Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Saturday, 14 June 2014

RIWAYA TAMU: JUDITH…JUDITH…! - 9


INNOCENT A. NDAYANSE (ZAGALLO)

0755 040 520 / 0653 593 546 

ILIPOISHIA:
Simulizi zimemnogea Makella na sasa anaamua kunywa pombe. Anamlazimisha Judith naye anywe. Kwa woga na hofu, anaamua kunywa pombe kwa mara ya kwanza maishani mwake. Makella anasimulia mengi na kuwaponda wanawake wa Tanzania. Anajiuona yuko huru zaidi. Hatimaye anaamua kwenda kuoga. Je, nini kitaendelea hali Judith naye akiendelea kunywa pombe? Ungana na msimulizi wako…

Judith hakujibu. Alitwaa tena chupa yake na kuipeleka kinywani. Sasa alikunywa bia hiyo kama anywaye maji ya kawaida. Hakikuwa kinywaji kigeni. Ulimi ulishazoea. Funda tatu zikapita kooni kwa mkupuo. Na Makella aliamini kuwa, kama Judith ataimaliza bia hiyo basi lazima atakuwa hoi, na hatakuwa na kipingamizi chochote cha kutendwa vyovyote. Zaidi, atatoa ushirikiano mkubwa bila ya woga wala aibu.
“Wewe endelea,” Makella alimwambia Judith. “Ikiisha, s’o vibaya ukiongeza moja. Nakuhakikishia, kinywaji hicho kitakufanya ujisikie vizuri sana kisaikolojia.”
Alipomaliza kuchojoa nguo, alitwaa taulo iliyokuwa imetundikwa kwenye eneo maalum, taulo ya hoteli, akajifunga kiunoni na kuelekea bafuni.
**********
DAKIKA ya kwanza baada ya Makella kuingia bafuni Judith alikuwa ameduwaa. Dakika ya pili ndipo akili yake ilipochangamka. Akazitazama zile chupa za bia zilizokuwa mbele yake. Akatema mate chini huku kakunja uso. Akasimama haraka na kutupa macho kitandani ambako bunduki ilikuwa imetulia. Akayahamishia macho kwenye nguo za Makella. Papohapo akazifuata na kuanza kuzipekua.
Sasa alikwishabadilika. Hakuwa yule Judith mwenye macho yaliyolegea kiasi cha kumfanya Makella ajiamini na kuwa na matumaini ya kustarehe kwa usiku huo. Hapana. Huyu alikuwa Judith mwingine, Judith ambaye alitaka aitimize azma yake iwe, isiwe! Kiwango cha bia aliyokunywa pia kikawa kinamwongezea ujasiri na kumwondolea woga.
Mfuko wa kwanza wa suruali hakuambulia kitu. Akauvaa mfuko wa pili. Humo akatoa kitambulisho cha uraia, na kitambulisho cha jeshi, akavitupa zuliani na kuukimbilia mfuko mwingine uliokuwa umetuna kidogo. Akashtuka baada ya kutoa bulungutu la pesa! Moyo ukapiga paa! Akashusha pumzi kwa nguvu.
Noti alizozitoa zilikuwa ni dola za Marekani 2,000. Hakuyaamini macho yake! Hakuwa mgeni wa noti hizi. Miezi kadhaa iliyopita marehemu baba yake mzazi aliwahi kumwonyesha sarafu na noti za Rwanda, Kenya, Tanzania, Uingereza, Ufaransa na Marekani.
Katika zoezi hilo alimwambia, “Mwanangu Judi, pesa za Wazungu zina thamani sana, na hasa pauni na dola. Pauni ni za Uingereza na Dola za Marekani. Hizo zina nguvu zaidi dunia nzima! Lakini haya mafaranga yetu ya Kinyarwanda, Kirundi na vikorokoro vya Tanzania, Uganda na Kongo mmh! Havina kitu! Afadhalli kidogo pesa ya Kenya, ile ina nguvu kuliko zingine za ukanda huu.”
Maneno hayo hakuyasahau, na sura za noti hizo hazikutoka katika kumbukumbu zake kichwani tangu siku hiyo. Na usiku huo, akiwa humo chumbani, peke yake, dola 2,000 za Marekani zikiwa mkononi mwake, alijiona kishaiweka Rwanda katika himaya yake.
Dola 2,000! Mungu ampe nini? Ndiyo, Mungu ampe nini yeye mtoto wa kike ambaye hajawahi kumiliki dola 100?
