Pages

Pages

Pages

Thursday 24 April 2014

WAZANZIBARI WAISHIO BARA WAWALAANI UKAWA KUSUSA BUNGE

UMOJA WA WAZANZIBAR WANAOISHI TANZANIA BARA (UWTB)
P.O. BOX 1019 DAR ES SALAAM TELL: 0718344443/0762812681

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

TUNALAANI UKAWA KUSUSIA BUNGE

Ndugu waandishi, sisi Wazanzibari tunaoishi Tanzania Bara tumestushwa, tumehudhunishwa na tumekerwa mno na kitendo cha Wabunge wa vyama vya upinzani vya NCCR, CUF na CHADEMA kutoka nje ya Bunge maalum la Katiba linaloendelea mjini Dodoma na kususia vikao vya Bunge hilo.

Ikumbukwe kuwa Bunge hili limeandaliwa kwa fedha nyingi za walipa kodi wa Taifa hili kwa madhumuni ya kuhakikisha kuwa Tanzania inapata Katiba mpya itakayoleta maendeleo kwa wananchi. Kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa kuhusu mchakato wa upatikanaji wa Katiba, mahali pekee pa kujadili na kupitisha hoja mbalimbali za kutunga Katiba hiyo ni Bungeni.

Sasa inashangaza na kustaajabisha kuona Wabunge hao wakiacha kutumia fursa hiyo ya kutumia Bunge kutoa maoni yao, badala yake wanatoka na kuzurura Mitaani huku tayari wakiwa wameshalipwa mamilioni ya fedha za wananchi. Je, kitendo hiki si usaliti kwa wananchi? Tunalaani kitendo hiki kwa nguvu zote na kutaka wananchi wote wa Bara na Visiwani kulaani kitendo hiki. Sisi tunaamini kuwa Katiba mpya haiwezi kupatikana kwa maandamano na mikutano ya hadhara, bali ni kwa kutumia Bunge Maalum linalogharamiwa na wananchi. Hivyo tunawataka Wabunge hao warejee haraka Bungeni ili wasitucheleweshe kupata Katiba mpya kwa ubinafsi wao.

Sababu walizozitoa kwa ajili ya kususia vikao vya Bunge hilo eti wanatukanwa na kubaguliwa, hazina mashiko. Kwa sababu kama ni matusi ndiyo ingekuwa sababu za kususia vikao vya Bunge hilo, basi Wabunge wote wangesusia pale Wabunge wa Upinzani walipowatusi na kuwakashfu Waasisi wa Taifa letu Mwalimu Julius Nyerere na Sheikh Abeid Karume. Lakini hata baada ya wao kuwatusi Waasisi hao, Bunge hilo liliwavumilia na kuendelea na wala hakuna aliyesusa.

Kuhusu muundo wa Serikali, sisi Wazanzibari tunaoishi na kufanyia shughuli zetu Tanzania Bara, bado tunasisitiza kuwa muundo peke utakaodumisha umoja wetu, mshikamano wetu na amani iliyopo, ni muundo wa Serikali mbili na si vinginevyo. Tunapinga muundo wa Serikali tatu kwasababu utaongeza gharama kubwa za uendeshaji na kusababisha mzigo mkubwa wa ulipaji kodi kwa wananchi.

Hivi sasa tupo katika muundo wa Serikali mbili tu, lakini hali ya kiuchumi kwa wananchi wa kawaida siyo ya kuridhisha. Je, tutakapoongeza idadi ya Serikali hadi ziwe tatu hali ya maisha itakuwaje? Mbali ya suala la gharama lakini pia tunaamini kuwa usalama wa muungano huu upo ndani ya Serikali mbili. Kinyume chake, muungano huu utavunjika na kusambaratika. Kitu ambacho hatupendi kitokee.

Mwisho:
Sisi Wazanzibari tunaoishi Bara tutaendelea kuufurahia Muungano wetu na kuwa pamoja na wale ambao wanautakia mema Muungano wetu. Tunawasihi na kuwaomba Watanzania wenzetu kuwapuuza Viongozi wa UKAWA kwa jambo lolote watakaloambiwa kwa nia ya kuwachukia Viongozi wetu wanaoongoza nchi hii pamoja na bunge linaloendelea, ni wazi hawana nia njema na Taifa letu, machafuko yatakapotokea wao ndio watakuwa wa kwanza kukimbia nchi hii na matokeo yake wananchi wa kawaida ndio watakaopatwa na matatizo. 
Tunamuomba mwenyezi Mungu kuendelea kuulinda Muungano wetu pamoja na Viongozi wetu wakiongozwa na Rais wetu Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete pamoja na Dr. Alli Mohamed Shein

Mungu ibariki Tanzania

……………………………….
SWALEHE OMARY
MWENYEKITI

No comments:

Post a Comment