Pages

Pages

Pages

Saturday 19 April 2014

MELI YAZAMA NA SHEHENA YA SUKARI ZIWA VICTORIA

Watu 10 wamenusurika kufa baada ya meli iliyokuwa imebeba shehena ya sukari kuzama kwenye Ziwa Victoria.

Tukio hilo limetokea jana majira ya mchana katikati ya visiwa vya Karebe na Mubilo wakati meli hiyo inayojulikana kwa jina la FB Matara ilikuwa ikitokea Kagera kuelekea mkoani Mwanza ikiwa na tani 280 za sukari.

Akizungumzia tukio hilo, Mkurugenzi wa Kampuni ya ya Mkombozi Fishing and Marine Transport LTD inayomiliki meli hiyo, Kitara Munaka, alisema kuwa ilipinduka baada ya kuelemewa na upepo mkali.

Alisema meli hiyo ilikuwa imekwenda kuchukua sukari kwenye kiwanda cha Kagera na ilipokuwa ikirejea mkoani Mwanza ilikumbana na upepo mkali ulioambatana na mawimbi makubwa na kusababisha maji kuingia ndani na kupinduka.

Hata hivyo, wafanyakazi 10 wa meli hiyo walifanikiwa kujiokoa baada ya kuchukua boti ndogo zilizokuwa ndani ya meli kwa ajili ya kujiokoa. Alisema kuwa baada ya meli hiyo kuzama kwa saa kadhaa iliibuka ikiwa tupu huku shehena hiyo ya sukari ikiwa imeteketea ndani ya maji.

Boti yenye shehena ya sukari imezama kwenye kisiwa kilichopo katika Ziwa Victoria mkoani Mwanza. Akizungumzia tukio hilo Kamanda wa Polisi Mkoani Mwanza, Valentino Mlowola, alikiri kutokea kwa tukio na kueleza kuwa tayari ameagiza timu kwa ajili ya kufuatilia jambo hilo.

Alisema taarifa kamili juu ya suala hilo bado hajapatiwa hivyo mpaka timu hiyo itakaporejea na kumpatia taarifa. 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment