Pages

Pages

Pages

Wednesday 9 September 2015

CUF WAZINDUA KAMPENI ZANZIBAR, MAALIM SEIF AAHIDI MAMLAKA KAMILI

Wafuasi na wapenzi wa CUF waliojitokeza kwenye
Wafuasi na wapenzi wa CUF waliojitokeza kwenye uzinduzi wa kampeni za chama hicho Kibandamaiti Zainzibar. Picha na Said Khamis 

Na Emmanuel Mtengwa, Mwananchi Digital
Zanzibar. Mgombea urais wa Zanzibar kwa tiketi ya Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad amesema  kama atapewa ridhaa ya kuwa rais atahakikisha Zanzibar inapata mamlaka kamili.
Akihutubia wananchi leo kwenye uzinduzi wa kampeni za Cuf katika viwanja vya Kibanda Maiti visiwani Zanzibar, Maalim Seif amesema kuwa kama wananchi watamchagua atapigania kupata serikali ya Muungano yenye serikali tatu.

“Kama mtanichagua kitu cha kwanza, nawaahidi wananchi wa Zanzibar ni kupata serikali ya muungano yenye serikali tatu… Zanzibar kuwa na mamlaka kamili na kurejesha rasimu ya Jaji Warioba’’ amesema Maalim.

Hii ni mara ya tano kwa Maalim ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar kugombea nafasi ya urais.

Mgombea huyo ambaye ametumia dakika zisizozidi 15 kueleza vipaumbele vya serikali yake, amesema kuwa atarejesha misingi ya utawala bora ili wananchi waishi kwa amani.

Pia Maalim ameeleza kuwa, atahakikisha anajenga uchumi imara na unaokua kwa kasi ikiwa ni sehemu ya ndoto yake ya siku nyingi katika harakati za maendeleo.

“lingine ni kujenga uchumi imara na unaokuwa kwa kasi, hiyo ndio ndoto yangu ya kuifanya Zanzibar kuwa Singapore ya Afrika Mashariki… kwa kuhakikisha kujenga bandari ya kisasa, sio kwa maneno lakini kwa matendo’’ alisema.

Sambamba na hayo, amewaahidi vijana kupata ajira na mitaji ili kujiendeleza kimaisha ‘’ Nitafungua benki ya uwekezaji ya Zanzibar ili kutoa mitaji kwa vijana wetu wanaojihusisha na uvuvi ili wamudu kujiendeleza na kujiajiri’’ alisisitiza Maalim.

Aidha, katika kumalizia vipaumbele vyake, Maalim ameahidi kuwa siku 100 za mwanzo ndani ya utawala wake atahakikisha sheria ya mafuta na gesi inapatikana ili kuanza kuchimba mafuta visiwani humo.

Katika uzinduzi huo wa kampeni, pamoja na kuhudhuriwa na maelfu ya wananchi, viongozi mbalimbali, pia tukio hilo limehudhuriwa na mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chadema chini ya mwamvuli wa Ukawa, Edward Lowassa na mgombea mwenza Juma Duni Haji.

CREDIT: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment