Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Tuesday, 10 June 2014

RIWAYA TAMU: JUDITH…JUDITH…! - 7

INNOCENT A. NDAYANSE (ZAGALLO)

0755 040 520 / 0653 593 546 
  
Kizungumkuti kinaendelea baina ya Judith na Makella anayedai anampenda wakati tayari amekwishaamuru familia ya Judith iuawe. Je, Judith atamjibu nini? Ungana na msimulizi wako…

Akatupa macho juu ya meza ndogo iliyokuwa katikati ya chumba hicho. Akauona ufunguo. Akakumbuka kuwa muda mfupi baada ya yule mfanyakazi wa hoteli kuwafungulia mlango, alimkabidhi ufunguo Makella. Kwa vyovyote ndio utakuwa huu, alijiaminisha.
Hata hivyo, aliwaza, hata kama ufunguo ndio huo, bado ilihitajika akili ya ziada katika kumzidi ujanja Makella. Akili yake ikaendelea kumjengea imani kuwa ndani ya jokofu lililo mbele yake kuna vinywaji na miongoni mwa vinywaji hivyo ni Primus, bia inayoaminika, kukubalika na kuheshimika kwa Wanyarwanda na Warundi wengi.
Judith aliomba Mungu kimoyomoyo, Makella awe mnywaji, anywe Primus na huo ndio utakuwa mwanzo wa yeye, Judith kunusurika. Kwamba atajinusuru vipi, hilo hakutaka kulifikiria wakati huo, lakini aliamini hivyo. Na aliamini kuwa Mungu yupo na atakuwa upande wake!
Bado mkono wa Makella ulikuwa katika ziara mwilini mwa Judith. Sasa ulikuwa umehama pajani na  kutua kifuani ambako ulianza kuyatomasa matiti machanga, yenye joto la uhai, joto liwezalo kumsisimua mwanamume yeyote mkamilifu.
Judith akiwa ni mwanadamu kamili, mwenye viungo vilivyokamilika, kwa mbali alijikuta akisisimkwa. Ndiyo, aliuhisi msisimko mwilini mwake lakini ukawa ni msisimko ambao haukudumu zaidi ya sekunde kumi. Angepata raha gani, angeupataje msisimko wakati familia yake yote imeteketezwa muda mfupi uliopita?
Kwa ustaarabu aliushika mkono wa Makella na kuutoa kifuani pake taratibu huku akiuminyamimya kiganjani katika namna iliyomchanganya zaidi Makella.
“Judi…Judi…” Makella alinong’ona kwa taabu huku akimvuta Judith na kumbusu shavuni. Kisha akataka kumbusu kinywani, tendo lililokumbana na kipingamizi kutoka kwa Judith lakini kikiwa ni kipingamizi kilichowekwa kwa namna nyingine ya kistaarabu. Alichofanya Judith ni kuukwepesha mdomo wake kwa namna ya kuona aibu huku akiachia tabasamu laini na kuuinamisha uso.
“Judi…” kwa mara nyingine Makella alinong’ona, safari hii akiwa kama anayeomboleza.
“Bwana nimechoka!” sauti ya Judith ilikuwa ya deko.
“Umechoka?” likamtoka Makella bila ya kutarajia.
Judith akaitika kwa kutikisa kichwa, kisha akaongeza kwa sauti, “Halafu nasikia kiu!”
“Kiu!” Makella aliropoka. Papohapo alinyanyuka na kulifuata jokofu. Akalifungua na kuliacha wazi. Macho yakatua ndani na kushuhudia shehena ya vinywaji mbalimbali; soda, maji, mvinyo, bia na pombe kali.
“Kinywaji gani mrembo?” Makella alimuuliza Judith huku bado akiwa ameuach wazi mlango wa jokofu labda ili na Judith pia avishuhudie vinywaji hivyo.
“Maji.”
“Maji?” Makella alishangaa. “Kwa nini usinywe bia au wine?”
“Sijazoea.”
Makella akacheka kidogo. “Ni vinywaji vizuri na bora kwa afya,” alisema huku akitoa chupa mbili za bia. Akaongeza, “Jaribu. Ukizoea utaitaka kila siku. Kwa leo ukinywa moja tu itatosha. Na utachangamka kimwili na kiakili. Sipendi uwe katika lindi la mawazo mtoto mzuri kama wewe.”
Akaziweka chupa hizo juu ya kimeza na kuzifungua. “Nikupatie glasi?”
“Hapana, nitakunywa hivihivi,” Judith alijibu. Wakati huo alikuwa akiwaza jinsi atakavyojisikia pale atakapolipenyeza funda la pombe kinywani mwake kwa mara ya kwanza maishani mwake.
“Hapo umeonyesha kuwa wewe ni binti wa kisasa,” Makella alisema huku akiachia tabasamu kubwa. Akaongeza, “Ningeshangaa, binti mzuri wa Kitutsi asinywe bia! Lingekuwa ni jambo la ajabu! Hapo kwa kweli nisingekuelewa. Wasichana wa Kitanzania ndio wenye ushamba wa aina hiyo.
“Kule Tanzania nilishakaa kwa mwezi mmoja na kitu. Nilikuwa Dar es Salaam. Tuache uongo, Dar es Salaam ni mji mkubwa sana…mkubwa sana kuliko Kigali hata Bujumbura! Ni jiji kubwa,  jiji lenye wakazi wengi sana, kama milioni tano au kumi!
“Ni jiji lenye majumba mengi, mazuri na makubwa sana! Kwa sasa kila kukicha jiji lile linabadilika. Kama ulikuwa kule miaka mitano iliyopita leo ukiingia utapotea! Wallahi nakuapia! Kila siku linazidi kupendeza, na hayo majumba yenyewe yanayojengwa acha tu…ni mazuri!
“Dar es Salaam pia ni jiji lenye mambo mengi kama ambavyo lina wakazi wengi. Ni jiji lenye maraha na karaha. Kuna baa nyingi na kumbi nyingi za starehe na pia kuna bendi nyingi za dansi, taarabu na bongo fleva. Ukilinganisha na huku kwetu, ni majirani zetu tu wa Burundi ambao miaka ya themanini walikuwa na vikundi vya taarabu ambavyo kwa kweli vilitikisa sana katika Ukanda wa Maziwa Makuu. Kulikuwa na vikundi vya Jasmine Musical Taarab na Shani Musical Taarab ambavyo vilitisha!

“Lakini siyo leo…! Leo Tanzania ina vikundi vya taarabu vinavyopiga huu mtindo mpya wa morden…mmmh acha tu! Watu wanakata viuno kama wanamuziki wa Kikongo! Hahahahahaha…” kicheko chake kikatisha badala ya kupendeza masikioni mwa Judith.
Itaendelea kesho... 

No comments:

Post a Comment