JAMHURI
YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA AFYA,
MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO
TAMKO KUHUSU MWENENDO WA UGONJWA WA KIPINDUPINDU
NCHINI PAMOJA NA TAHADHARI YA UGONJWA WA HOMA YA ZIKA, LILILOTOLEWA NA MHE. UMMY
MWALIMU (MB); WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO, TAREHE
8 FEBRUARI 2016
Ndugu Waandishi wa Habari,
Kuhusu
ugonjwa wa kipindupindu, huu ni mwendelezo wa taarifa ya wiki kwa umma, ya mwenendo
wa ugonjwa huu hapa nchini. Hadi kufikia tarehe 7 Februari 2016, jumla ya watu 15325 wameugua ugonjwa huo, na kati yao
watu 238 wamepoteza maisha kwa ugonjwa
huu.
Takwimu
za Kuanzia tarehe 1 hadi 7 Februari 2016, zinaonyesha kuwa idadi ya wagonjwa
walioripotiwa wiki hii imepungua kutoka 459 ya wiki iliyoishia tarehe 31
Januari hadi 258 ambapo ni sawa na punguzo la asilimia 44. Kuna vifo 5, sawa na idadi ya vifo vilivyoripotiwa
katika wiki iliyopita.
Jumla
ya mikoa ambayo imeripoti kuwa na wagonjwa ni 13 ambapo mkoa wa Mara ndio umeongoza kwa kuripoti idadi
kubwa zaidi ya wagonjwa ukilinganishwa na mikoa mingine, ukiwa na wagonjwa 73 (Musoma
Vijijini 33, Musoma mjini 5, Bunda 1, Butiama
13, na Tarime Vijijini 21), ukifuatiwa na mkoa wa Mwanza (70)- (Ukerewe 21, Nyamagana 24, Ilemela 8, Sengerema 5 na
Buchosa 12). Mikoa mingine ni pamoja na Simiyu
(30), Morogoro (26) na Kilimanjaro (16).
wagonjwa
258 na vifo 5 vimeripotiwa. Idadi ya wagonjwa walioripotiwa wiki hii imepungua
ukiliinganisha na idadi ya wiki iliyoishia tarehe 31 Januari ambapo wagonjwa 459 na
vifo 5 viliripotiwa, punguzo hilo ni
sawa na 44%.
Katika
mapambano ya kudhibiti mlipuko huu wa Kipindupindu, kuna changamoto mbalimbali
zilizobainishwa na Wizara yangu kupitia wataalam ambao wanashirikiana na timu
zilizopo katika mikoa na wilaya zilizoathirika. Mojawapo wa changamoto utoaji
wa idadi pungufu ya wagonjwa au kutotoa kabisa taarifa za wagonjwa wa
Kipindupindu. Hii inapelekea kusababisha mikakati iliyowekwa kutokuwa na
mafanikio hivyo ugonjwa kuendelea kuwa ni tishio katika jamii. Ninapenda kusisitiza
kuwa, taarifa za wagonjwa wa Kipindupindu zitolewe bila kufichaatendaji
watakaoficha taarifa za wagonjwa watawajibishwa ipasavyo.
Changamoto
nyingine iliyopo ni ushiriki mdogo wa sekta nyingine katika kupambana na
ugonjwa huu. Ninaomba ieleweke kuwa mapambano dhidi ya Kipindupindu
yatafanikiwa ikiwa sekta nyingine kama Maji, miundombinu, biashara, elimu,
mazingira n.k zitashirikiana. Wizara yangu imeendelea kusisitiiza ushirikiano
huu katika ngazi ya Taifa, Mkoa na Wilaya, ili mipango ya kupambana na Kipindupindu
ishirikishe sekta mbalimbali.
Wizara
imeendelea kupeleka timu mbalimbali kutoka nngazi ya taifa katika mikoa ambayo
bado kuna changamoto ikiwa ni pamoja na Morogoro, Simiyu, Mwanza, Mara, Mbeya
na Manyara ili kuweza kushirikiana na mikoa hiyo katika kudhibiti Ugonjwa wa
Kipindupindu. Bado naendelea kusisitiza mapambano ya Kipindupindu yanahitaji ushirikishwaji
wa ngazi zote hadi katika ngazi ya kaya hivyo tukishirikiana kwa pamoja
tutatokomeza Kipindupindu
Ndugu Waandishi wa Habari,
Pamoja
na mapambano dhidi ya Kipindupindu, Wizara yangu inaendelea kutoa tahadhari ya
Ugonjwa wa Homa ya Zika, unaosababishwa na kirusi kijulikanacho kama “Zika Virus”. Ugonjwa wa Homa ya Zika unaenezwa
na mbu aina ya Aedes ambaye ana tabia ya kuuma asubuhi na pia nyakati za mchana
au jioni. Aina hii ya kirusi ipo katika familia ya “Flavivirus” ambapo pia vipo
virusi vya ugonjwa wa Dengue, Homa ya Manjano (Yellow Fever) na wengineo.
