Pages

Pages

Pages

Friday 11 December 2015

HII NDIYO KANSA ITAKAYOIMALIZA CHADEMA 2020




Na Daniel Mbega

YAMETOKEA tena ndani ya Chadema, kama ilivyokuwa mwaka 2010. Viti Maalum vya ubunge vimeleta nongwa na vimezidi kudhihirisha wazi hakuna demokrasia ndani ya chama hicho cha upinzani.
Pengine walichofanikiwa mwaka huu ni ‘kuwalipa fadhila mashushushu’ wao waliokuwa ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) kwa kuwapatia ubunge wa viti maalum.
Lakini kidonda bado kibichi japo kinaonekana kukauka. Ndani kinafukuta. Na daima kidonda kiko kwako, kwa mwenzio hakiumi!

Naam. Nilisema mwaka 2010 mara tu baada ya kukamilika kwa zoezi la uteuzi wa wabunge wa viti maalum, kwamba kulikuwa na undugunaizesheni katika uteuzi ule. Kama kawaida, wapo waliopinga kwamba andiko langu lilikuwa ‘la kinafiki’ kama ambavyo watasema hata sasa.
Wakati ule nilisema kulikuwa na figisu nyingi tangu katika uchaguzi wa kwanza wa viti maalum kupitia chama hicho, kwa sababu ilidaiwa kulikuwa na hujuma huku baadhi ya wagombea wakidaiwa kuwachukua mamluki ili wawachague.
Uongozi wa juu ukaingilia kati na kusitisha zoezi hilo kwa maelezo kwamba wateule wa viti hivyo wangepatikana kulingana na matokeo ya kura za ubunge katika uchaguzi mkuu kwa kuangalia wanawake ambao walijitokeza kwenye majimbo na kushindwa, ambao ndio wangepewa kipaumbele cha kwanza.
Kwa kifupi, njia ya kura ilishindikana kutokana na kuibuka kwa makundi ya Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na Naibu Katibu Mkuu (wakati huo), Zitto Kabwe, wakati wa uchaguzi wa wabunge hao kupitia wajumbe wa Baraza la Wanawake wa Chadema (Bawacha).
Ndipo hatimaye wakaamua kumtumia mtaalamu kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ‘school mate’ wangu wa enzi zile Pugu Sekondari, Prof. Kitila Mkumbo, mwanaharakati mahiri tangu tulipokuwa na mijadala ya kupitisha mfumo wa vyama vingi mwaka 1992.
Kulikuwa na vigezo kadhaa ambavyo vilipaswa kuzingatiwa kwenye uteuzi huo, miongoni mwake ni mchango wa muombaji katika kukijenga na kukiimarisha chama tangu mwaka 2005 hadi 2010, kiwango cha elimu cha muombaji (kuanzia Shahada ya Uzamivu, Shahada ya Uzamili, Shahada ya Kwanza, Stashahada, Kidato cha Sita, cha Nne au Darasa la Saba) na pia mchango wa muombaji katika kampeni za uchaguzi 2010.
Yakapatikana majina 105 ya wateule hao ambayo orodha yake iliwasilishwa kwenye Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) Septemba 30, 2010 na Kaimu Katibu Mkuu wa Chadema John Mnyika.
Waliopewa kipaumbele, na ambao walipitishwa, walikuwa wake, watoto na ndugu wa vigogo na viongozi wa chama hicho, wakiwemo pia wabunge wote wa viti maalumu wa Chadema waliomaliza muda wao, na waliokuwa wakigombea katika majimbo ya uchaguzi ambao walirudishwa katika orodha hiyo na kupewa nafasi za juu.
Waliomaliza muda wao na kurejea tena Bungeni kupitia viti maalum ni Lucy Owenya (mtoto wa aliyekuwa Mbunge wa Moshi Mjini, Philemon Ndesamburo), huyu alikuwa wa kwanza kwenye orodha hiyo.
