi ya vyombo vya habari.
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam Waziri wa Mambo ya nje na ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Augustine Mahiga alisema  wanaendelea kuwasiliana na Serikali ya Uturuki kuhusu taarifa hizo ili kupata ukweli.

Balozi Mahiga alisema kuwa kumekuwepo na taarifa zinazohusisha wamiliki wa shule hizo na baadhi ya wafanyabiashara ambao  walifadhili na kuongoza jaribio la mapinduzi lililoshindwa Julai 15, mwaka huu nchini humo.
“ Serikali  inaendelea kufanya mawasiliano na Serikali ya Uturuki kupitia ubalozi wake hapa nchini ili tuweze kupata taarifa kuhusu kuhusishwa kwa wamiliki wa shule za Feza na baadhi ya wafanyabiashara katika jaribio la kuipindua serikali ya uturuki,”  alisema Balozi Mahiga.
Aliongeza kuwa  kwa sasa serikali ya Tanzania haiwezi kufanya  uamuzi wowote kuhusu wamiliki wa shule ya Feza na wafanyabiashara wa uturuki waliopo hapa nchini.
Kuhusu wanafunzi wa kitanzania wanaosoma nchini humo, Balozi Mahiga alisema kuwa wamemuagiza afisa ubalozi wa Tanzania  aliyepo Roma nchini Italia  kufuatilia hatma ya wanafunzi katika vyuo vilivyopo kwenye miji ya Ankara na Instanbul baada ya  kufungwa kwa shule na vyuo kufuatia jaribio hilo la mapinduzi.
Kwa upande wake, Balozi wa  Uturuki nchini Bw. Yasemin Eralp, hivi karibuni alisema kuwa wanafunzi wa Tanzania wanaosoma nchini mwake  katika vyuo na shule zilizofungwa watahamishiwa vyuo vingine kuendelea na masomo yao.
Balozi Eralp alisema kuwa hatua hiyo imefikiwa  baada ya kufungwa kwa baadhi ya vyuo na taasisi za kielimu zilizobainika kuwa na uhusiano na kikundi cha kigaidi cha Fetullah Terrorist Organization(FTO) kinachotajwa kufadhili na kuongoza jaribio la mapinduzi lililoshindwa hivi karibuni nchini humo.
Hivi karibuni Serikali inatarajia kukutana na balozi wa Uturuki nchini ili kujua ni vyuo vingapi vilivyofungwa nchini humo ikiwa ni pamoja na idadi ya wanafunzi wa kitanzania wanaosoma katika vyuo hivyo ili kupatiwa msaada zaidi.




No comments:

Post a Comment