Pages

Pages

Pages

Wednesday 8 January 2014

ZITTO KABWE AIBUKA KIDEDEA MAHAKAMANI, HAKUNA WA KUMJADILI

Zitto Kabwe
Dar es Salaam. Aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Zitto Kabwe ameshinda maombi yake dhidi ya chama hicho mahakamani.

Katika maombi hayo namba 1 ya mwaka 2014, Zitto ambaye pia ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini, aliiomba Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam kuizua Kamati Kuu (CC) ya Chadema kumjadili au kuchukua uamuzi wowote kuhusu uanachama wake.

Zitto kupitia kwa Wakili Albert Msando alikuwa akiiomba Mahakama itoe zuio hilo la muda hadi kesi yake ya msingi itakaposikilizwa na kutolewa uamuzi.
Katika uamuzi wake jana, Mahakama Kuu ilikubaliana na maombi na hoja za Zitto na kutoa zuio kwa Kamati Kuu ya Chadema na au chombo chake chochote cha uamuzi kumjadili na kutoa uamuzi wowote kuhusiana na uanachama wake, hadi kesi yake ya msingi itakaposikilizwa na kuamuliwa.

Awali, Mawakili wa Chadema wakiongozwa na Mwanasheria Mkuu, Tundu Lissu na Mkurugenzi wa Katiba, Sheria na Haki za Binadamu, Peter Kibatala walipinga maombi hayo wakidai kuwa hayajakidhi matakwa ya kupewa zuio la muda.

Katika uamuzi wake, Jaji John Utamwa alikubaliana na hoja za Wakili Msando kuwa maombi hayo yametimiza matakwa yote ya kupewa zuio hilo.

Matakwa hayo ni pamoja na kuwapo kwa mgogoro baina ya pande mbili, hasara au madhara yasiyoweza kufidiwa na usawa katika athari kwa pande zote.

Jaji Utamwa alikubaliana na hoja za Wakili Msando kuwa iwapo Mahakama haitaingilia kati na kutoa zuio hilo, mtoa maombi ataathirika zaidi kuliko wajibu maombi.

Akijibu hoja ya Wakili Lissu aliyepinga hoja ya mtoa maombi kuathirika pamoja na wananchi wa jimbo lake kwa kukosa uwakilishi bungeni, kuwa hata akipoteza ubunge kwa kuvuliwa uanachama utaitishwa uchaguzi mdogo, Jaji Utamwa alisema uchaguzi mdogo huwa unachukua mchakato mrefu.

Baada ya kurejea vifungu mbalimbali vya sheria, kanuni, amri na uamuzi wa kesi mbalimbali za Mahakama Kuu, Mahakama ya Rufani na za nje, Jaji Utamwa alisema anakubaliana mtoa maombi.

“Kwa hiyo ninatoa zuio la muda kwa Kamati Kuu ya Chadema na au chombo chake chochote cha uamuzi kwamba kisimjadili na kutoa uamuzi wowote dhidi ya mleta maombi kuhusiana na uanachama wake kusubiri kusikilizwa na kuamuriwa kwa kesi yake ya msingi,” alisema Jaji Utamwa.

Kabla ya kufikia uamuzi huo, Jaji Utamwa alitupilia mbali hati ya kiapo kinzani ya Chadema iliyotolewa na Wakili Kibatala baada ya kuwekewa pingamizi na Wakili Msando ambaye alidai kuwa katika hati hiyo, kuna taarifa za kusikia ambazo hakueleza alipozitoa.

http://www.mwananchi.co.tz/habari/Kitaifa/Zitto-aibuka-kidedea-mahakamani/-/1597296/2138132/-/xo1utq/-/index.html

No comments:

Post a Comment