Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Saturday 14 May 2016

SERIKALI KUTUNGA SERA YA KUSIMAMIA SEKTA NDOGO YA FEDHA NCHINI

NAIBU Waziri, Wizara ya Fedha na Mipango, Dkt. Ashatu Kijaji, ameliambia Bunge Mjini Dodoma, leo tarehe 12 Mei, 2016, kwamba serikali inaandaa sera ya Taifa ya huduma ndogo za fedha ya mwaka 2016, itakayosimamia na kutatua changamoto zinazoikabili sekta hiyo.
Alisema kuwa sera hiyo itawasilishwa mbele ya Baraza la Mawaziri hivi karibuni kabla ya kupelekwa bungeni hatimaye itapatikana sheria ya kusimamia taasisi ndogo za fedha-microfinance Act, 2016.


"Serikali inatambua changamoto ya taasisi binafsi za fedha zinazosumbua wananchi, hivyo sheria hiyo ikitungwa itasaidia kuondoa matatizo hayo" alisisitiza Dkt. Kijaji


Naibu Waziri huyo wa Fedha na Mipango alikuwa akijibu swali lililoulizwa na Mhe. Rahisa Abdalah Musa (Viti maalumu), aliyetaka kujua serikali ilikuwa na mpango gani wa kudhibiti utitiri wa taasisi za fedha pamoja na mabenki ili yalete tija kwa Taifa kwa kuwakopesha wananchi


Akijibu swali la msingi na maswali ya nyongeza yaliyoulizwa na Mhe. Faida Mohamed Bakar (Viti maalumu) aliyetaka kujua mikakati ya serikali ya kuanzisha benki ya wafanyabiashara wakubwa na wadogo ili kuwawezesha kupata huduma bora, Dkt. Ashatu Kijaji alisema kuwa serikali haina mpango wowote wa kufanya hivyo.


Alisema kuwa badala yake serikali inafanya jitihada za kuimarisha benki zake zilizopo ikiwemo Benki ya maendeleo ya Kilimo (TADB) na Benki ya Rasilimali (TIB) ili kukidhi mahitaji ya wafanyabiashara wa kada mbalimbali.


"Serikali imeiboresha kimuundo, Benki ya Rasilimali (TIB) kwa kuunda kampuni tatu zinazofanyakazi kwa kujitegemea lakini kwa ushirikiano wa karibu" alisisitiza Dkt. Kijaji

Alizitaja kampuni hizo kuwa ni TIB Benki ya Maendeleo itakayotoa mikopo ya muda wa kati na mrefu kwa wafanyabiashara wakubwa na wa kati, TIB Benki ya Biashara itakayowahudumia wafanyabiashara wakubwa, wa kati na wadogo na TIB Rasilimali itakayohusika na masuala ya ushauri kwenye Soko la Hisa na Mitaji la Dar es salaam


"Pamoja na mambo mengine, kampuni hii inawajibika kuwashauri wafanyabiashara, hususan wa sekta ndogo ya fedha kupata mitaji kupitia Soko la Hisa la Dar es salaam" aliongeza Dkt. Kijaji


Dkt. Kijaji alisema kuwa pamoja na juhudi za serikali za kuboresha benki hizo, ikiwemo Benki ya Posta, Serikali kupitia Benki Kuu (BOT) inaendelea kuweka mazingira wezeshi ikiwemo kutunga sheria, kanuni na taratibu za kusaidia nguvu za wananchi na sekta binafsi kuanzisha benki au taasisi za fedha katika maeneo yao


"Ni matarajio yetu kuwa wananchi wanatumia fursa ya mazingira mazuri ya uwekezaji yaliyopo nchini kuwekeza wao wenyewe au kuzishawishi benki za biashara kuanzisha huduma za kibenki katika maeneo yao" alisema Dkt. Kijaji


Kuhusu ombi la mbunge huyo kuitaka serikali iingilie kati masuara ya riba zinazotozwa na taasisi za fedha na kuwaumiza wananchi, Dkt. Kijaji alisema kuwa serikali haiwezi kudhibiti wala kuingilia jambo hilo.


Alisema kuwa Serikali ilijitoa katika uendeshaji wa moja kwa moja wa shughuli za kifedha tangu mwaka 1991 ili kuruhusu ushindani huru na kuboresha huduma katika sekta ya fedha hivyo viwango vya riba na mikopo vinavyotozwa na benki hizo na taasisi nyingine za fedha zinapangwa kutokana na nguvu ya soko.


Dkt Kijaji alieleza kuwa katika upangaji wa viwango vya tozo na riba mbalimbali benki na taasisi za fedha huzingatia gharanma za upatikanaji wa fedha, halikadhalika gharama za uendeshaji na sifa alizonazo mkopaji"Alisisitiza Dkt Kijaji





Imetolewa na:


Benny Mwaipaja


Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini


Wizara ya Fedha na Mipango


DODOMA


12/5/2016

No comments:

Post a Comment