Hiki ndicho kikosi cha Simba kilichofika fainali ya Kombe la CAF mwaka 1993. Kocha Abdallah Hussein 'Kibadeni' ni wa tatu kushoto waliosimama, anafuatiwa na Often Martin, Razack Yussuf 'Careca', George Lucas 'Gazza', Idd Selemani 'Meya', Damian Morisho Kimti, Abdul Ramadhan 'Machine', George Magere Masatu, Ramadhan Maufi 'Lenny', kocha msaidizi Etenne Eshente kutoka Ethiopia na Meneja wa Timu Abdulrahman Muchacho.
Waliochuchumaa ni Kassongo Athumani, Selemani Pembe, Edward Cyril Chumila, Dua Said, Fikiri Magoso, Malota Soma 'Ball Juggler' na Mohammed Mwameja.
Na Daniel Mbega
Simba
ilikuwa inashiriki kwa mara ya kwanza, au niseme Tanzania ilikuwa inawakilishwa
kwa mara ya kwanza kwenye michuano hii ya tatu ya kuwania Kombe la CAF
lililotolewa na mfanyabiashara wa Nigeria, Chifu Moshood Abiola, ambaye alikuwa
katika harakati za kuwania urais wa nchi hiyo kabla haujavurugwa na Jenerali
Sani Abacha.
Msimu huo wa 1993 kikosi cha Simba kilichokuwa kinanolewa na Abdallah Hussein 'Kibadeni' aliyesaidiwa na Etenne Eshente kutoka Ethiopia kilikuwa na wachezaji hawa: Mohammed Mwameja, Mackenzie Ramadhani, Often Martin (Ushirika), Deo Mkuki
(Pamba), Twaha Hamidu, Selemani Pembe, Fikiri Magosso, George Masatu, Godwin
Aswile, Kassongo Athumani, Ramadhani
Lenny, George Lucas, Hussein Marsha, Abuu Omar, Idd Selemani, Joachim
Masumbuko, Damian Kimti, Edward Chumila, Nico Kiondo, Malota Soma, Bakari Iddi,
Abdul Ramadhani Mashine, Razak Yusuf
'Careca' (Coastal Union), David Mihambo (Reli), Mbuyi Yondani (Reli), Feruzi
Teru (Milambo), Dua Said (Small Simba), Rashid Abdallah Magongo (Breweries -
Ndovu), Michael Paul na Thomas Kipese.
Simba
ilianza kampeni zake katika raundi ya kwanza kwa kupambana na Ferroviario de
Maputo ya Msumbiji kwenye uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza Februari 20, 1993,
ambapo timu hizo hazikufungana. Ziliporudiana tena Machi 6 mjini Machava,
Msumbiji, timu hizo zilifungana goli 1-1. Hivyo, Simba ikasonga mbele kwa
sheria ya goli la ugenini.
Katika
raundi ya pili ya michuano hiyo, Simba ilikumbana na Manzini Wanderers ya
Swaziland. Mchezo wa kwanza uliofanyika Mei 22, 1993 mjini Dar es Salaam, Simba
ilishinda kwa goli 1-0, ambalo lilifungwa na Malota Soma 'Ball Juggler' katika
dakika ya 14.
Ziliporudiana
Juni 6, 1993 mjini Manzini, Simba tena ilitoa kipigo cha goli 1-0 na kufanikiwa
kuingia robo fainali ya michuano hiyo. Timu nyingine zilizoingia robo fainali
ni Gor Mahia (Kenya), Insurance (Ethiopia), Al-Harrach (Algeria), Zamunta
(Niger), Mbilinga (Gabon), Atletico Sports Aviacao (Angola) na Stella Abidjan
(Ivory Coast).
Kwenye
robo fainali, Simba ilikumbana na Al-Harrach ya Algeria. Mchezo wao wa kwanza
ulifanyika mjini Dares Salaam Septemba 5, 1993 ambapo Simba iliichabanga
Al-Harrach kwa magoli 3-0 yaliyofungwa na Edward Chumila (mawili) na Abdul Mashine. Simba iliingia nusu fainali ingawa ilifungwa magoli 2-0 mjini
Algiers, Septemba 18, 1993.
Katika
nusu fainali , Simba, ambayo tayari ilikuwa imeahidiwa kupewa magari aina ya Isuzu
KIA kwa kila mchezaji na kiongozi kutoka kwa mfadhili wao mkuu, Azim Dewji, endapo wangelitwaa kombe
hilo, safari hii iliamua kuonyesha nia ya kuyapata magari hayo. Ilikuwa
inapambana na Atletico Sports Aviacao ya Angola, iliyoifunga Gor Mahia ya Kenya
kwa jumla ya magoli 4-2 katika robo fainali.