Wengine ni dada-binamu wa Zitto Kabwe, Mhonga Said Ruhwanya (alikuwa namba 3), Grace Kiwelu (alikuwa wa 9 - ambaye ni mkwewe Ndesamburo), Anna Maulida Komu (13), Susan Anselem Lyimo (10), Rose Kamil Sukum (19 - ambaye ni mke wa zamani wa Dk. Willibrod Slaa).
Halima Mdee alishika nafasi ya tano kwenye orodha hiyo, lakini yeye alipenya moja kwa moja baada ya kushinda kwenye Jimbo la Kawe jijini Dar es Salaam. Walioshindwa kwenye majimbo ni pamoja na Rose Kamili (Hanang’), Leticia Musobi Nyerere (Kwimba), Regia Mtema (Kilombero), Anna Komu (Kigamboni), na Mwanamrisho Abama.
Wengine waliopita walikuwa Christina Lissu Mughwai (dada wa Tundu Lissu), Joyce Mukya (mzazi mwenzake na Mbowe), Paulina Slaa Narcis, Easther Matiko, Anna Mallac, Paulina Gekul, Conjesta Rwamlaza, Susan Kiwanga, Christowaja Mtinda, Joyce Mukya, Naomi Kaihula, Chiku Abwao, Raya Hamisi, Philipa Mturano, Mariam Msabaha, Rachel Mashishanga, mwanahabari Rebecca Mngodo, na Cecilia Pareso.
Ndiyo. Ni wale wale wenye nasaba na ujamaa na viongozi wa juu wa Chadema, ambao kwa kiasi kikubwa ndio waliokuwa wakitajwa hata katika uchaguzi kwamba walikuwa wanapendelewa.
Sinema bado inaendelea. Baada ya kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, Tume ya Taifa Uchaguzi (NEC) ilitangaza mgawanyo wa wabunge wa viti maalum kwa CCM, Chadema pamoja na Chama cha Wananchi (CUF), ambapo CCM ilipata wabunge 64, Chadema 36 na CUF 10.
Baada ya mgawanyo huo, vyama mbalimbali vya kisiasa vilifanya michakato yao ya ndani na kutangaza majina ya wabunge husika watakaoviwakilisha vyama vyao. 
Malalamiko yakaibuka zaidi kwa Chadema, ambapo mpaka sasa baadhi ya wanachama bado wanahoji vigezo vilivyotumika kupata majina ya wateule.  Tuhuma za kuwepo kwa urafiki na undugu zimeelezwa na wanaolalamika.
Baadhi ya majina ambayo yamesikika yakilalamikiwa ni pamoja na Anna Gideria, ambaye aliteuliwa huku akiwa bado Katibu wa UVCCM Wilaya ya Mbulu mkoani Manyara.  Kwa hiyo alilazimika kujiuzulu kwanza nafasi ya ukatibu na kukabidhi barua yake kwa Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Manyara, Regina Ndege kabla hajapokea uteuzi mpya.
Minong’ono inaeleza kuwa Gideria alipoteza imani na CCM baada ya jina la Waziri Mkuu wa zamani, Frederick Sumaye, kukatwa katika kinyang’anyiro cha kumtafuta mgombea Urais kwa tiketi ya CCM na kufuatia kitendo hicho cha Sumaye kukatwa, aliomba likizo ya mwezi mmoja – kumbe ‘akatoroka’ pamoja na Sumaye kwenda Chadema.
Tukio hilo liliwashtua wanaChadema wilayani Mbulu hususan waliokuwa wakimuona Gideria kama kiongozi na mpambanaji wa CCM na hivyo kuteuliwa kwake kulionekana kuwakatisha tamaa wanaChadema wilayani humo wanaojiuliza kwanini wachukuliwe wanaCCM huku wakiwaacha wapambanaji wa Chadema ambao walikuwa wakikipigania chama usiku na mchana.
Kwa upande wa Zanzibar, vyombo vya habari viliripoti juu ya Bawacha Zanzibar kushusha bendera za chama hicho na kufunga ofisi za katika mikoa ya Unguja na Pemba, kupinga uteuzi wa wabunge Viti Maalum baada ya Zanzibar kukosa hata nafasi moja japo wanasema ilikuwa ipate walau nafasi tano.  
