Pages

Pages

Pages

Saturday 4 January 2014

SERIKALI YA TANGANYIKA 2020

Hii ndiyo Bendera ya Tanganyika kabla ya kuungana na Zanzibar

IWAPO muundo wa Serikali tatu utapitishwa na Bunge maalumu la Katiba na baadaye kuridhiwa na wananchi, Serikali ya Tanganyika itaanza kufanyakazi rasmi mwaka 2020. Siri hiyo ilifichuliwa jana na mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Alli Saleh, wakati akizungumza na MTANZANIA Jumamosi, kuhusiana na ujio wa Serikali ya Tanganyika iwapo itaundwa.Mjumbe huyo alisema, Serikali ya Tanganyika iliyokamilika utendaji wake utaanza kuonekana baada ya kumalizika kwa kipindi cha mpito kitakachoanza mara baada ya uchaguzi mkuu wa 2015 hadi mwaka 2018.

“Ukweli baada ya uchaguzi wa mwaka 2015, hakutakuwa na Serikali ya Tanganyika inayoonekana, kwani Serikali ya Tanganyika itakuwa haina wizara wala wafanyakazi.
“Kutakuwa na kugawana ofisi, wafanyakazi na mambo mengine. Mambo haya yatafanyika hatua kwa hatua hadi 2018, hiki ndicho kinaitwa kipindi cha mpito.
“Serikali ya Tanganyika itaanza rasmi 2020 mara baada ya kukamilika kwa kipindi cha mpito ambacho kimewekwa kwa mujibu wa masharti ya mpito kwenye rasimu ya pili ya Katiba Mpya,” alisema.
Baadhi ya masharti yaliyoainishwa katika kipindi cha mpito, chini ya rasimu hiyo kifungu nambari 269 na 270 yanayotajwa kukamilisha muda wa mpito, mojawapo ni kutungwa kwa Katiba ya Tanganyika.
Masharti mengine ni kurekebishwa kwa Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 iweze kuoana na masharti ya Katiba ya Jamhuri ya mwaka 2014, pamoja na kuwapo na mgawanyo wa rasilimali baina ya Serikali ya Muungano na Serikali za nchi washirika.
Masharti mengine ni kutungwa na kurekebishwa kwa sheria mbalimbali za nchi washirika, ili kuwiana na masharti ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 2014.
Mengine ni kuwapo kwa mgawanyo wa madeni baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali za Nchi Washirika pamoja na kufanya uteuzi katika nafasi za madaraka kwa utaratibu ulioainishwa kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 2014.
Masharti hayo pia yanaeleza kuwa kukamilika kwa maoni ya wananchi yaliyokusanywa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba yaliyotumika kuandaa rasimu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka 2014, ambayo yanaweza kutumika kuandika rasimu ya Katiba ya Tanganyika.
Mjumbe mwingine wa tume hiyo, Profesa Mwesiga Baregu akizungumza na MTANZANIA Jumamosi alisema iwapo Bunge la Katiba litapitisha mapendekezo ya kuundwa kwa Serikali ya Tanganyika, itakuwapo fursa nyingine ya kuundwa kwa Tume ya Uchaguzi ya Tanganyika.
Prof. Baregu ambaye ni mtaalamu wa Sayansi ya Siasa nchini, alisema mapendekezo hayo yakipita, katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 kutakuwa na uchaguzi mkuu wa Muungano, uchaguzi wa Tanganyika na Uchaguzi wa Zanzibar.
Prof. Baregu alisema Tanzania hivi sasa inapita katika kipindi cha mpito ambacho si rahisi watu wote wakakubaliana juu ya masuala mbalimbali na muda ukatosha.
“Hakuna ugumu, haya mambo yatafanyika iwapo viongozi watakuwa na dhamira makini itakayowezesha kufanya hivyo na nguvu yetu kubwa tuelekeze kwenye Bunge maalumu la Katiba lifanye kazi yake kwa muda waliopewa.
Prof. Baregu alisema ingawa rasimu ya pili ya Katiba imependekeza kuwapo Serikali tatu, lakini pia imependekeza kipindi cha mpito na masharti ya mpito ikiwamo kufanyika kwa mabadiliko.
Alisema mabadiliko hayo ni pamoja na kupatikana kwa Katiba ya Tanganyika pamoja na kufanyiwa marekebisho kwa Katiba ya Zanzibar, ili ioane na Katiba mama.
“Katika tume sisi hatuna wasiwasi, tulishakusanya maoni yetu bila kujali kitu gani kitatokea, maoni tuliyokusanya yapo tayari kutengeneza Katiba ya Tanganyika, kuna wepesi si kazi ngumu.
“Hapa ni suala la kupanga muda vizuri, Bunge likimaliza kwa wakati wake itafuata kura ya maoni kwa Watanzania na masuala ya kuboresha daftari la wapiga kura, nia ipo na dhamira ipo sina wasiwasi,” alisema Prof. Baregu.


CHANZO: Mtanzania

No comments:

Post a Comment