Mchezo wa
kwanza baina ya Simba na Atletico ulifanyika mjini Dar es Salaam Oktoba 17,
1993 na Simba ilishinda kwa magoli 3-1. Edward
Chumila alifunga bao la kwanza na la tatu, wakati lile la pili Aviacao walijifunga. Bao la Waangola hao lilifungwa na Nello. Ziliporudiana mjini Luanda
Oktoba 31, 1993 timu hizo hazikufungana na hivyo Simba ikawa imeingia fainali.
Kwenye
hatua ya fainali ndiko kulikokuwa na kazi ngumu. Ilikutana na Stella Abidjan ya
Ivory Coast na mchezo wao wa kwanza ulifanyika mjini Abidjan Novemba 14, 1993
na timu hizo zilitoka sare ya 0-0, lakini ziliporudiana mjini Dar es Salaam
Novemba 27, 1993 Stella iliifunga Simba magoli 2-0 na kutwaa kombe hilo la CAF.
Magoli ya Stella yalifungwa na Kouame Desire (dk.17) na Jean Boli Zozo (dk.
77).
Baada ya
mechi hiyo, Simba walitaka kukata rufaa CAF kulalamika kwamba wachezaji wawili
wa Stella, N'Guessan Serges na Jean Boli Zozo walikuwa wanachezea klabu ya
Paris Saint Germain ya Ufaransa. Mhariri wa michezo wa gazeti la Mfanyakazi, James Nhende na mwandishi
wake, Francis Lucas, waliandika katika gazeti toleo la Desemba 8, 1993 kuwa
wachezaji hao walikiri wenyewe kuwa walikuwa wanaichezea PSG ambayo ilikuwa
inaongoza Ligi Kuu ya Ufaransa.
Hata
hivyo, Mtanzania mmoja aliyekuwa akifanya kazi katika Benki ya Maendeleo ya
Afrika (ADB), Bwana Bishota, aliyekuwa akifanyia kazi mjini Abidjan, aliishauri
Simba isikate rufaa dhidi ya mchezaji Boli Zozo, kwani mchezaji huyo wa Stella
ni tofauti na Boli Zozo wa timu ya Eistre ya ufaransa iliyokuwa inashiriki Ligi
Daraja la Pili nchini humo.
Zaidi ya
hayo, klabu hiyo ya Eistre ilikwishaijulisha Simba kwamba mchezaji wao Boli
Zozo Laurent alikuwa Ufaransa na alicheza katika mchezo wa ligi siku hiyo
ambayo Simba ilikuwa inapambana na Stella.
Gazeti la Dimba toleo la Jumapili ya Desemba 5,
1993 lilikuwa limeandika kuwa mchezaji Boli Zozo wa Eistre ingawa alifanya
mazoezi Ijumaa ya Novemba 26, 1993 na timu yake hiyo ya Ufaransa, lakini
Jumamosi alikosekana kwenye mechi, hivyo kuleta wasiwasi kuwa huenda alikuja
Dar es Salaam kuichezea Stella.
Klabu ya
Eistre ilisema kuwa mchezaji wao alifanya mazoezi na timu yake Ijumaa ya
Novemba 26, 1993 na pia alikuwa mazoezini Novemba 28, hivyo isingewezekana awe
Dar es Salaam Novemba 27, siku ambayo pia alicheza mechi ya ligi.
Kwa ujumla
kulikuwa na utata mkubwa wa jina la Boli, kwani walikuwepo akina Boli wengi
waliokuwa wakicheza soka ya kulipwa nchini Ufaransa, na wote walikuwa wanatoka
Ivory Coast. Baslie Boli ndiye aliyekuwa akijulikana zaidi na alikuwa nyota
katika timu kongwe nchini humo ya
Olympique Marseille akifuatiwa na mdogo wake, Roger Boli, ambaye alikuwa
anaichezea timu ya Lens nchini humo.
Wakati
ambapo yule wa Eistre alikuwa akiitwa Boli Zozo Laurent, huyu wa Stella alikuwa
Boli Zozo Jean. Kwa hali hiyo Simba wakabwaga manyanga na kuruhusu tonge
kuponyoka mdomoni.
WASILIANA NAMI KUPITIA SIMU/WHATSAPP/TELEGRAM 0656-331 974
No comments:
Post a Comment