Kuanzia
mwezi Mei 2015, ugonjwa huu ulianza kutolewa taarifa ambapo hadi sasa umeathiri
zaidi Bara la Amerika ya Kusini. Kuna takriban nchi 22 ambako wagonjwa
wamethibitishwa kimaabara kuwa na ugonjwa wa Zika. Mlipuko wa ugonjwa huu umethibitishwa
na Shirika la Afya Duniani kuwa ni janga la kimataifa. Napenda kusema kuwa hakuna
mgonjwa yeyote ambaye amekwisharipotiwa nchini Tanzania hadi sasa.
Hata
hivyo, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, pamoja na
kuwatoa hofu wananchi, inawakumbusha kuwa waendelee kuchukua tahadhari dhidi ya
ugonjwa wa Homa ya Zika pamoja na magonjwa mengine yanayoenezwa na mbu ikiwa ni
pamoja na kuzingatia yafuatayo:-
(i)
Kuangamiza mazalio ya mbu kwa:
Ø kufukia
madimbwi ya maji yaliyotuama au kunyunyizia viuatilifu vya kuua viluwiluwi vya
mbu kwenye madimbwi hayo.
Ø kuondoa
vitu vyote vinavyoweza kuweka mazalio ya mbu kama vile; vifuu vya nazi, makopo,
magurudumu ya magari yaliyotupwa hovyo, nk.
Ø kufyeka
vichaka vilivyo karibu na makazi ya watu.
Ø Kuhakikisha
kuwa maua yanayopandwa kwenye makopo au ndoo hayaruhusu maji kutuama.
Ø kufunika
mashimo ya maji taka kwa mifuniko imara.
Ø kusafisha
gata za paa la nyumba ili kutoruhusu maji kutuama.
(ii)
Kujikinga na kuumwa na mbu kwa;-
Ø Kutumia
viuatilifu vya kufukuza mbu “mosquito repellants”.
Ø Kuvaa
nguo ndefu ili kujikinga na kuumwa na mbu.
Ø Kutumia
vyandarua vilivyosindikwa viuatilifu (kwa wale wanaolala majira ya mchana hasa
watoto).
Ø kuweka
nyavu kwenye madirisha na milango ya nyumba za kuishi.
Serikali, kupitia Wizara yangu pamoja na
wadau inaendelea kusimamia yafuatayo:
·
Kuimarisha ufuatiliaji wa ugonjwa huu katika
vituo vya kutolea huduma za afya pamoja na mipakani kupitia mfumo wa ufuatiliaji
magonjwa “surveillance” ya Wizara.
·
Aidha, kufuatilia kwa karibu ongezeko la
wagonjwa wenye homa isiyokuwa ya malaria kwa Mikoa na Wilaya zote nchini ili
kuweza kufanya uchunguzi wa kina iwapo kuna ugonjwa huu.
·
Kuendelea na mikakati ya kudhibiti mbu
waenezao magonjwa ikiwa ni pamoja na kusistiza
matumizi ya vyandarua vyenye viuatilifu
·
Kuimarisha uwezo wa kutambua ugonjwa huu kwa
kina kupitia maabara ya Taifa iliyopo katika Taasisi ya uchunguzi wa Magonjwa
ya Binadamu (NIMR). Wizara itashirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo Shirika
la Afya Duniani (WHO) na Kituo cha Kudhibiti Magonjwa (Centre for Disease
Control (CDC) katika kuhakikisha kuwa vitendanishi vya kutambua ugonjwa huu
vinapatikana.
·
Kushirikisha program ya Malaria na NIMR
katika kudhibiti mbu kwa kupulizia na kunyunyizia viuatilifu. Hii inalenga kuangamiza mbu wapevu na viluwiluwi.
·
Kuhakikisha utoaji wa tiba sahihi na kwa
wakati
·
Wizara itaanza kutoa elimu kwa wananchi
kupitia Radio na Runinga kuhusu ugonjwa huu sambamba pia na ugonjwa wa Dengue
ambao uambukizi wake unasababishwa na Mbu aina ya Aedes.
·
Kufuatilia wajawazito kwa ajili ya kupata
taarifa za watoto watakaozaliwa wakiwa na ulemavu wowote wa kichwa ikiwemo
“microcephaly” au “anencephaly”.
Hitimisho
Wizara
itaendelea kutoa taarifa za mara kwa mara kwa wananchi ili waweze kuelewa
kuhusu magonjwa haya pamoja na ugonjwa wa Zika na kuchukua hatua stahiki. Aidha,
ninatoa rai kwa jamii, wataalamu na viongozi katika ngazi zote kila mmoja
kutimiza wajibu wake katika harakati za kuudhibiti ugonjwa wa Kipindupindu na
tahadhari ya Ugonjwa wa Zika.
Tunawashukuru
wadau wote, yakiwemo Mashirika ya Kimataifa kwa mchango wao mkubwa katika
jitihada zetu za kupambana na magonjwa.
Nawashukuru
kwa kunisikiliza.
No comments:
Post a Comment