Pages

Pages

Pages

Tuesday 4 November 2014

TAASISI NNE ZAPIGWA 'STOP' KUTIBIWA MUHIMBILI

Muhimbili
Na Veronica Romwald, Dar es Salaam
HOSPITALI ya Taifa Muhimbili (MNH) imesitisha kutoa huduma za matibabu kwa mkopo kwa taasisi nne nchini.

Taasisi hizo ni Shirika la Umeme Tanzania (Taneseco), Shirika la Bima la Taifa (NIC), Chuo cha Kilimo cha Sokoine (SUA) na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).
Hatua hiyo imekuja ikiwa ni siku chache tangu kupandishwa kwa gharama za huduma kwa wagonjwa wa rufani ambapo kwa sasa wanalazimika kulipia kitanda Sh 5,000 pamoja na Sh 2,000 ya chakula kwa siku.
Kwa mujibu wa tangazo lililobandikwa katika mbao za matangazo hospitalini hapo na kusainiwa na Mkuu wa Idara ya Uhasibu, Cassian Faustine, hatua ya kusitishwa kwa huduma kwa taasisi hizo imechukuliwa tangu Oktoba 29, mwaka huu.
“Wakusanya mapato na watoa huduma wote, mnataarifiwa kwamba huduma za afya hazitatolewa kwa makampuni na taasisi hizi kwa mkopo (Credts) kuanzia Oktoba 29, mwaka huu hadi mtakapotaarifiwa.
“Aidha wahusika wanaweza kutibiwa kwa kulipia gharama za matibabu wao wenyewe,” lilisomeka tangazo hilo.
Kutokana na tangazo hilo, MTANZANIA ilimtafuta Ofisa Uhusiano wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Amiel Eligaesha ili kupata ufafanuzi wa kina, lakini hakupatikana.
Hata hivyo, alipotafutwa ofisa habari msaidizi wa hospitali hiyo, Dorice Ishinda, alijibu kwa kifupi atafutwe mkuu wake wa kazi ndiye anaweza kuzungumzia suala hilo.
Hospitali ya Muhimbili hivi sasa inakabiliwa na deni la Sh bilioni 8 inazodaiwa na Bohari Kuu ya Dawa (MSD).
Kutokana na deni hilo, MSD imetangaza kusitisha kutoa dawa kwa hospitali hiyo.
CREDIT: MTANZANIA

No comments:

Post a Comment