Akashusha pumzi ndefu huku akizipachika kwenye mfuko wa bukta yake aliyoivaa ndani ya sketi. Akairudia tena suruali hiyo. Akaukagua mfuko wa mwisho lakini hakupata kitu. Akahamia kwenye mfuko wa shati. Huko akaambulia sigara tatu na kibiriti. Akasonya na kuvirudisha.
Sasa akayatupa macho kwenye mlango wa bafu. Ni muda mfupi tu uliopita tangu Makella alipoingia bafuni humo, na kwa mbali alisikia michirizi ya maji, hali iliyompa taswira kuwa tayari Makella kishaanza kuoga.
Papohapo Judith akaifuata ile bunduki, AK-47 na kuikamata mkononi. Akaguna. Uzito wa silaha hiyo ukamvunja moyo. Hakutaka kujidanganya kuwa anaweza kuitumia silaha hiyo dhidi ya adui yake yeyote kama akiamua kutoroka nayo. Kwanza, ni nzito. Pili, hajawahi hata kujifunza jinsi ya kuitumia. Akahema kwa nguvu huku akiirudisha taratibu kitandani. Akahisi woga ukimjia, lakini akajitahidi kujipa ujasiri, akijua kuwa hakuna mtu wa kumwokoa bali anapaswa kutumia akili yake yote ili ajinusuru dhidi ya jahili huyo.
Huo ulikuwa ni muda pekee ambao aliamini kuwa ndiyo angeweza kuutumia katika kujiokoa. Akapiga ngumi kiganjani na kuamua kuondoka. Papohapo akautwaa ufunguo na kutoka taratibu, kisha taratibu vilevile akaurudisha mlango na kuuchomeka ufunguo kwenye kitasa. Akafunga taratibu na kwa umakini huku akiangaza macho kushoto na kulia katika korido hiyo. Korido yote ilikuwa tulivu na hakukuwa na mtu yeyote.
Akafurahishwa na hali hiyo na papohapo akauchomoa ufungo katika kitasa, akautumbukiza katika mfuko wa bukta yake. Akatoka taratibu, akipita katika korido hiyo ya ghorofa ya kwanza ya hoteli hiyo yenye ghorofa nne, mwendo wake ukiwa ni wa mtu wa kawaida na asiye na wasiwasi. Watu wawili aliokutana nao, mmojawao akiwa ni mwanamke wa Kizungu hawakumtilia shaka wala kumshangaa.
Alipofika chini alikwenda moja kwa moja mapokezi na kumtazama yule mhudumu kwa uso wa kirafiki, huku akiachia tabasamu la mbali. Kisha, akamwambia, “Dada, natoka kidogo. Nafika mtaa wa pili mara moja. Sitachelewa.”
“Ok,” mhudumu yule alimjibu huku akimtazama kwa macho ya wivu, akivutiwa na umbo zuri alilojaaliwa  Judith hususan yale ‘makalio ya kumimina’ ambayo yalijitupa huku na kule wakati Judith alipokuwa akiondoka.
Ilikuwa ni saa 5 usiku!
**********  
MIONGONI mwa kanuni ambazo Makella hakuwa tayari kuzitengua ni kuoga maji baridi. Awe na malaria, awe amekumbwa na uchovu mkali kiasi gani au hata awe anaihisi baridi kali maungoni, kamwe hakuwa tayari kuoga maji moto.
Usiku huo, pale tu alipoingia bafuni hakuwa na haraka. Alifungua bomba na kuyaacha maji yaingie kwa wingi ndani ya sinki ndipo akaingia na kuoga kwa raha zake.
Alioga kwa utulivu, moyoni akijihisi amani, akikumbuka kuwa huko chumbani kamwacha msichana mzuri ambaye kwa muda mrefu amekuwa akihangaika ili ampate. Leo, usiku huu, yuko naye! Ni raha iliyoje?
Akajifariji kwa imani kuwa, pindi watakapokiangukia kitanda, ataburudika kwa kuyanyonya yale matiti yaliyoshiba, yenye joto la uhai na ambayo ujazo wake pale kifuani uliongeza urembo wa Judith badala ya kutoa sura ya kuchusha. Hataishia hapo, ataendelea kujiliwaza kwa kuyatomasa na kuyapapasa maeneo mengine nyeti ya mwili huo unaovutia kabla ya kuhitimisha starehe kwa hatua nyingine muhimu zaidi.
Mungu ampe nini?

Dakika kumi baadaye alikuwa akijifuta maji mwilini kisha akajifunga taulo kiunoni kama awali na kutoka taratibu bafuni humo.
Itaendelea kesho....

No comments:

Post a Comment