Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Wednesday, 11 June 2014

RIWAYA TAMU: JUDITH…JUDITH…! - 8

INNOCENT A. NDAYANSE (ZAGALLO)

0755 040 520 / 0653 593 546 
 Ilipoishia jana:

Makella yuko na Judith, anaamini kwamba binti huyo sasa atampenda kutokana na ukweli kuwa yeye ndiye aliyeushikilia uhai wake. Anaanza kusimulia mambo mbalimbali ikiwemo uzoefu wake wa kuishi Dar es Salaam. Judith anaendelea kumsikiliza. Ungana na msimulizi wako…

Akaendelea, “Na siyo  taarabu tu, pia kuna wapenzi wa bongo fleva ambao ni vijana wa kishkaji-shkaji na wengine nd’o wanapenda dansi. Kuna bendi za Kikongo zilizolowea hapo Dar na nyingine ni za hapohapo Tanzania kama kongwe za Msondo Ngoma, Mlimani, African Stars na nyingine ndogondogo.”
Ukimya mfupi ukatawala. Makella akanyanyua chupa na kuipeleka kinywani. Akagugumia funda kadhaa na kuirejesha juu ya kimeza. Akayagandisha macho usoni pa Judith kama vile anayemuuliza, “mbona na wewe hunywi?”
Judith hakuwa mbumbumbu wa fikra. Dhamira yake ya kuhakikisha kuwa anailinda heshima na uhai wake ilikuwa palepale! Na hakukuwa na binadamu wa kuweza kuitengua. Alimtazama mara moja tu Makella na kubaini ni kipi alichohitaji. Kwamba anywe bia yake hiyo iliyokwishafunguliwa.
Hakutaka kumfanya Makella ahisi tofauti yoyote. Bado ilikuwa ni mapema hivyo Judith alijali kuwa makini ili mambo yasiharibike. Alitaka afanye kila jambo kwa uangalifu na umakini wa hali ya juu ili kisiharibike kitu. Akaitwaa chupa hiyo na kuipeleka kinywani. Akameza funda moja  kwa jitihada kubwa. Mwili ukamsisimka lakini akajitahidi kutoukunja uso. Akataka aonekane kuwa ni mtu aliyekwishakizoea kinywaji hicho.
Hakuwa na kumbukumbu sahihi za maisha yake wakati akiwa  mtoto mdogo. Lakini alikumbuka vizuri kuwa tangu aanze kuwa na akili ya kutambua jema na baya, hadi usiku huu, hakuwahi kupitisha tone la pombe kinywani mwake. Katika umri huu mkubwa aliokwishafikia, aliwahi kusikia kuwa baadhi ya wazazi huwa na tabia ya kuwanywesha watoto wao wachanga kijiko kimoja cha pombe kali kwa kile walichodai kuwa ni  ‘kuua michango.’
Hakuwa na hakika kuwa na yeye alifanyiwa hivyo na wazazi wake. Hakujua na kwa usiku huu asingeweza kujua na hakuwa na haja ya kujua. Alichojua hapo ni kwamba, kwa mara ya kwanza anaipitisha pombe kinywani mwake na kuiruhusu iteremke tumboni mwake!
Mara ya kwanza kunywa pombe!
Funda la kwanza lilipopenya kooni alihisi kanywa shubiri. Akajikaza kisabuni, akainama kidogo na kwa sekunde chache akaukunja uso katika namna ambayo Makella hakumwona na punde akaunyanyua na kumtazama sawia.
Hata hivyo haikumwingia akilini Makella kuwa kinywaji hicho kilimsumbua Judith hata kidogo. Aliamini hivyo na ndivyo akili yake ilivyomtuma kuamini kuwa kila Mhutu, kila Mtutsi na yeyote wa kabila lolote nchini humo, pombe ni sehemu ya maisha yake.
Hivyo, yeye pia aliitwaa chupa yake ya bia na kunywa funda kadhaa kwa pupa kabla hajaitua kwenye kijimeza.
Kisha akaendelea, “Turudi kwenye hoja yetu. Cha kushangaza, wanawake wengi wa Tanzania, wana tabia za ajabu. Utakuta mwanamke kaingia baa tangu saa sita mchana na kuganda akinywa ile mimaji yao ya chupa! Shaa! Sijui wako-aje? Au labda…” akasita  na kukunja uso.
Akamtazama Judith kwa macho makali. Kisha akasema, “Ndiyo, nina shaka huenda wengi wao wako kwenye dozi kubwa.” Akacheka kicheko cha dhihaka.
Kicheko hicho kilimshangaza Judith kiasi cha kumuuliza, “Dozi kubwa?! Una maana gani?”
Kwa mara nyingine Makella alicheka. Kisha kwa sauti ya bezo akasema, “Wengi wameshaukwaa…!” akacheka tena, safari hii kwa sauti ya chini  zaidi. Akaongeza, “Hili gonjwa la Ukimwi limeharibu mambo. Utakuta mwanamke mzuri…lakini kumbe yuko kwenye dozi ya zile dawa ya kuongeza siku za kuishi. Mtu unakunywa kila siku mpaka siku yako ya mwisho ya kuishi. Na zamani nasikia ilikuwa ukishaanza kunywa midawa ile, wewe na bia basi! Yaani wewe na raha za dunia nd’o basi tena! Unakuwa mtu wa kula sana na kuhakikisha kila siku unakunywa dawa hizo! Lakini siku hizi nasikia mtu anaweza kuwa anapiga hizo dawa…wenyewe wanaziita ‘karanga’ na bia akanywa na hata sigara anavuta!”
“Hee!” Judith alishangaa, mkono kaziba mdomo, macho yamemtoka, akimtazama Makella.
“Basi tuachane na mambo hayo,” Makella alisema huku akitwaa chupa yake na kugugumia tena kinywaji chake.
Judith hakutaka makuu. Naye alitwaa chupa na kuipeleka kinywani, akashusha kooni funda dogo la kinywaji hicho kisha akamtazama Makella. Akamwona jinsi anavyojisikia kuwa huru zaidi.
“Nadhani nikaoge,” Makella alisema huku akiimaliza bia yake chupani.
Akasimama na kuchojoa nguo zake. Papohapo harufu kali ya jasho ikajitokeza na kumfanya Judith akunje uso kidogo na kwa siri.
“Sasa hivi?” Judith aliilazimisha sauti yake. Kwa ujumla swali hilo lilimtoka tu wala hakuwa amepanga kuhoji chochote, na ukweli ni kwamba hakuwa mtu wa kuzungumza chochote na Makella.

“Ndiyo, ni vizuri nikaoge sasa hivi. Pilikapilka za mchana kutwa zimenifanya nijisikie ovyo na kunitia kichefuchefu. Nadhani nikioga nitajisikia fresh kiasi. Nitakunywa bia kwa starehe na tutaongea kwa amani na utulivu, eti mpenzi?”
Itaendelea kesho...

No comments:

Post a Comment