Alinukuliwa Makamu Mwenyekiti wa Bawacha Zanzibar, Hamida Abdallah Aweshi, akisema kuwa wamechoka na maamuzi yaliyofikiwa na kwamba Makao Makuu ya Chadema walikataa kusikiliza kilio chao.
Katika mikoa ya Mbeya na Songwe, Bawacha ilitangaza kutounga mkono uteuzi wa wabunge hao kwa madai kuwa haukuzingatia usawa na haki kwa wanachama. Mwenyekiti wa Bawacha anayewakilisha mikoa hiyo, Happiness Kwilabya alisema wanawake wa Chadema wamekatishwa tamaa kwa kiasi kikubwa na uteuzi wa wabunge hao uliofanywa bila kuzingatia haki na sawa.
“Tumesikitishwa na uteuzi usioeleweka umetumia vigezo gani sijui. Tunakusudia kukutana ili kutoa tamko letu rasmi,” alisema na kuhoji: “Je, ni haki kwa Mkoa wa Songwe ambao una wabunge watatu wa Chadema kutokana na mchango mkubwa wa wanawake, kukosa mbunge wa viti maalum?”
Kauli iliyotolewa na aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati za Wagombea Ubunge wa Chadema na Umoja wa Katika ya Wananchi (Ukawa) Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Jacob Kalua kuwa wanawake wa Chadema waliokuwa mstari wa mbele kukisadia chama, hawajateuliwa na badala yake wamepewa nafasi watu ambao hawakushiriki popote, iliongeza ukakasi na kutoa taswira hasi kwa Chadema.
“Hapa Mbeya ameteuliwa mmoja, lakini ushiriki wake kwenye chama unazidiwa na wanawake wengine walioomba nafasi hiyo waliopo hapa. Kwa upande pia wa mkoani Songwe kuna majimbo matatu ya Chadema hajateuliwa mwanamke hata mmoja. Je, hii ni halali?” alikaririwa akihoji Kalua.
Wakati Mbeya wakihoji, wenzao wa mkoa  Rukwa walifika mbali zaidi kufuatia kujiuzulu kwa  aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema Mkoa, Kapteni Zeno Nkoswe, kutokana na kutoridhika na uteuzi wa wanawake mkoani humo.
Nkoswe alisema sababu ya kuachia ngazi ilitokana na hali ya sintofahamu ya wanachama wa mkoa huo waliokuwa wakimhoji mara kwa mara juu ya uteuzi uliofanywa wa mtu ambaye wanasema alikuwa akikipigia debe chama cha TLP.
Uteuzi mwingine uliolalamikiwa ni ule wa Zubeda Sakuru kwa Mkoa wa Ruvuma.  Walalamikaji walihoji uhalali wa kuletewa Mbunge wa Viti Maalum kutoka Tanga kwani inaelezwa kwamba, Sakuru aliihadaa Chadema kuwa kwao ni Ruvuma wakati ni mwenyeji wa Tanga.
Naibu Katibu Mkuu Chadema Zanzibar, Salum Mwalimu alisema mchakato wa kuwatafuta wabunge hao huanzia ngazi za chini katika majimbo na kwamba wanachama walihusishwa huku akisema wanaotoa hoja za upendeleo ni wa kupuuzwa.
Haya ni majibu mepesi kwa maswali magumu.  Na kama majibu hayo aliyoyatoa ni sahihi Je, ilikuwaje Katibu wa UVCCM Wilaya ya Mbulu, Anna Gideria akateuliwa na Chadema kuwa mbunge wa viti maalum huku wapambanaji wa muda mrefu wakiachwa? Au alikuwa ‘shushushu’ wao ndani ya CCM?
Hili ni suala nyeti kwa Chadema, na kama halikupatiwa ufumbuzi, ‘kansa’ hiyo inaweza kuwaangamiza kabisa mwaka 2020.

0656-331974

CREDIT: RAIA TANZANIA, DEC. 11, 2015


No comments:

Post a Comment